ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumatano, 6 Aprili 2016

MWENYEKITI WA CHADEMA MKOA WA IRINGA AFARIKI KWA AJALI .


TANZIA.!
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Iringa Ndg.Sinkala Mwenda amepata ajali jioni ya leo eneo la Tanangozi na kukimbizwa Hospitalini kwa ajili ya matibabu. Lakini amefariki dunia muda mfupi uliopita wakati madaktari wakijitahidi kuokoa uhai wake. Pumzika kwa amani Kamanda Sinkara.!


 https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiURS8unHWqPLjZ7lS8VqDGY7D2FC8WTe3ZeZc4uFUDAy0R4IGJYQ_23W2JrVw1UBD1C67dZXYkU2Sx3k7kpLpA4eVYocaUcTsVpBy19HJZT2r-DF4HV-R1YyDDjVLuTbHxgl8YXLuCRIo/s640/jamiiforums-20160405-0003.jpg

Kocha: Yanga imenoga Pemba

Imeandikwa na Mohamed Akida na Grace Mkojera BAADA ya kuanza kambi ya `nguvu’ kisiwani Pemba, Yanga imetamba ina uhakika wa kupata ushindi mnono Jumamosi wiki hii itakapokutana na Al Ahly ya Misri katika mchezo wa Kwanza wa Raundi ya Pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Akizungumza na gazeti hili jana, Kocha Msaidizi wa Yanga, Juma Mwambusi alisema vijana wake wameiva vya kutosha na ana matumaini makubwa ya kupata ushindi mnono.
Alisema kwa namna ambavyo wachezaji wake wanavyotimiza majukumu yao vizuri kwenye mazoezi Uwanja wa Gombani, ana uhakika ushindi lazima na mashabiki wasiwe na hofu.
“Nafarijika kuona vijana wangu wakitimiza kikamilifu majukumu yao katika mazoezi ambayo tunawapa, kila mchezaji amekuwa akionesha bidii kwa anachotakiwa kufanya, jambo hili linatupa matumaini na kuamini tuna uwezo wa kushinda ingawa ni vigumu kutabiri idadi ya mabao, lakini yatakuwa ya kutosha,” alisema Mwambusi.
Kocha huyo ambaye anamsaidia Mholanzi Hans Pluijm, alisema katika siku tatu zilizobaki kabla ya mchezo huo wamepanga kuwafundisha wachezaji vitu vichache ambavyo ni muhimu vitakavyowapatia matokeo mazuri.
Alisema wanaelekea kwenye mchezo huo wakiwa na furaha baada ya idadi kubwa ya wachezaji wao kuwa fiti kwa ajili ya pambano hilo isipokuwa kiungo Haruna Niyonzima ambaye hatacheza kutokana na kuwa na kadi mbili za njano.
“Ukimtoa Niyonzima, wachezaji wengine wote wapo katika hali nzuri kwa ajili ya mchezo huo, akiwemo Juma Abdul na Nadir Haroub `Cannavaro’…,” alisema Mwambusi na kuwaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi Jumamosi kuwashangilia wakiwa na imani kwamba hawatawaangusha.
Alisema wanataka kushinda ili watakaporudiana ugenini mambo yasiwe magumu zaidi na kusisitiza kuwa ushindi ni lazima kwa mchezo wao.
Zitarudiana wiki ijayo huko Misri. Yanga ilifikia hatua ya raundi ya pili baada ya kuzitoa Cercle de Joachim ya Mauritius katika mchezo wa raundi ya awali kwa jumla ya mabao 3-0 na APR ya Rwanda kwa jumla ya mabao 3-2.
Lakini jana Pluijm (pichani) alikaririwa akisema ushindi katika mchezo huo utategemea na namna wachezaji watakavyojituma na kucheza kama wanavyoelekezwa kutokana na siku za karibuni washambuliaji wake kutengeneza nafasi nyingi za kufunga, lakini wanashindwa kuzitumia.

UPINZANI WAPEWA NAFASI ZANZIBAR


RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ameteua wanasiasa saba kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakiwamo watatu waliowania Urais wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa marudio wa Machi 20, mwaka huu.
Hao ni aliyekuwa mgombea wa nafasi ya urais wa chama cha ADC, Hamad Rashid Mohammed, Said Soud Said aliyewania nafasi ya urais kupitia AFP Wakulima na Juma Ali Khatib wa ADA-TADEA.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu kwa vyombo vya habari, wengine walioteuliwa ni Balozi Ali Karume, Waziri wa zamani wa Fedha na Uchumi katika Serikali ya Rais mstaafu Dk Salmin Amour, Balozi Amina Salum Ali pamoja na Mohamed Aboud Mohamed aliyekuwa Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais.
Pia yumo Mouldine Castico ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Katika hotuba yake ya uzinduzi wa Baraza la Wawakilishi, Rais Shein aliahidi kuunda serikali itakayovishirikisha vyama vya siasa kwa ajili ya kuleta maendeleo ya wananchi wote bila ya kujali itikadi za kisiasa.

Rais Magufuli ziarani Rwanda leo

maguuli 
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Rais Dk. John Magufuli leo anatarajia kuondoka nchini kuelekea Rwanda, ikiwa ziara yake ya kwanza nje ya nchi tangu aapishwe kuingia madarakani Novemba 5, mwaka jana.
Taarifa iliyotolewa jana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, ilieleza kuwa katika ziara hiyo Rais Magufuli na mwenyeji wake Rais Paul Kagame wanatarajia kufungua daraja la kimataifa la Rusumo na kituo cha pamoja cha ukusanyaji ushuru mpakani, ambacho ni moja ya miradi muhimu iliyoanzishwa kwa hisani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Miundombinu hiyo ambayo ipo katika mpaka wa Tanzania-Rwanda, ni muhimu si tu katika kurahisisha mchangamano baina ya nchi hizi mbili, bali pia kuunganisha zaidi ardhi zisizo na bahari katika mataifa ya Afrika Mashariki na Kati na Bahari ya Hindi.
Baada ya sherehe ya ufunguzi, viongozi hao wawili wataelekea mjini Kigali, ambako watafanya mazungumzo pamoja na kuweka shada la maua kuadhimisha kumbukumbu ya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.
Kama mwenyekiti wa sasa wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ziara ya kwanza ya kigeni ya Rais Magufuli katika eneo hilo pia inaashiria dhamira yake ya kupanua mchakato wa uchangamano na kuimarisha uhusiano baina ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo.
Rais Magufuli ambaye staili yake ya kubana matumizi na vita dhidi ya ufisadi, maarufu kama ‘utumbuaji majipu’ imeteka vyombo vya habari duniani, ataanza ziara hiyo ya siku mbili kwa kufungua kituo cha mpakani cha Rusumo.
Baada ya ufunguzi wa kituo hicho cha pamoja cha ukusanyaji ushuru, ambacho kinaunganisha mataifa haya mawili jirani, atafanya mkutano na waandishi wa habari akiwa na mwenyeji wake Rais Kagame.
Katika siku yake ya pili ya ziara hiyo ya kikazi kesho, Rais Magufuli ataungana na Wanyarwanda kote duniani kuadhimisha miaka 22 ya mauaji ya kimbari dhidi ya Watutsi na Wahutu wenye msimamo wa wastani.
Siku hiyo ambayo Wanyarandwa huomboleza vifo vya watu zaidi ya milioni moja vilivyotokea mwaka 1994, wengi wao wakiwa Watutsi, Rais Magufuli na mwenyeji wake Kagame pamoja na wake zao wataweka mashada ya maua na kuwasha mishumaa ya kumbukumbu.
Baada ya tukio hilo, Dk. Magufuli ataungana na Wanyarwanda katika matembezi yajulikanayo kama ‘Walk to Remember’ maalumu kwa kumbukumbu ya mauaji hayo na kuwasaidia walionusurika kabla ya kuhudhuria mkesha kwenye Uwanja wa Taifa wa Amahoro mjini Kigali.
Rais Magufuli amekuwa akitumia muda mwingi akiwa Ikulu Dar es Salaam kwa shughuli za utendaji kazi kwa Serikali yake na alisafiri mara chache nje ya jiji hilo kwenda mikoa ya Dodoma, Arusha, Mwanza, Morogoro, Singida na Geita.

Jumanne, 5 Aprili 2016

Mamlaka ya mji mdogo ILULA na idara ya afya vinara kwa rushwa IRINGA 2015/2016

kikoti blog
WAFAMASIA wawili, mmoja wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa na mwingine wa hospitali ya wilaya ya Mufindi pamoja na watuhumiwa wengine wawili waliokuwa viongozi wa kijiji cha Ilula Mwaya wilayani Kilolo wamefikishwa mahakamani kati ya Januari na Machi mwaka huu wakituhumia kwa makosa mbalimbali ya rushwa.
Akitoa taarifa ya utendaji kazi ya kipindi hicho, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Iringa, Eunice Mmari alisema watuhumiwa hao wanne wamefikishwa mahakamani kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Namba 11 ya mwaka 2007.
Aliwataja wafamasia hao kuwa ni Lucas Mwandi wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa na Selemani Fulano wa hospitali ya wilaya ya Mufindi, na Deogratias Vangiliasas aliyekuwa Mwenyekiti wa kijiji cha Ilula Mwaya na Robert Kisaka aliyekuwa afisa mtendaji wa kijijiji hicho.
Azungumza na wanahabari ofisini kwake jana, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Iringa, Eunice Mmari alisema wafamasia hao wanashitakiwa kupitia kesi namba 53/2016 na kesi namba 39/2016 kwa makosa ya wizi wa mali ya umma wakiwa mtumishi wa umma kinyume na kifungu cha 270 cha sheria ya kanuni ya adhabu iliyorekebishwa mwaka 2002.
Kuhusu waliokuwa viongozi wa kijiji hicho, alisema nao wanashitakiwa kwa makosa ya wizi wa mali za umma kupitia kesi namba 23/2016, kinyume na sheria hiyo ya rushwa kifungu namba 28, 29, 30 na 31.
Mmari alisema katika kipindi hicho cha Januari hadi Machi, Takukuru pia imepokea malalamiko 28 ya rushwa na 14 kati yake yamefunguliwa majadala ya uchunguzi, malalamiko tisa yanafanyiwa uchunguzi wa awali, huku malalamiko matano yakifungwa baada ya kukosekana kwa ushahidi.
Alikitoa mchanganuo wa mamalamiko hayo alisema afya iliongoza kwa kuwa na malalamiko saba, serikali za mitaa, vijiji na kata (6), elimu (3), ardhi (2), sekta binafsi (1), Tanroads (1), Ushirika na Kilimo (2), Polisi (1), Ujenzi (1) na sekta binafsi (2).
Akizungumzia mwamko wa wakazi wa mkoa wa Iringa kuyaripoti matukio ya rushwa katika taasisi yao, Mmari alisema; “mwamko ni mdogo sana ikilinganishwa na mikoa mingine.”
Alisema Takukuru inaamini kuwepo kwa makosa mengi yanayoangukia katika sheria ya rushwa lakini yemekuwa hayaripotiwi katika taasisi yao jambo linalowaathiri wananchi wenyewe na uchumi wa Taifa.
Aliwataka wananchi hao kutoa taarifa kwao wakati wowote wanapokosa huduma baada ya kudaiwa rushwa au pale wanapobaini miradi ya maendeleo katika maeneo yanayowazunguka inafanywa chini ya kiwango.
Kwa kupitia elimu kwa umma, Mmari alisema wananchi 4,957 wamepatiwa elimu ya rushwa katika kipindi hicho, wakiwemo wanafunzi 3,693.
Alisema ofisi yao pia imefanya vikao vinne vya kujadili dhibiti zilizofanyika ili kuziba mianya ya rushwa katika usimamizi wa mali za vijiji, zabuni ya ununuzi wa pampu ya kusukuma maji katika mji wa Mafinga, ajira za vibarua katika mamlaka ya maji Mafinga na taratibu za kuchukua walimu wa kujitolea shule za msingi za mjini Iringa.

vichwa vya habari vya magazeti leo tarehe 05/04/2016.


CUF tutadai haki kwa amani


CHAMA cha Wananchi (CUF) kimesisitiza kuwa kitaendelea na juhudi za kutafuta haki yake kwa njia yoyote, lakini ya amani ambayo itaungwa mkono na wananchi wa Zanzibar na kwa kuanzia wametangaza kutoitambua Serikali itakayoundwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Shariff Hamad aliwataka wananchi na wafuasi wa chama hicho kuwa watulivu katika kipindi hiki ambacho alisema CUF ipo katika juhudi za kutafuta haki wanayodai ilitokana na kushinda katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana ambao ulifutwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).
Maalim Seif alisema hayupo tayari kukaa meza moja na Dk Shein kwa ajili ya kutafuta suluhu ya Zanzibar.
“Sipo tayari kukutana na Shein Ikulu kwa ajili ya mazungumzo ya kuleta amani na utulivu Zanzibar...... nitakutana na yeye kama nani kwa sababu sisi CUF hatutambui ushindi wa Shein katika uchaguzi wa marudio pamoja na serikali yake,” alisema Maalim Seif aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Aidha, Baraza Kuu la CUF limepitisha maazimio ya kuunga mkono uamuzi wa Marekani kuinyima Tanzania msaada kupitia Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) hivi karibuni.
Kwa upande wake, Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimeipongeza Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa juhudi zake ikiwemo kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika juhudi zake za kuleta maendeleo kwa wananchi wake na miradi ya maendeleo.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Serikali ya Watu wa China ni miongoni mwa nchi marafiki makubwa wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mara baada ya nchi mbili kuwa Jamhuri viongozi wake walikuwa marafiki wakubwa wakitembeleana na kubadilisha wataalamu.