ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumanne, 21 Juni 2016

Kesi ya Mauaji ya Mwanahabari, Daud Mwangosi Kuendelea Leo

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhoazFB8bM7gvRXquhdly5-I_1j41gQROJwXeBU3nmM-cKn427Q4PkYRdE2YOWV-U4VPdYYddjjMH1V_RiHMqlfIOic85iNLdbpC_R6-cSPpwiqXZWzA_kANdiwUqktOOh3koENL5QQVJL6/s1600/1.jpg

Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, jana iliahirisha kesi ya mauaji ya mwanahabari, Daud Mwangosi inayomkabili askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Iringa (FFU), Pasificus Simon hadi leo. 
Kesi hiyo iliahirishwa baada ya upande wa Serikali kufunga ushahidi wake. Kesi hiyo iliyoanza kusikilizwa Februari 12, mwaka 2012, leo inaendelea kwa upande wa utetezi kuleta mashahidi wake mbele ya Jaji Paul Kihwelo anayeisikiliza.

Katika kesi hiyo ambayo haikuchukua muda mrefu mahakamani hapo jana, mawakili wa Serikali wakiongozwa na Sandy Hyra na Ladislaus Komanya walisema wamefunga ushahidi kwa mashahidi wanne wa awali.

Baada ya wakili wa utetezi, Rwezaura Kaijage kukubaliana na maombi ya upande wa Serikali kufunga ushahidi wao, Jaji Kihwelo aliiahirisha kesi hiyo hadi leo.

Awali, mtuhumiwa Simon alifikishwa mahakamani hapo akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi ambao hawaruhusi apigwe picha na waandishi wa habari.

Mwangosi aliuawa kwa kupigwa bomu Septemba 2, 2012 katika Kijiji cha Nyololo Wilaya ya Mufindi alipokuwa akiwajibika kwa kazi za kihabari wakati wa ufunguzi wa matawi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Wabunge wa Upinzani Watoka Bungeni Kimyakimya

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEg3bKyzxtKYL76P-vuVlq3rm0ja7lfhYCpwfHC0NAuZlp5ZBmjzib29EDPjzoSqRkwWaHy_zbWtBEsT2m0JM6rQArepqB6Pgrd9sszmGssvheN96loa08SEvql370QYYz8xA-M-xEgGlV9l/s1600/1.jpg
Wabunge wa Ukawa wameendelea kususia vikao vinavyoongozwa na Dk Tulia Ackson, lakini leo wametoka kimyakimya bila mbwembwe kama za jana.

Kwa sasa kamati ya uongozi ya umoja huo imeingia kufanya kikao kujadili mustakabali wao.

Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi), James Mbatia amesema watatoa taarifa kamili baada ya kumaliza kikao hicho.

Marais, maspika wastaafu watwishwa zigo la Bunge



MARAIS wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na maspika wastaafu, wametakiwa kusaidia kutoa ushauri ya namna bora ya uendeshaji wa shughuli za vikao vya Bunge kwa sasa, hususan katika kipindi hiki cha vyama vingi ili wananchi wawakilishwe vyema zaidi kuhusu mahitaji yao bungeni.
Pia Watanzania wametakiwa kufanya maombi maalumu, yenye lengo la kuombea Bunge ili lirudi katika misingi ya awali ya Utanzania kwa kujenga umoja, mshikamano na uvumilivu na kuweka mbele dhamira ya dhati ya kuwawakilisha wananchi katika mahitaji yao na si kutanguliza dhamira za kivyama wakati wa vikao vyake.
Hayo yalisemwa na Paroko wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Paulo wa Msalaba la mjini Dodoma, Padri Sebastian Mwaja wakati wa mahubiri ya ibada za Jumapili zilizofanyika kanisani hapo juzi.
Padri Mwaja alisema Bunge la sasa, linaloendelea na vikao vyake hapa linawanyong’onyesha wengi kwa kushindwa kujikita katika taratibu na desturi nzuri za Kitanzania za kujenga umoja, mshikamano na kuvumiliana katika mambo mbalimbali na badala yake limeshuhudia mvutano, mgawanyiko na kutovumiliana.
“Tunapofanya ufuatiliaji wa hoja za wabunge katika vikao vyake, hatupati kuona ile dhamira ya wazi ya kuwakilisha hoja na mahitaji ya Watanzania wa ngazi za chini ili mahitaji yao yapatiwe ufumbuzi na badala yake tunashuhudia hoja zenye mlengo wa kujipendelea mambo yao zaidi na kuwaacha wananchi na hofu ya kujiuliza endapo kweli dhamira ya kuwatumikia wananchi endapo ni kipaumbile cha kwanza,” alieleza Padri Mwaja.
Alieleza jinsi Bunge linavyojikita katika uvyama na kudhoofisha msingi wa umoja, mshikamano na usawa pamoja na kuvumiliana kama ilivyo tangu awali ambako Watanzania walisifiwa kimataifa kwa sifa hiyo lakini sasa, haipo hivyo, na kushauri juhudi za makusudi lazima zifanyike ili kurudi katika mstari huo mzuri.
Alifafanua kwa undani kwamba kujadili hoja bungeni kwa kuweka mbele dhamira za kivyama, kwa kushuhudia hoja za msingi za kuwatetea wananchi, zikiwekwa pembeni na kuweka mbele dhana ya uvyama, akisema hilo halitasaidia kuwatatulia wananchi kero zao nyingi kama Bunge halitarudi katika misingi ya kizalendo.
Alieleza kusikitishwa na mparaganyiko wa umoja bungeni na kutokuwa na mshikamano katika kuendesha shughuli za Bunge na kutoa mwito kwa marais wastaafu na maspika wastaafu kwa umoja wao kusaidia kulishauri Bunge njia nzuri zaidi ya kurejea katika misingi ya Kitanzania ili tumaini lililojengeka kwenye nyoyo za watu lisififie.
Padri Mwaja alisema wastaafu haswa marais na maspika ni hazina kubwa kwa Taifa, ambao wanaweza kutumika kama kisima cha hekima kwa taifa ili kutoa ushauri bora wa namna ya kurejea katika misingi ya kizalendo ya kitanzania na si kama mambo yanavyoendeshwa bungeni hivi sasa.

Magazeti ya Leo jumanne ya tarehe 21/06/2016




 Pamoja tunasonga na kikoti.com















Jumatatu, 20 Juni 2016

Majibu 10 ya Bajeti yasubiriwa bungeni leo



MAMBO makubwa 10 yaliyojitokeza kwenye mjadala wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/17 pamoja na Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2015, yatajibiwa na kutolewa ufafanuzi leo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango bungeni.
Moja ya mambo hayo ni hoja ya kufuta au kutofuta kodi kwenye kiinua mgongo cha wabunge. Kabla ya Dk Mpango kutoa ufafanuzi na marekebisho ya Bajeti Kuu ya Serikali, kama yatakuwepo na hatimaye kupitishwa au kutopitishwa kwa kupigiwa kura, mawaziri mbalimbali wanatarajiwa pia kujibu baadhi ya hoja zilizoelekezwa kwenye wizara zao.
Kutokana na mjadala wa bajeti uliochukua takribani wiki nzima, wabunge walipendekeza kodi na tozo kadhaa kufutwa ili kuwapunguzia wananchi mzigo, hatua itakayosababisha serikali kuongeza kodi kwenye baadhi ya vitu kama itakubaliana na hoja za wabunge. Moja ya eneo linaloweza kukumbwa na ongezeko la kodi kama serikali kama wanavyopendekeza wabunge ni petroli.
Alipowasilisha Bajeti ya Serikali Juni 8, Waziri Mpango alisema serikali haikuongeza kodi yoyote kwenye petroli na dizeli ili kutowaongezea wananchi mzigo na hofu ya kusababisha mfumuko wa bei.
Kiinua mgongo cha wabunge Wawakilishi hao wa wananchi wamekuwa wakipinga hatua ya serikali kupendekeza kuwakata kodi ya asilimia tano kwenye kiinua mgongo chao wanacholipwa kila baada ya miaka mitano, wakidai kitawaumiza kwa kuwa wao hawalipwi pensheni na kwamba fedha hizo, mbali na kujikimu, zinawasaidia pia katika kuchangia shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii kwenye majimbo yao.
Takwimu zilizopo zinaonesha kwamba mwaka jana Bunge la 10 lilipovunjwa, kila mbunge alilipwa kiinua mgongo cha Sh milioni 230 na kama wabunge watalipwa kiasi kama hicho mwaka 2020, kila mbunge atabakiwa na Sh milioni 218.5 baada ya kukatwa kodi hiyo wanayoilalamikia.
Mbunge wa Nsimbo, Richard Mbogo (CCM), alidai kwamba hatua ya kuwakata wabunge kodi kwenye kiinua mgongo inapaswa kuangaliwa upya kwani wabunge wa Tanzania ndio wanaolipwa mshahara mdogo kulinganisha na wenzao wa Afrika Mashariki.
Alidai kwamba mbunge wa Kenya analipwa Dola za Marekani 11,000, Rwanda Dola 9,000, Uganda Dola 8,000, Sudan Kusini Dola 7,000, Burundi Dola 6,000, wakati wabunge wa Tanzania hulipwa Dola 5,000. Wabunge wanaona pia kama hatua hiyo ni ya kibaguzi wakisema kama serikali imefikia uamuzi huo katika kusaka mapato zaidi, basi ni vyema kodi ya kiinua mgongo iende hadi kwa marais, makamu wa rais, mawaziri wakuu, maspika na naibu spika na wakuu wa mikoa na wilaya.
Mtazamo huu wa wabunge ni tofauti na walio nao wananchi wengi nje ya Bunge wakiwemo wasomi ambao wanaamini kwamba wabunge ambao wamekuwa wakiomba sana maendeleo kwenye majimbo yao, wangekuwa wa kwanza kuonesha utayari wa kuchangia mapato ya serikali kwa kukubali kukatwa kodi hiyo. Hata hivyo, wapo wabunge kadhaa wa CCM na karibu wote wa upinzani wamehiari kukatwa kodi kwenye kiinua mgongo chao.
VAT kwenye utalii Suala la pili lililozungumziwa na wabunge wengi ni kuitaka serikali kuachana na hatua ya kuanzisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya asilimia 18 kwenye huduma za utalii. Wakati akiwasilisha hotuba yake ya Bajeti, Dk Mpango alisema kwamba kodi hiyo ipo pia katika nchi za Kenya, Afrika Kusini na Rwanda. Lakini wabunge katika mjadala walimpa angalizo Waziri kwamba Kenya imeondoa kodi hiyo na bila shaka sababu ni kujikuta wakipoteza watalii wengi.
Walisema kama serikali haitaondoa kodi hiyo basi itegemee mpango wa kuongeza watalii zaidi kutofanikiwa kwani wengi watakimbilia maeneo yatakayoonekana kutokuwa ghali. CAG aongezewe fedha Suala la tatu lililozua mjadala mkubwa ni hatua ya serikali kuipunguzia fedha ofisi ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) kulinganisha na kiwango kilichoombwa wakisema hatua hiyo itaifanya ofisi hiyo muhimu katika kupambana na ufisadi kushindwa kutimiza majukumu yake.
Ofisi hiyo iliomba Sh bilioni 68.8 katika mwaka huu wa fedha ili itekeleze majukumu yake kwa ufanisi lakini katika bajeti inayopendekezwa imepewa Sh bilioni 32.3 pekee. Wabunge walisema ofisi hiyo ni chombo muhimu katika kupeleka ushahidi kwenye Mahakama ya Mafisadi inayotarajiwa kuundwa mwezi ujao hivyo ni lazima serikali ihakikishe utendaji wake haukwamishwi na uhaba wa fedha.
Wabunge pia waliitaka serikali kuongeza fedha kwenye miradi ya maji kwani maji ndio kero kubwa inayowasumbua wananchi wengi na hata wakati wa kampeni, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan alikiri kwamba ndio kilikuwa kilio kikubwa cha wananchi alichokutana nacho. Walitaka serikali iongeze Sh 50 kwenye petroli kwa ajili ya miradi ya maji vijijini sawa na ambavyo imekuwa ikifanyika kwenye mkakati wa kupeleka umeme vijijini ambao kwa kiwango kikubwa umeleta mafanikio.
TRA na kodi ya majengo Lingine lililozua mjadala mkubwa kwenye mapendekezo ya serikali katika bajeti yake ni kuhamisha jukumu la ukusanyaji wa kodi za majengo kutoka katika halmashauri na kupelekwa katika Mamlaka ya Mapato (TRA). Wabunge waliopinga mpango huo walitaja sababu zaidi wakidai taarifa walizonazo ni kwamba hata mpango wa majaribio wa TRA kukusanya kodi za majengo katika mkoa wa Dar es Salaam haukuzaa matunda makubwa.
Waliokubaliana na pendekezo hilo la serikali nao walitoa angalizo kwamba kama hatua hiyo itachukuliwa ni lazina kuwe na utaratibu utakaohakikisha kwamba fedha hizo hazichelewi kupewa halmashauri husika kwa kuwa zimekuwa zikitegemewa sana kwa shughuli mbalimbali. Takwimu za mikoa masikini Lingine lililowagawa wabunge ni kuhusu takwimu za mikoa mitano masikini zaidi nchini na mitano yenye ahueni ambapo baadhi ya wabunge walizitilia mashaka.
Mbunge mmoja alishangaa kuona mkoa wa Mwanza ukiwa miongoni mwa mikoa mitano masikini wakati taarifa ya Benki Kuu inaonesha kwamba mkoa huo ni wa pili katika kuipatia Hazina mapato mengi nyuma ya Dar es Salaam.
Akiwasilisha bungeni Taarifa ya Hali ya Uchumi ya Mwaka 2015, Dk Mpango alitaja mikoa masikini zaidi kuwa ni Kigoma, Geita, Kagera, Singida na Mwanza huku yenye ahueni ikiwa ni Dar es Salaam, Kilimajaro, Arusha, Pwani na Manyara.
Kodi miamala ya simu, mitumba Jambo la saba ambalo wawakilishi hao wa wananchi walitaka serikali iliangalie kwa mapana yake pia ni kodi kwenye miamala ya simu na benki. Hofu ya wabunge ilikuwa kwamba kama kodi hiyo itawekwa bila udhibiti wowote, kampuni, hususan za simu zitahamishia ‘maumivu’ ya kodi hiyo kwa wananchi.
Lingine ambalo wabunge walililalamikia ni Bajeti inayopendekezwa na serikali kupandisha ushuru wa nguo na viatu vya mitumba kutoka Dola za Marekani 0.2 mpaka Dola za Marekani 0.4 kwa kilo. Hatua hiyo ambayo ni sehemu ya makubaliano ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, inalenga kudhibiti mitumba ikiwa ni sehemu ya kujiandaa kwa kuzuia kabisa uingiaji wake.

Kubenea Amshitaki Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhX_Uu0rd3SUKTl3HmU2FuEV8Ie094VQpVONzHzbW2vlmS2djTNJnKfTZvzsw-MGvE0scowzKDy_2ydPJmsVG_IzHK0z0k_zOqYYBtPlQu3kOd24ENWyCsABKSGhX7xFN1H1_sDUfWxEIOw/s1600/1.jpg

Wakati Kamati ya Haki, Maadili na Madara ya Bunge imepokea mashtaka dhidi ya Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson, mbunge mwingine wa upinzani ameamua kumshtaki kiongozi huyo kwenye Kamati ya Kanuni ya Bunge.

Mbunge wa kwanza kumshtaki Dk Tulia, alikuwa Mbunge wa Simanjiro (Chadema), James ole Millya aliyewasilisha kusudio lake kwa Spika wa Bunge hilo, Job Ndugai mashtaka sita na tayari yamewasilishwa kwenye kamati husika.

Mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea alitangaza jana uamuzi wake wa kumshtaki Dk Tulia, ambaye ndiye anayeliongoza Bunge kwa sasa.

Dk Tulia atakuwa na kesi mbili, Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka na kwenye Kamati ya Kanuni.

Dk Tulia anakuwa Naibu Spika wa kwanza tangu kuanza Bunge linalojumuisha wabunge wa upinzani, kushtakiwa kwa madai ya kukiuka kanuni na taratibu za Bunge.

Kubenea alisema ameamua kumshtaki Dk Tulia katika kamati hiyo akidai kuwa alivunja kanuni na taratibu wakati akiwasilisha malalamiko ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuwa mbunge huyo alisema uongo bungeni.

Akizungumza na wanahabari, mbunge huyo alisema hakuridhishwa na hatua ya Dk Tulia aliyoifanya Mei 13 na kwamba tayari alishawasilisha barua yake yenye hoja tano za mapungufu ya kikanuni kwa Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah tangu Ijumaa iliyopita.

Kubenea alieleza kuwa Dk Tulia alitumia kanuni ya 71 kupokea malalamiko ya Dk Mwinyi kinyume na utaratibu kwa kuwa kanuni hiyo huruhusu watu wasio wabunge kupeleka malalamiko yao kwa Spika, iwapo masuala yaliyojadiliwa bungeni yamewaathiri.

Alisema wakati akichangia hoja ya wizara hiyo Mei 10, alimtaka Dk Mwinyi aeleze juu ya kuwapo kwa mkataba baina ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na Kampuni ya Heinan Guoji Industry & Investment Limited na kama upo haoni kama kuna mgongano wa masilahi kutokana na kushiriki kumjengea nyumba yake.

Hata hivyo, alidai hakuna mbunge aliyesimama kudai hoja hiyo ilikuwa ya uongo kama kanuni ya 63(3) inavyotaka, badala yake siku tatu baadaye alitakiwa kufuta bungeni jambo ambalo anaona Dk Tulia hakumtendea haki.

“Naibu Spika wakati akitoa mwongozo wa Spika alinukuu sehemu tu ya maelezo yangu jambo lilipotosha misingi na mantiki ya mchango wangu bungeni hivyo kuashiria alikuwa na nia mbaya dhidi yangu,” alisema Kubenea na kuongeza: “Hata nilipoomba kufanya hivyo siku aliposoma mwongozo na kunipa nafasi ya kufuta maneno yangu au kuyathibitisha, alikataa na endapo angezingatia mchango wangu wote angetenda haki.”

Katika barua hiyo, Kubenea amelalamika kuwa wakati Dk Tulia anapokea malalamiko kutoka kwa Dk Mwinyi hakumpelekea nakala ili kurahisisha utetezi wake.

Pia, alieleza kuwa Naibu Spika aliamua kimakosa kuwasilisha tuhuma dhidi yake kwenye kamati hiyo bila kuzingatia maelezo aliyowasilisha kwake na vielelezo huku akijua Waziri huyo wa ulinzi alikiuka kanuni ya 63 (3) na 64(2).

Kubenea alisema anaiomba Kamati ya Kanuni yenye nguvu kuliko Spika kusimamisha mchakato unaoendelea kufanywa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge juu ya suala lake hadi pale itakapofanya uamuzi iwapo ilifuata kanuni ama la.

Katika barua hiyo, Kubenea anamuomba Dk Kashililah amjulishe Spika ili aweze kuitisha kikao cha Kamati ya Kanuni kwa mujibu wa kanuni ya 5(5) ili kuona kama kulikuwa na uhalali wa shauri lake na anaamini Katibu huyo wa Bunge atamtendea haki.

Kubenea alishahojiwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge Alhamisi iliyopita na kueleza kuwa alikubali kufanya hivyo kwa kuwa kamati hiyo ina nguvu kubwa ya kikanuni ikiwamo kukamatwa.

Kubenea alisema hana wasiwasi na aliyoyasema ila anataka haki itendeke kwa kufuata kanuni na hadi sasa ana vielelezo vya kutosha kuhusu suala lake.

Dk Kashililah alieleza jana kuwa hawezi kuzungumzia kwa kina jambo hilo kwa kuwa taratibu zote za kufuata zinafahamika.

 “Inawezekana ameandika, lakini mpaka ifike tuipokee. Mimi nilikuwepo Ijumaa hadi saa tano usiku sikuiona. Huenda ipo njiani ikifika tutaipokea na tutaifanyia kazi,” alisema Kashililah.

Serikali Yasitisha Ajira Zote Kwa Muda

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjAIrlBPh9sm_M79kyqv0Z_oAbm_aBjaIjuL7VzcBegpJsUB0GMWOFzBu9g_SZFQLez-Q-PM1odxbdz4k2CFtp8gIqPpTMoWaZ72MyOtiSeKIW1HKrnTt0oD5kFXUg7CMf3k4Y4y0DnnHI9/s1600/1.jpg

SERIKALI imesitisha ajira zote, kama njia ya kukabiliana na wimbi la watumishi hewa.

Kutokana na uamuzi huo hivi sasa hakuna nyongeza ya mishahara kwa watumishi wa Serikali na wakala zake pamoja na utoaji wa vibali wa likizo ya bila malipo.

Katibu Mkuu Utumishi, Dk. Laurean Ndumbaro,  jana alisema kuwa Serikali imesitisha kwa muda utoaji wa ajira, ili kupitia upya muundo wa Serikali na taasisi zake.

Alisema utekelezaji wa mkakati huo utakwenda sambamba na kusitisha kwa muda utoaji wa vibali vya ajira zote mbadala pamoja na uidhinishaji wa ajira hizo zilizopo Sekreterieti ya Ajira katika utumishi wa umma na kwenye mfumo wa taarifa za kiutumishi.

“Ni kweli tumesitisha kwa muda ili kupitia mfumo wa Serikali na hata kuangalia ulipaji wa mishahara kama upo katika malipo stahiki.

“…na hili litakwenda sambamba na hata kusitishwa malipo ya mishahara yanayotokana na upandishwaji wa vyeo kwa watumishi. Tukimaliza zoezi hili ndipo tunaweza kuanza kutoa ajira za Serikali,” alisema Dk. Ndumbaro.

Alisema muundo mpya wa utumishi wa Serikali unakwenda sambamba na uhakiki wa malipo ya mishahara, hivyo ni lazima ujue ni nani unayemlipa kuliko ilivyo sasa.

Kwa mujibu wa maelekezo hayo uhamisho na uidhinishaji katika mfumo wa watumishi ambao wamehamishwa kutoka kwa mwajiri mmoja kwenda kwa mwajiri mwingine ambao atalipwa mshahara mkubwa kuliko ule wa sasa pia utaangaliwa kwa lengo la kupata taarifa sahihi za mtumishi husika.

“Baada ya kukamilika kwa zoezi la uhakiki watumishi pamoja na tathmini ya muundo wa Serikali na taasisi zake, wote wataarifiwa ni lini utekelezaji utaendelea,” alisema.

Taarifa kutoka maeneo mbalimbali nchini, zinaarifu kuwa maelekezo hayo yalitolewa Juni 13, mwaka huu na kusambazwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo kwa makatibu wakuu wote, makatibu tawala wa mikoa, kwa wakuu wa idara za Serikali zinazojitegemea.

Waliotakiwa kutekeleza maelekeo hayo ya Serikali ni wakurugenzi wote wa majiji, manispaa na miji, wakurugenzi watendaji wa halmashauri za wilaya, watendaji wa taasisi za umma na watendaji wa wakala za Serikali kwa upande wa Tanzania Bara.

Kamatakamata
Wiki iliyopita vyombo vya dola vilianza kuwatia mbaroni watumishi hewa kwa kuwafuata na pingu majumbani.

Hatua hiyo imetajwa kuwa ni mkakati wa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Magufuli, kuanza kupambana na watendaji ambao wamekuwa wakiisababishia hasara Serikali ya kulipa mamilioni ya shilingi kwa watumishi hewa.

Kutokana na uamuzi huo  ambapo mtumishi mmoja wa moja  za Mkoa wa Kigoma, alifuatwa na askari wa polisi na kutiwa mbaroni nyumbani kwao Ubungo Kibangu jijini Dar e Salaam.

Tukio hilo la aina yake lilitokea mchana wa juzi na kuibua hisia miongoni mwa majirani ambao waalisema kuwa, askari hao walifika nyumbani kwao na mtumishi huyo na kumfunga pingu mikono na miguuni na kuondoka naye.

Kutokana na hekaheka hiyo ya watumishi hewa, taarifa kutoka wilayani Nyasa mkoani Ruvuma, zilidai kuwa walimu watano wastaafu nao walikamatwa na polisi kwa madai ya kupokea mishara hewa.Mbali na walimu hao pia alikuwepo muuguzi mmoja.

Hivi karibuni akizungumza Dar es Salaam, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki, alisema Serikali imewaondoa jumla ya watumishi 12,246 kwenye mfumo wa malipo ya mishahara kwa sababu mbalimbali, ikiwemo umri wa kustaafu kwa lazima, kufukuzwa kazi, vifo na kumalizika kwa mikataba.

Waziri Kairuki alisema kuondolewa kwa watumishi hao kumeokoa Sh bilioni 25 ambazo zingelipwa kwa watumishi hao.

Alisema kuwa fedha hizo zingepotea endapo watumishi wasingeondolewa kwenye mfumo, ikilinganishwa na watumishi 10, 295 walioondolewa kwenye mfumo kuanzia Machi 15 hadi Aprili 30 mwaka huu.

Alisema pia kuwa watumishi hewa 1,951 wameongezeka ikiwa ni pamoja na Sh bilioni 1.8.

Alifafanua kuwa ofisi hiyo ilitoa maelekezo kwa Makatibu Wakuu, Wakuu wa taasisi za umma na Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuwasilisha taarifa ya watumishi hewa ifikapo Juni 10, mwaka huu. 
Chanzo: Mtanzania