ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumapili, 10 Januari 2016

Karibu elimumsingi bila malipo


KAMA Mzazi inapenda kuanza mwaka huu mpya wa 2016 kwa kuwapongeza wote waliobahatika kwa mapenzi ya aliyetuumba kuwa hai na salama na kuendelea kuomba Mungu awalinde kwa mwaka huu tangu mwanzo hadi mwisho wake.
Tunawajibika kushukuru kwa sababu kuna wenzetu hawakubahatika kuuona mwaka huu kutokana na sababu mbalimbali zilizo nje ya uwezo wetu. Lakini kubwa kwa Januari hii ya 2016 ni zawadi ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli kwa wazazi na walezi kwa kuanzisha elimumsingi bila malipo kwa vitendo.
Elimumsingi inajumuisha elimu ya awali,ya msingi na sekondari, kuwa bure kwa gharama za serikali kwa shule za ngazi hiyo zinazomilikiwa na serikali ispokuwa shule 11 tu nchi nzima. Hongera sana serikali ya Rais Magufuli kwa kuishi kwa vitendo.
Kwa mujibu wa waraka wa serikali uliotolewa katikati ya Desemba mwaka jana, uliainisha wazi majukumu ya serikali katika utekelezaji wa elimumsingi bila malipo lakini pia ulioanisha majukumu ya wazazi katika utekelezaji wa jambo hili ili watoto waweze kusoma bila kupata changamoto zisizo za lazima.
Kama Mzazi nataka kuwakumbusha majukumu ya wazazi na walezi katika utekelezaji wa jambo hili kwani yale ya serikali, yenyewe inayajua vilivyo na tayari imeshaanza kutekeleza kwa kutenga fedha za kugharimia elimu hiyo.
Wazazi na walezi kwa mujibu wa waraka wa serikali wanatakiwa kununua sare za shule na vifaa vya michezo,vifaa vya kujifunzia ikiwa ni pamoja na daftari na kalamu, vifaa vya usafi binafsi, chakula kwa wanafunzi wa kutwa na bweni na gharama za matibabu.
Gharama nyingine kwa wazazi na walezi ni kulipia nauli ya kwenda na kurudi shule kwa wanafunzi wa kutwa na wanafunzi wa bweni kwa wakati wa likizo, kununua magodoro, shuka na vifaa vya usafi.
Ili kuhakikisha kwamba hayo yanafanyika bila kuleta manung’uniko kwa kutumbukiza gharama zisizokuwemo katika orodha hiyo, wazazi na walezi wanatakiwa kukemea na kutoa taarifa kwa vyombo husika juu ya mienendo inayokwenda kinyume na utaratibu wa elimumsingi bila malipo.
Kwa uhalisia wake kila mzazi na mlezi anatakiwa kuwa macho kwa kuwa msimamizi wa utekelezaji wa sera hiyo ya serikali ya elimumsingi bila malipo huku watoto wakibakiwa na jukumu la kusoma kwa bidii na uwezo waliojaliwa kwa ajili ya kujipatia ufunguo wa maisha yaani elimu. Visingizio na figisufigisu zisipewe nafasi katika hili ili tuweze kunufaika vilivyo.
Visingizio vya watoto kutokwenda shule kwa sababu ya wazazi au walezi kushindwa kumlipia ada mwanafunzi katika ngazi hizo tatu visipewe nafasi kama ilivyokuwa kabla ya utaratibu huu mpya. Kila mmoja wetu, hususan ni wazazi na walezi wajiandae kwa gharama zilizoorodheshwa ili watoto wetu wote waingie madarasani kwa kazi moja ya kujifunza. Hapa Kazi Tu sasa!

Jumamosi, 9 Januari 2016

Prof. Ndalichako ameipa NECTA siku 7 itoe maelezo kwanini mfumo wa kupanga matokeo kwa GPA ni bora kuliko wa Divisheni uliokuwa unatumika tokea awali.

WAZIRI wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako ametoa siku saba kwa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) limpe sababu za kubadili mfumo wa utunuku viwango vya ufaulu wa awali( Division) na kwenda wa wastani wa pointi (GPA) unaotumika sasa Kidato cha Nne na Sita.

Aidha, ametaka litoe maelezo ya kitaalamu juu ya sababu za kuanzisha mtihani wa pili kwa watahiniwa wa kujitegemea na kwamba zisipomridhisha, mwaka huu wasifanyishwe mtihani huo.

Mfumo wa GPA ulianza kutumika kwa wanafunzi waliofanya mtihani wa mwaka 2014 ambao matokeo yao yalitoka mwaka jana.Vile vile mitihani miwili kwa watahiniwa wa kujitegemea, ilianza mwaka 2014 na 2015.

Ndalichako ambaye aliwahi kuwa Katibu Mtendaji wa baraza hilo kwa miaka tisa, alitoa maagizo hayo jana ambako pamoja na masuala mengine, alishuhudia namna alivyojaribiwa na kuletewa vishawishi jambo ambalo alisema, alilishinda kwa kusimamia taaluma.

Maagizo hayo aliyatoa alipotembelea na kuzungumza na viongozi, wafanyakazi wa NECTA ambako hakuridhishwa na maelezo yaliyotolewa na Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde.

Alisema tangu alipoteuliwa kuwa Waziri, amepokea malalamiko mengi kutoka kwa wadau wa elimu na wananchi juu ya mfumo wa sasa wa upangaji matokeo wa GPA ambao umekuwa haueleweki na kwamba hawakushirikishwa katika mabadiliko hayo.

“ Nataka nijue sababu za kitaalamu za kubadilisha mfumo wa upangaji wa matokeo kutoka kwenye ule wa Division (madaraja) kwenda kwenye ule wa GPA na kama huo mfumo una tija kwa elimu yetu,” alisema.

Awali , Dk Msonde alisema mfumo huo ulipitishwa baada ya vikao kati yake, Tume ya Vyuo Vikuu (TCU), Baraza la Vyuo vya Ufundi (Nacte) na Wizara.

Alisema baraza lilitakiwa kuendesha mfumo huo ili kwenda na mifumo mingine ya elimu ya juu katika kurahisisha udahili wa wanafunzi kwenda sanjari na mfumo wa serikali mtandao na ajira.

Watahiniwa kujitegemea
Kuhusu uanzishwaji wa mtihani wa pili kwa watahiniwa wa kujitegemea, Ndalichako alisema, “Nataka sababu za watahiniwa wa kujitegemea kupewa mtihani wa pili ambao unachukuliwa kama alama upimaji endelevu kwa mwanafunzi.

“ Kama baraza ambalo ndio wataalamu, mnasema mmeamua kutoa mtihani wa pili kutokana na kupokea malalamiko ya kufeli na mtihani mgumu, basi hatuwezi kuendelea nao, nataka nipate sababu za kitaalamu na kama sababu haziridhisha basi mwaka huu wasifanyishwe mtihani wa pili,” alisema.

Alisema kwa kawaida, mtihani wa pili kwa watahiniwa wa kujitegemea hauwezi kuwa mbadala wa alama endelevu kwa wanafunzi. Alisema unaongeza mzigo kwa watahiniwa na gharama za kulipa wasimamizi na wasahihishaji wa mitihani hiyo.

Ashuhudia alivyojaribiwa
Ndalichako aliwataka viongozi wa baraza hilo kutokukurupuka katika kutoa uamuzi na kufanya mabadiliko yasiyo na tija kwa taifa. Badala yake, alisisitiza watumie utaalamu wao kushauri na kukataa maagizo yasiyo na tija kusaidia katika kuboresha elimu.

Katika hatua nyingine, Ndalichako aliwataka watendaji wa Baraza hilo kufanya kazi yao kwa umakini na uadilifu na kuepuka vishawishi. “ Baraza la Mitihani ni sehemu ngumu sana, hasa kutokana na kuhudumia watu na hasa katika suala zima la mitihani.

"Na ni eneo ambalo lina vishwishi vingi, hata mimi nilijaribiwa kuletewa vishawishi lakini nilisimama misimamo ya taaluma,” alisema.

Ndalichako pamoja na kuwapongeza Baraza kwa kutoa vyeti mbadala, ametaka kuwa makini katika suala hilo kuzuia udanganyifu.

Alisisitiza watoe tathmini ya kina katika matokeo ya wanafunzi ambayo yatasaidia wizara kufanya uboreshaji. “Nilipokuwa hapa, kuna wakati nilikuwa nakosa usingizi linapokuja suala la kutangaza matokeo, unakuta matokeo ya wanafunzi 30 yote ni mbaya, sasa hapa si kuwa wanafunzi wote walikuwa hawafundishiki ila kuna tatizo la ziada, na hilo ndio tunatakiwa kushughulikia,” alisema.

Alisema, “ Nilikuwa naumia sana na ubora wa elimu iliyokuwa ikitolewa kwa baadhi ya shule, sasa nimepewa kazi ya kuhakikisha elimu inakuwa bora, tunaondoa watu wa kuchora mazombi na ule wakati wa shule kugeuka vituo vya kulelea watoto badala ya kutoa elimu umefika mwisho.”

Yanga SC yamkuna Pluijm

KOCHA wa timu wa Yanga, Hans Van Pluijm amesema kuwa ameridhishwa na kiwango kinachoendelea kuoneshwa na wachezaji wake katika michuano ya Kombe la Mapinduzi mjini hapa.
Yanga imetinga hatua ya nusu fainali baada ya kumaliza michezo ya makundi wakiwa na pointi saba na kushika nafasi ya kwanza katika msimamo wa kundi A huku Mtibwa Sugar ikishika nafasi ya pili ikiwa na pointi nne.
Akizungumza baada ya kumaliza mchezo baina yake na Mtibwa, Pluijm alisema kuwa wachezaji wake wanacheza kwa jinsi alivyowaelekeza. “Naridhika na kiwango chao hasa kwa vile wanafuata maelekezo yangu na wanacheza vile ninavyotaka wacheze,”alisema.
Hata hivyo, alisema kuwa mashindano hayo ya Kombe la Mapinduzi ni mazuri kutokana na kuwa na ushindani ambao unazidi kuongeza uimara wa timu yake. Katika mchezo huo, Yanga ilishinda mabao 2-1 na mabao yake yalifungwa na Yussuf Abubakar dakika ya 42 na Mwalimi Busungu dakika ya 82, wakati lile la Mtibwa lilifungwa na Shiza Kichuya katika dakika ya 10. I

Magufuli ampa 5 Samatta

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk John Magufuli amemtumia salamu za pongezi mshambuliaji wa Tanzania anayecheza soka la kulipwa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mbwana Samatta kwa kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa Afrika kwa wachezaji wa ndani.
Magufuli alituma salam hizo jana kupitia Wizara ya Habari, Michezo, Utamaduni na Sanaa. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa kwa vyombo vya habari, Dk Magufuli alimtumia salamu za pongezi Waziri wa Wizara hiyo, Nape Nnauye afikishe salamu zake za pongezi kwa Samatta.
“Rais Magufuli amemtaka Waziri Nnauye amfikishie salamu zake za pongezi kwa mchezaji huyo, ambaye pia anaichezea TP Mazembe,” imesema taarifa hiyo ikiongeza kuwa tuzo hiyo imejenga heshima kwa Samatta na Tanzania.
Katika taarifa hiyo, Magufuli amewasihi wachezaji wa soka wote na wadau wa mchezo huo kuongeza juhudi kuuendeleza mchezo ili upige hatua zaidi kimaendeleo. Samatta alitwaa tuzo ya mchezaji bora juzi usiku iliyotolewa na Shirikisho la Soka Afrika (Caf) katika sherehe zilizofanyika Abuja, Nigeria.
Mchezaji huyo alikuwa akipambana na wachezaji wengine wawili ambao ni Robert Kidiaba Muteba (wa TP Mazembe na Congo) na Baghdad Bounedjah (Algeria & Etoile du Sahel).
Samatta alipata pointi 127, mbele ya mchezaji mwenzake wa TP Mazembe, kipa Kidiaba wa DRC aliyepata pointi 88, wakati mshambuliaji wa Etoile du Sahel ya Tunisia na timu ya taifa ya Algeria, Bounedjah alipata pointi 63.
Mchezaji huyo wa Tanzania ameweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza wa Afrika Mashariki kushinda tuzo kubwa ya Afrika. Mafanikio hayo yamekuja baada ya kuiwezesha Mazembe kutwaa taji la tano la Ligi ya Mabingwa Afrika, huku akiibuka mfungaji bora kwa mabao yake manane.
Mshambuliaji wa Gabon, Pierre-Emerick Aubameyang ameshinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Afrika kwa mara ya kwanza na kumshinda Yaya Toure wa Man City na Ivory Coast aliyekuwa akisaka tuzo hiyo kwa mara ya tano.
Aubameyang wa Borussia Dortmund ya Ujerumani mwenye umri wa miaka 26, amewaangusha Toure aliyekuwa anashikilia tuzo hiyo na Andre Ayew wa Ghana. Amekusanya pointi 143, saba zaidi ya Toure wakati Ayew ameshika nafasi ya tatu kwa kupata pointi 112.
Wakati huo huo, Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ametoa pia pongezi zake kwa mchezaji huyo. Naye, Kocha wa Yanga, Hans Pluijm amempongeza Samatta kwa tuzo hiyo akisema kuwa, itawatia moyo wachezaji wengine wa ndani wa Tanzania kubadilika katika mtizamo wa kucheza soka la kulipwa.
“Tuzo hiyo itawafanya wachezaji wengine wa Tanzania kucheza katika kiwango cha juu sio tu katika kujipandisha wao wenyewe, bali kuisaidia timu ya taifa hasa katika mashindano ya kimataifa,” alisema.

Bomoa bomoa iko pale pale

SERIKALI imesema ubomoaji na uondoaji wananchi waishio katika Bonde la Mto Msimbazi utaendelea kwa utaratibu ambao hautaleta mateso na usumbufu kwa wananchi. Watakaohusika na uhamishwaji huo, sasa ni wale tu ambao makazi yao yapo ndani ya bonde, kwenye miteremko ya kuingia bondeni na kwenye kingo za mto.
Imesisitizwa, awamu hii ya ubomoaji, itajikita katika Bonde la Mto Msimbazi tu na watakaokuwa na nyaraka halali walizopewa na mamlaka za umma, zilizowamilikisha na kuwaruhusu kujenga katika bonde hilo, hawatahamishwa bila kupewa sehemu nyingine za kujenga.
Maamuzi hayo yamefikiwa juzi baada ya mawaziri watatu wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI); Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii.
Mawaziri hao walifanya mkutano wa kutathmini uhamishaji wa wakazi wa mabondeni katika jiji la Dar es Salaam. Waliamua kuwa watumishi wa umma waliowamilikisha wakazi maeneo hayo, watachukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria.
Taarifa ya maamuzi hayo ilitolewa jana na Ofisi ya Makamu wa Rais. Pia, taarifa hiyo ilisema mawaziri hao wameamua katika siku tatu zijazo, serikali itaanza kuzoa kifusi na kusafisha maeneo ambapo ubomoaji umefanyika.
Mawaziri hao walibainisha kuwa serikali itaheshimu amri za mahakama kuhusu mapingamizi yaliyowekwa na baadhi ya wakazi wa mabondeni, lakini pia itafuatilia kesi hizo ziishe haraka ili taratibu zinazofuata zifanyike.
“Serikali itawachukulia hatua za kinidhamu watumishi wake wanaoendesha zoezi hili kinyume na misingi ya sheria zinazotekelezwa, na kinyume na misingi ya haki na uwazi, ikiwemo wanaoweka alama za X zaidi ya mita zilizowekwa kisheria,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, serikali imeanzisha dawati la malalamiko katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupokea malalamiko au maswali kuhusu zoezi hilo.
Walisema nyumba na majengo yaliyokuwepo miaka mingi kabla ya kutungwa kwa sheria zinazotekelezwa katika ubomoaji huo hayatabomolewa, isipokuwa tu pale maisha ya wakazi yapo hatarini.
Vile vile ilisema wanaoishi katika makazi hayo, watapewa miongozo ya hatua za kuhifadhi mazingira na kujiokoa na maafa, kwani serikali haina dhamira ya kubomoa hoteli kubwa za siku nyingi zilizo karibu na fukwe katika maeneo ya Masaki. Wamiliki wa hoteli hizo, watapewa masharti na miongozo ya kuhifadhi mazingira kwa mujibu wa Sheria.
Pia, serikali inaweka utaratibu wa karibu zaidi miongoni mwa taasisi zake ili hatua za utekelezaji wa sheria za nchi, zisiwe chanzo cha taharuki katika jamii. “Serikali haina dhamira ya kuwatesa wananchi wake kwa kuwalazimisha kuhama katika makazi yao bila sababu za msingi.
Lakini, pia haiwezi kuruhusu wananchi waendelee kukaa katika maeneo ambayo ikinyesha mvua kubwa maisha yao yapo hatarini,” ilisisitiza taarifa hiyo. Itakumbukwa kwamba katika mafuriko ya mwaka 2011, wananchi 49 waishio mabondeni walipoteza maisha.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Hali ya Hewa, mwaka huu zinatarajiwa kunyesha mvua kubwa kuliko zilizowahi kutokea miaka ya hivi karibuni. Tathmini ya ubomoaji huo iliyotolewa ripoti kwa mawaziri hao, ilieleza kuwa hadi sasa wananchi katika nyumba 774 wamehama na nyumba hizo kubomolewa.
Taarifa hiyo ilieleza pia kwamba kabla ya mkazi kuombwa kuhama, uhakiki kuhusu uhalali wa makazi anayoishi hufanywa. Kutokana na uhakiki huo, jumla ya wakazi 20 walikuwa na hati halali za makazi na wakazi 119 walikuwa na leseni za makazi za muda mfupi, hivyo hawakuhamishwa.
Nchi ina kingo za mito na mabonde na maeneo mengi hatarishi, ambamo watu wanaishi kinyume cha sheria, huku wakiharibu mazingira na kuhatarisha maisha yao, lakini kutokana na uhaba wa makazi, hali ni mbaya zaidi katika mabonde ya jiji la Dar es Salaam, hasa bonde la Mto Msimbazi.
Taarifa hiyo ilisema sababu za kufanya usafishaji wa mabonde na mito katika jiji la Dar es Salaam na mazingira yanayozunguka, unalenga kunusuru maisha ya wananchi wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Eneo la Bonde la Mto Msimbazi, lilitangazwa ni eneo hatarishi kuishi binadamu tangu mwaka 1949 na baadaye 1979, hivyo usafishaji huo utapanua uwezo wa mito ya Dar es Salaam kupitisha maji ya mvua kwa kasi kubwa na kupunguza uwezekano wa kutokea mafuriko na maafa wakati wa mvua nyingi.
Taarifa hiyo ilisema kabla ya nyumba kubomolewa, taasisi zinashirikiana kuhakiki iwapo nyumba anayokaa mkazi ina nyaraka za umiliki na vibali vya ujenzi na iwapo nyaraka hizo zina uhalali wowote.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo nyumba ambazo zimethibitika kuwepo katika maeneo yasiyostahili, ndizo zinawekwa alama X kuashiria kwamba wakazi wanapaswa kuhama au kubomolewa, baada ya hapo mkazi hupewa muda wa kubomoa na kuhama mwenyewe.
“Kutokana na utaratibu huu, sehemu kubwa ya nyumba zinazobomolewa ni zile ambazo watu wamekwishaamua kubomoa wenyewe, baada ya hapo alama huwekwa kuonesha mpaka wa bonde,” ilisisitiza taarifa hiyo.
Pia, taarifa hiyo ilieleza kwamba imebainika sehemu kubwa ya wakazi wa mabondeni ni wapangaji huku wamiliki wanakaa sehemu nyingine salama. Suala la Mchungaji Rwakatare Taarifa ya mawaziri hao pia ilieleza kuhusu suala la Mchungaji Getrude Rwakatare.
Ilisema mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) amefukuzwa kazi Januari 6 mwaka huu na taarifa zake zimekwishafikishwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutokana na tuhuma za kufanya udanganyifu kwa niaba ya Baraza, kwa lengo la kumlinda Mchungaji huyo wa kiroho.
Aidha, Ofisi ya Makamu wa Rais imeshafungua upya kesi mahakamani kuanzia Desemba 29 mwaka jana, kuomba “makubaliano” kati ya mwanasheria huyo wa NEMC na Mchungaji Rwakatare, yawekwe pembeni kwa sababu yalipatikana kwa njia ya udanganyifu.
Taarifa hiyo ilisema Mchungaji Rwakatare amejenga nyumba yake mahali ambapo amezuia mtiririko wa mto kwa kujaza kifusi ili kupata eneo zaidi katika eneo la miti ya mikoko, kinyume na sheria tatu muhimu.
Ilielezwa kwamba tangu wakati ujenzi unaanza, jitihada za kumsimamisha zilifanyika na mamlaka za serikali za mitaa, lakini ikashindikana kutokana na sababu mbalimbali. NEMC ilipoingilia kati na kutaka kubomoa nyumba hiyo, Baraza lilishtakiwa mahakamani na wakati kesi inataka kuanza kusikilizwa, mwanasheria mdogo wa Baraza, yeye mwenyewe bila kuagizwa wala kuwaarifu wakubwa zake, Mei 11 mwaka jana aliingia makubaliano na mawakili wa Mchungaji Rwakatare kwa niaba ya Baraza ya kuondoa kesi hiyo mahakamani na kukubali kwa niaba ya Baraza, kutombughudhi kabisa Mchungaji Rwakatare.
Ilielezwa kuwa makubaliano hayo yalisajiliwa na Mahakama kama hukumu Mei 13 mwaka jana, kisha Mwanasheria huyo alificha makubaliano hayo kwa miezi mitano hadi Oktoba mwaka jana, yalipogundulika na mtumishi mwingine wa Baraza.
Karakana ya Mradi wa Mabasi Yaendayo kwa Haraka (DART) Taarifa hiyo ilisema mkutano wa mawaziri hao, ulielezwa kwamba Sheria ya Mazingira Kifungu 57 (2) inatoa nafasi ya kutolewa ruhusa kwa miradi au shughuli zenye maslahi ya taifa kufanyika katika maeneo ya mabondeni.
Hivyo, waziri mwenye dhamana ya mazingira anaruhusiwa kutoa miongozo ya namna ya shughuli hizo, zinavyoweza kufanyika bila kuathiri mazingira. “Mradi wa DART ulipata kibali hicho na una mkataba na Baraza la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira kuhusu hatua za hifadhi ya mazingira, zinazopaswa kutekelezwa katika mradi huo,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Mawaziri walitaka kufahamu hayo kutokana na hoja inayozungumzwa kwamba wananchi wanaondolewa katika maeneo ya kuishi mabondeni, lakini mradi wa DART umeachwa.

Wasiopeleka watoto shule kuburuzwa kortini Machi


SERIKALI imesema haitosita kuwafungulia mashtaka na kuwapeleka mahakamani ifikapo Machi 30, mwaka huu, wazazi ama walezi wote watakaoshindwa kupeleka watoto wao shuleni ili kupata elimu ya msingi na sekondari.
Aidha, imepiga marufuku kwa jamii kutumia jina la ‘watoto wa majumbani’, badala yake waitwe wasaidizi hao ‘wasichana wa kazi’ au ‘vijana wa kazi’. Hayo yalisemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Dar es Salaam jana.
Alisema hayo ili kuhamasisha wazazi na walezi juu ya watoto kujiunga na shule za msingi na sekondari kwa mwaka huu 2016. Kuhusu kuwafungulia wazazi mashtaka, alisema serikali inaamini kuwa ikiwa inataka kujenga taifa lililoelimika ni lazima kuwekeza kwenye elimu, hivyo ni wajibu wa kila anayehusika kuhakikisha anatimiza wajibu wake.
“Elimu ndio njia bora ya kuwajengea watoto wetu msingi imara wa maisha yao…serikali haitosita kuchukua hatua za kisheria kwa wazazi au walezi ambao watazembea, kumficha, kumtorosha au kuzuia mtoto kuanza masomo ya shule za msingi na sekondari,” alisema Ummy.
Alisema serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, itawafungulia mashtaka na kuwapeleka mahakamani wazazi na walezi wote watakaoshindwa kutimiza wajibu wao wa kuwapeleka watoto shule, kwani hata Sheria ya Mtoto Namba 2 ya mwaka 2009 Kifungu cha 8, inaelekeza kuwa ni wajibu wa mzazi kuhakikisha mtoto anapata elimu.
Waziri Ummy alisema Kifungu cha 14 kinatamka kuwa ni kosa la jinai, kushindwa kutimiza wajibu huo na adhabu yake ni faini isiyozidi Sh milioni 5 na kifungo kisichozidi miezi 6; au vyote kwa pamoja.
Alisema pia wazazi na walezi, wahakikishe kuwa watoto wanaoendelea na masomo ya shule ya msingi na sekondari, wanahudhuria masomo yao kwa ufanisi, kwa kuwa serikali haitarajii kuendelea kuona utoro wa watoto shuleni kutokana na sababu zinazoweza kuepukika.
Kuhusu kuwepo kwa mwitikio mkubwa wa watoto wanaoanza masomo, alisisitiza kuwa wazazi, walezi na jamii kuhakikisha kila mtoto mwenye umri wa kuanza elimu ya msingi yaani darasa la kwanza na elimu ya awali, kujiunga na shule kwa muda uliopangwa na kuhudhuria masomo ipasavyo.
Kuhusu kuwepo kwa michango mbalimbali katika baadhi ya shule wakati huu wa maandalizi ya shule, alisema serikali imeshatoa mwongozo stahiki. Waziri huyo alisisitiza kwamba sio ada peke yake iliyofutwa, bali hata michango yote na tayari serikali imekwishatoa fedha za kugharimia elimu bure na zimekwishapelekwa katika shule zote nchini.
Kwa ujumla, walimu wakuu hawatakiwi kutoza mchango wa aina yoyote, kama vile ya ulinzi, maji, umeme, uzio, fagio, jembe, ndoo na mingineyo, kwani fedha za kugharimia elimu ya bure zitatumika pia kwenye masuala hayo yote

Ijumaa, 1 Januari 2016

Magufuli ateua makatibu wakuu 29, manaibu 21

Thursday, December 31, 2015


Rais John Magufuli 
By Mwandishi Wetu, Mwananchi
Rais wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli amefanya uteuzi wa Makatibu wakuu na Manaibu Katibu wakuu wa wizara mbalimbali.
Aidha, Dkt Magufuli pia amemteua Eliakimu Maswi kuwa Kaimu Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na kutengua uteuzi wa Naibu Kamishina wa Mamlaka ya Mapato Tanzania Lusekelo Mwaseba.
Miongoni mwa Makatibu walioteuliwa ni pamoja na nafasi ya Katibu Mkuu Kiongozi, ambaye amebaki Balozi Ombeni Sefue.
Baadhi ya Makatibu waku hao waliochaguliwa ni pamoja na Mhandisi Mussa Iyombewa ameteuliwa katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Ofisi ya Makamu wa Rais anakuwa Mbaraka A. Wakili.
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano waliochaguliwa ni Mhandisi Joseph. Nyamuhanga (Katibu Mkuu – Ujenzi), Dokta Leonard Chamuliho (Katibu Mkuu - Uchukuzi) na Profesa Faustine R. Kamuzora (Katibu Mkuu - Mawasiliano).
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ni Dokta Yamungu Kayandabira, Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ni Maimuna Tarishi.
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wanakuwa ni Dokta Mpoki Ulisubisya atakayesimamia Afya na Sihaba Nkinga - Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Wizara ya Nishati na Madini ni Profesa Justus W. Ntalikwa, Wizara ya Mambo ya Ndani ni Jaji Meja Jenerali Projest A. Rwegasira.
Wizara ya Fedha na Mipango anabaki kuwa Dokta Silvacius Likwelile , Wizara ya Mambo ya Nje, Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa ni Dkt Aziz Mlima. Huku Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa akiteuliwa Job D. Masima.