Imeandikwa na 
Waandishi Wetu
- Imechapishwa: 01 Januari 2016
 
WAKATI makatibu wakuu wateule na manaibu wao wanaapishwa leo Ikulu 
jijini Dar es Salaam, baadhi ya wasomi wamesema uteuzi wao ambao 
ameufanya Rais John Magufuli unalenga kuisaidia nchi iweze kuingia 
kwenye uchumi wa Viwanda.
 
Profesa Emrod Elisante wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) alisema 
kwamba uteuzi huo ni mzuri kwani umezingatia utaalamu zaidi. Alisema 
lazima wizara ziwe na wasimamizi madhubuti ambao wataisaidia nchi kuwa 
yenye viwanda.
“Nikiwaangalia watu kama Dk Chamriho (Leonard, Katibu mkuu Uchukuzi) 
Profesa Mkenda (Adolf, Katibu mkuu katibu Mkuu Biashara na Uwekezaji) 
hawa ni watu makini na ni watendaji wazuri naamini wataisaidia nchi,” 
alisema.
Alisema iwapo watapewa malengo na rais, wana uwezo wa kuyatekeleza 
hasa kuifanya Tanzania iwe sekta ya viwanda kama alivyoahidi Rais 
Magufuli wakati wa kampeni.
Profesa Elisante alisema licha ya nchi kuwa na changamoto mbalimbali 
kama za kifedha na rasilimaliwatu, lakini alisema uteuzi huo umejaa 
wataalamu ambao wengi wamepelekwa kwenye fani zao.
“Unajua hata waliopita ni wazuri, ila tatizo waliingia kwenye siasa, 
Rais Magufuli akiweza kuwadhibiti hawa wasiingie kwenye siasa na 
wakafanya kazi yao kwa weledi na kujua malengo ya wizara na nchi naamini
 tutachomoka,” alisema.
Naye Mwanaharakati za haki za Binadamu, Onesmo Olengurumwa alisifu 
uteuzi wa makatibu wakuu hao kwa maelezo kuwa umewapeleka watu katika 
fani walizosomea.
“Mfano Profesa Mchome (Sifuni ambaye ni Katibu mkuu wizara ya katiba 
na sheria) yule ni mwanasheria aliyebobea naamini ataisaidia nchi kwa 
kutumia taaluma yake,” alisema Olengurumwa.
Alisema kitendo cha Rais Magufuli kujaza wataalamu kama maprofesa na 
madaktari katika Serikali yake kunaonesha kuwa anathamini wataalam hao 
na angependa kuona wanatumia taaluma yao kuisaidia nchi.
“Utakuta katika wizara kwa mfano ya Madini, kuanzia Waziri hadi 
makatibu wakuu ni profesa na daktari, wakikaa pamoja wanaweza kufanya 
vizuri lakini pia wanaweza kufanya vibaya,” alisema Olengurumwa.
Alisema dhamira ya rais ni nzuri, hata hivyo alikosoa wingi wa 
makatibu wakuu hao hasa uteuzi wa manaibu makatibu wakuu kuwa haukuwa na
 maana kwani kila kitengo na idara kina mkurugenzi ambaye kama katibu 
mkuu hayupo anaweza kufanya kazi zake.
“Alipunguza baraza la mawaziri tukafurahi, lakini amerudi nyuma kwa 
kuleta makatibu wakuu wengi tofauti na alivyotangaza kuwa makatibu wakuu
 pia wangepungua, kwa hiyo tuko kule kule,” alisema Olengurumwa.
Naye Katibu Mkuu mteule wa Afya katika wizara ya Afya,Maendeleo ya 
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Mpoki Ulisubisya amesema ameupokea 
uteuzi wake kwa mshituko mkubwa kwa kuwa ni jambo ambalo hakuwahi 
kulifikilia.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi yake ya Ukurugenzi wa
 Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya, Dk Ulisubisya alisema uteuzi wake
 umekuja kwa ghafla huku akiwa na mipango aliyokuwa amejiwekea ya 
kuendeleza hospitali hiyo.
Alisema mawazo yake yote ilikuwa ni kujipanga kuhakikisha anatekeleza
 majukumu aliyokuwa ameachiwa na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya na
 Ustawi wa Jamii majuma mawili yaliyopita, Dk Donan Mbando aliyefanya 
ziara ya kushtukiza katika hospitali hiyo.
Dk Ulisubisya alisema agizo lingine lilikuwa kuhakikisha hospitali 
hiyo inaanzisha Chuo Kikuu kwa ajili ya kuongezea taaluma kwa madaktari 
na kuboresha huduma za dharura na kupunguza foleni kwa wagonjwa, mambo 
ambayo tayari alianza kuyafanyia kazi na kuyawekea mikakati.
Wakati huo huo, leo Rais Magufuli anawaapisha makatibu wakuu na 
manaibu katibu wakuu wa wizara mbalimbali aliowateua juzi. Kazi ya 
kuwaapisha inafanywa leo Ikulu na kwa hatua hiyo, Rais atakuwa 
amekamilisha kazi ya kupata watendaji wa ngazi za juu katika wizara 
mbalimbali, ambazo ni moja ya vyombo vinavyotegemewa kuleta maendeleo ya
 watanzania ikiwa kila mmoja kwa nafasi yake, atatimiza wajibu wake. 
Imeandikwa na Shadrack Sagati, Dar na Joachim Nyambo, Mbeya.