ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Ijumaa, 1 Januari 2016

Magufuli ateua makatibu wakuu 29, manaibu 21

Thursday, December 31, 2015


Rais John Magufuli 
By Mwandishi Wetu, Mwananchi
Rais wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli amefanya uteuzi wa Makatibu wakuu na Manaibu Katibu wakuu wa wizara mbalimbali.
Aidha, Dkt Magufuli pia amemteua Eliakimu Maswi kuwa Kaimu Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na kutengua uteuzi wa Naibu Kamishina wa Mamlaka ya Mapato Tanzania Lusekelo Mwaseba.
Miongoni mwa Makatibu walioteuliwa ni pamoja na nafasi ya Katibu Mkuu Kiongozi, ambaye amebaki Balozi Ombeni Sefue.
Baadhi ya Makatibu waku hao waliochaguliwa ni pamoja na Mhandisi Mussa Iyombewa ameteuliwa katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Ofisi ya Makamu wa Rais anakuwa Mbaraka A. Wakili.
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano waliochaguliwa ni Mhandisi Joseph. Nyamuhanga (Katibu Mkuu – Ujenzi), Dokta Leonard Chamuliho (Katibu Mkuu - Uchukuzi) na Profesa Faustine R. Kamuzora (Katibu Mkuu - Mawasiliano).
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ni Dokta Yamungu Kayandabira, Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ni Maimuna Tarishi.
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wanakuwa ni Dokta Mpoki Ulisubisya atakayesimamia Afya na Sihaba Nkinga - Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Wizara ya Nishati na Madini ni Profesa Justus W. Ntalikwa, Wizara ya Mambo ya Ndani ni Jaji Meja Jenerali Projest A. Rwegasira.
Wizara ya Fedha na Mipango anabaki kuwa Dokta Silvacius Likwelile , Wizara ya Mambo ya Nje, Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa ni Dkt Aziz Mlima. Huku Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa akiteuliwa Job D. Masima.

Maxime amlalamikia mwamuzi


BAADA ya Mtibwa Sugar kupata kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Azam, Kocha Mecky Maxime amemlaumu mwamuzi wa mchezo huo akidai aliwabeba wapinzani wao.
Katika mchezo huo uliochezwa kwenye uwanja wa Azam Complex Chamazi juzi, bao pekee la Azam lilifungwa na John Bocco.
Akizungumza baada ya mchezo huo Maxime alisema mwamuzi Ngole Mwangole ambaye alikuwa akichezesha mchezo huo alikuwa akitafuta namna ya kuipa ushindi Azam.
“Ukiangalia kwa mfano faulo iliyotolewa kwa Azam na Mwangole haikuwa ya haki, wanadai Bocco alitendewa madhambi na Salim Mbonde katika eneo la hatari, lakini ukiangalia halikuwa kosa,” alisema.
Alisema kikosi chake kilicheza vizuri mechi hiyo isipokuwa mchezo uliharibiwa na mwamuzi huyo na kuvuruga baada ya kupata kipigo hicho. Maxime alisema mara nyingi waamuzi wamekuwa wakiharibu mpira hata kama timu imeanza vizuri.
“Timu zote zilicheza vizuri inavyotakiwa lakini refa tu aliharibu mpira, alikuwa anatafuta kitu na ndio alichokifanya kwa sababu mchezaji wangu ndio alianza kushikwa,” alisema.
Alieleza kuwa waamuzi imekuwa tatizo la muda mrefu na wanachangia kuua soka nchini kutokana na kufanya makosa yanayojirudia bila kuchukuliwa hatua yoyote.
Alisema halalamiki kwa kuwa amefungwa kwani ni sehemu ya mchezo isipokuwa afungwe kihalali.

Yanga, Azam kamili kwa Mapinduzi

YANGA na Azam FC zinatarajia kuondoka leo kwenda Zanzibar kwa ajili ya kushiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi inayotarajiwa kuanza keshokutwa mpaka Januari 13 kwenye uwanja wa Amani mjini Zanzibar.
Akizungumza na gazeti hili jana Meneja wa Yanga, Hafidh Salehe alisema timu yao inaondoka na wachezaji wote isipokuwa Nadir Haroub ambaye ni majeruhi. “Mchezaji ambaye hataungana na sisi ni Haroub peke yake ambaye ni majeruhi,” alisema.
Katika michuano hiyo, Yanga imepangwa Kundi B pamoja na Azam FC, Mtibwa Sugar na Mafunzo, wakati Kundi A lina timu za Simba, ambao ni mabingwa watetezi, URA ya Uganda, JKU na Jamhuri ya Pemba.
Yanga watafungua dimba kwa kucheza na Mafunzo keshokutwa, mchezo ambao utafuatiwa na mechi kati ya Mtibwa Sugar na Azam FC usiku. Mabingwa watetezi, Simba SC watateremka uwanjani kwa mara ya kwanza Januari 4, kumenyana na Jamhuri usiku, mchezo ambao utatanguliwa na mechi kati ya URA na JKU.
Nusu fainali zitachezwa Januari 10, wakati fainali itachezwa Januari 13 sambamba na kilele cha sherehe za Kombe la Mapinduzi 2016.

Wasomi wapongeza makatibu wakuu

  Imeandikwa na Waandishi Wetu
WAKATI makatibu wakuu wateule na manaibu wao wanaapishwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam, baadhi ya wasomi wamesema uteuzi wao ambao ameufanya Rais John Magufuli unalenga kuisaidia nchi iweze kuingia kwenye uchumi wa Viwanda.
Profesa Emrod Elisante wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) alisema kwamba uteuzi huo ni mzuri kwani umezingatia utaalamu zaidi. Alisema lazima wizara ziwe na wasimamizi madhubuti ambao wataisaidia nchi kuwa yenye viwanda.
“Nikiwaangalia watu kama Dk Chamriho (Leonard, Katibu mkuu Uchukuzi) Profesa Mkenda (Adolf, Katibu mkuu katibu Mkuu Biashara na Uwekezaji) hawa ni watu makini na ni watendaji wazuri naamini wataisaidia nchi,” alisema.
Alisema iwapo watapewa malengo na rais, wana uwezo wa kuyatekeleza hasa kuifanya Tanzania iwe sekta ya viwanda kama alivyoahidi Rais Magufuli wakati wa kampeni.
Profesa Elisante alisema licha ya nchi kuwa na changamoto mbalimbali kama za kifedha na rasilimaliwatu, lakini alisema uteuzi huo umejaa wataalamu ambao wengi wamepelekwa kwenye fani zao.
“Unajua hata waliopita ni wazuri, ila tatizo waliingia kwenye siasa, Rais Magufuli akiweza kuwadhibiti hawa wasiingie kwenye siasa na wakafanya kazi yao kwa weledi na kujua malengo ya wizara na nchi naamini tutachomoka,” alisema.
Naye Mwanaharakati za haki za Binadamu, Onesmo Olengurumwa alisifu uteuzi wa makatibu wakuu hao kwa maelezo kuwa umewapeleka watu katika fani walizosomea.
“Mfano Profesa Mchome (Sifuni ambaye ni Katibu mkuu wizara ya katiba na sheria) yule ni mwanasheria aliyebobea naamini ataisaidia nchi kwa kutumia taaluma yake,” alisema Olengurumwa.
Alisema kitendo cha Rais Magufuli kujaza wataalamu kama maprofesa na madaktari katika Serikali yake kunaonesha kuwa anathamini wataalam hao na angependa kuona wanatumia taaluma yao kuisaidia nchi.
“Utakuta katika wizara kwa mfano ya Madini, kuanzia Waziri hadi makatibu wakuu ni profesa na daktari, wakikaa pamoja wanaweza kufanya vizuri lakini pia wanaweza kufanya vibaya,” alisema Olengurumwa.
Alisema dhamira ya rais ni nzuri, hata hivyo alikosoa wingi wa makatibu wakuu hao hasa uteuzi wa manaibu makatibu wakuu kuwa haukuwa na maana kwani kila kitengo na idara kina mkurugenzi ambaye kama katibu mkuu hayupo anaweza kufanya kazi zake.
“Alipunguza baraza la mawaziri tukafurahi, lakini amerudi nyuma kwa kuleta makatibu wakuu wengi tofauti na alivyotangaza kuwa makatibu wakuu pia wangepungua, kwa hiyo tuko kule kule,” alisema Olengurumwa.
Naye Katibu Mkuu mteule wa Afya katika wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Mpoki Ulisubisya amesema ameupokea uteuzi wake kwa mshituko mkubwa kwa kuwa ni jambo ambalo hakuwahi kulifikilia.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi yake ya Ukurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya, Dk Ulisubisya alisema uteuzi wake umekuja kwa ghafla huku akiwa na mipango aliyokuwa amejiwekea ya kuendeleza hospitali hiyo.
Alisema mawazo yake yote ilikuwa ni kujipanga kuhakikisha anatekeleza majukumu aliyokuwa ameachiwa na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii majuma mawili yaliyopita, Dk Donan Mbando aliyefanya ziara ya kushtukiza katika hospitali hiyo.
Dk Ulisubisya alisema agizo lingine lilikuwa kuhakikisha hospitali hiyo inaanzisha Chuo Kikuu kwa ajili ya kuongezea taaluma kwa madaktari na kuboresha huduma za dharura na kupunguza foleni kwa wagonjwa, mambo ambayo tayari alianza kuyafanyia kazi na kuyawekea mikakati.
Wakati huo huo, leo Rais Magufuli anawaapisha makatibu wakuu na manaibu katibu wakuu wa wizara mbalimbali aliowateua juzi. Kazi ya kuwaapisha inafanywa leo Ikulu na kwa hatua hiyo, Rais atakuwa amekamilisha kazi ya kupata watendaji wa ngazi za juu katika wizara mbalimbali, ambazo ni moja ya vyombo vinavyotegemewa kuleta maendeleo ya watanzania ikiwa kila mmoja kwa nafasi yake, atatimiza wajibu wake. Imeandikwa na Shadrack Sagati, Dar na Joachim Nyambo, Mbeya.

Alhamisi, 24 Desemba 2015

Pengo kuongoza misa mkesha wa Krismasi


ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Policapy Kardinali Pengo leo saa tatu usiku anatarajiwa kuongoza misa ya mkesha wa sikukuu ya Kuzaliwa Yesu Kristo.
Wakati Wakristo wakifanya mkesha wa Krismasi kote nchini leo, wenzao Waislamu wote nchini leo wanaadhimisha sikukuu ya kuzaliwa Mtume Muhammad (S.A.W), ambapo Kitaifa Baraza litafanyika kwenye Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam kuanzia saa tisa alasiri na mgeni rasmi atakuwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Misa ya mkesha wa Krismasi itafanyika katika makanisa yote yaliyopo jimboni humo na kote Tanzania, lakini kwa Jimbo la Dar es Salaam, Askofu Pengo ataongoza misa hiyo katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph.
Ratiba ya ibada hiyo iliyotolewa na Katibu wa Jimbo hilo, Padri Aidan Mubezi ilisema siku ya Krismasi ambayo ni kesho, Askofu Pengo ataadhimisha misa hiyo katika Kanisa la Mtakatifu Petro lililopo Oysterbay, Dar es Salaam.
Padre Mubezi alisema kuwa misa hiyo itaanza saa 3 asubuhi na kwamba Wakristo wote wanakaribishwa kusali katika misa hiyo. Alisema Askofu Pengo anawatakia Wakristo wote duniani sikukuu njema ya kuzaliwa Kristo na kwamba washerehekee siku hiyo kwa utulivu na amani.
Pamoja na hayo, jimbo hilo kwa kushirikiana na majimbo mengine duniani, wanasherehekee sikukuu hiyo huku wakiadhimisha mwaka wa Huruma ya Mungu uliozinduliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francis.
Alisema katika sikukuu hiyo Wakristo wote hususan Wakatoliki, wanatakiwa kufanya matendo ya huruma kwa watu wasiojiweza ili kupata baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Kwa upande wa Waislamu, baada ya mkesha wa Maulid uliofanyika jana usiku, leo Baraza la Maulid litafanyika kwenye Ukumbi wa Karimjee, huku Mufti wa Tanzania Shehe Abubakar Zuber akiwataka Waislamu kujitokeza kwa wingi katika sherehe hizo.
Mufti Zuberi alisema ujio wa Mtume Muhammad (S.W.A) ni kudumisha amani na hekima ya kumjua Mungu.

Mawaziri wapya wanne wateuliwa

RAIS John Magufuli amemalizia kujaza nafasi za uteuzi wa Mawaziri na Naibu Waziri alizobakiza wakati akitangaza Baraza la Mawaziri la Kwanza katika awamu ya tano ya utawala wake.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, Ikulu, Gerson Msigwa kwa vyombo vya habari, Dar es Salaam jana, katika uteuzi wake Rais Magufuli amemteua Profesa Jumanne Maghembe kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii.
Aidha, Dk Philip Mpango aliyekuwa Kaimu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ameteuliwa kuwa Waziri wa Fedha na Mipango. Amemteua kuwa Mbunge na kumteua pia kuwa Waziri.
Rais Magufuli pia amemtangaza Profesa Makame Mbarawa kuwa Waziri mpya wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, akimhamisha kutoka Wizara ya Maji na Umwagiliaji. Naibu Waziri wa zamani wa Ujenzi, Gerson Lwenge ameteuliwa kuwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji.
Aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ni Dk Joyce Ndalichako ambaye mapema jana aliteuliwa kuwa Mbunge. Dk Ndalichako aliwahi kuwa Katibu Mtendaji wa Baraza na Mitihani la Taifa (NECTA).
Katika uteuzi wake mwingine, Rais Magufuli amemteua Hamad Masauni kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Waziri wake ni Charles Kitwanga. Rais Magufuli, Desemba 9 mwaka huu alitangaza kuunda wizara 18 zenye mawaziri 19. Mawaziri hao na wizara zao kwenye mabano ni George Simbachawene na Angela Kairuki (Ofisi ya Rais-Tamisemi, Utumishi na Utawala Bora) wakati Naibu wa wizara hiyo na Selemani Jaffo.
Wengine ni Mwigulu Nchemba (Kilimo, Mifugo na Uvuvi) na Naibu wake ni William ole Nasha, Jenista Mhagama (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu), Balozi Augustine Mahiga (Mambo ya Nje na Afrika Mashariki). Naibu wake ni Dk Suzan Kolimba.
William Lukuvi (Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi) ambaye Naibu wake ni Angelina Mabula, Ummy Mwalimu (Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto) na Naibu wake ni Dk Hamisi Kigwangalla.
Waziri wa Nishati na Madini ni Profesa Sospeter Muhongo ambaye Naibu wake ameteuliwa Dk Medard Kalemani. Waziri wa Katiba na Sheria ni Dk Harison Mwakyembe na Waziri wa Ulinzi ni Dk Hussein Mwinyi.
Aidha, Nape Nnauye aliteuliwa kuwa Waziri wa Habari na Michezo na Naibu wake ni Anastazia Wambura. January Makamba aliteuliwa Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) na Naibu wake ni Luhaga Mpina.
Katika uteuzi wa awali, Rais Magufuli alimteua Charles Mwijage kuwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Wengine walioteuliwa kuwa Naibu Mawaziri, wakati wizara zao zikisubiri mawaziri kamili ni Edwin Ngonyani (Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano), Ashantu Kijaji (Wizara ya Fedha), Ramo Makani (Maliasili na Utalii) na Stella Manyanya (Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi).
Naibu Waziri mwingine ni Isack Kamwela wa Maji na Umwagiliaji. Wakati huo huo, Katibu Mkuu, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Kidata ameteuliwa kuwa Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA.
“Mbali ya kukamilisha uteuzi wa Baraza lake la Mawaziri, Rais Magufuli pia amewatakia heri Watanzania wote katika Sikukuu za Maulid, Krismasi na Mwaka Mpya na kuwataka washerehekee kwa amani na utulivu,” ilieleza taarifa hiyo ya Ikulu.

KHERI YA SIKUKUU




Nawatakieni watazamaji na wasomaji wa blog hii furaha na amani katika sikukuu hizi za MAULIDI, KRISMASI NA MWAKA MPYA ni matumaini yangu kwamba mwaka tuliouaga ulikuwa ni wa mafanikio na wenye heri na baraka tele bila kusahau changamototulizopata . tumuombe mungu atujarie baraka katika mwaka ujao 2016 uwe na baraka tele na tufanye kazi kwa juhudi zote

happy new year to all.

BY kikot blog managements