ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Ijumaa, 1 Julai 2016

Yanga hatarini kuadhibiwa Caf

Imeandikwa na Vicky Kimaro
KLABU ya Yanga huenda ikaondolewa kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho inayoendelea baada ya vurugu kubwa ikiambatana na mabomu kurindima katika mchezo wao na TP Mazembe uliofanyika Jumanne iliyopita Juni 28, kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
Katika mchezo huo ambao Yanga ilitangaza kiingilio bure, ulifurika mashabiki zaidi ya 60,000 ingawa walitakiwa kuhakikisha mashabiki wao wasizidi 40,000 na Kamisaa wa mchezo ambaye aliwatadharisha Yanga iwapo watu watazidi, basi angeufuta mchezo huo.
Hata hivyo, vurugu zilizozuka zilisababisha uharibifu wa mali za uwanja ikiwemo kuvunjwa kwa mageti na viti ndani ya uwanja huo wa taifa ambao kwa sasa zinafanyika tathmini ya uharibifu huo na Yanga watalazimika kulipa.
Juni 18 mwaka huu, CAF iliitoa Entente Setif ya Algeria katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa wa Afrika baada ya vurugu za mashabiki na kuipa ushindi Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.
Agosti 2011, wawakilishi wa Tunisia kwenye michuano hiyo ya klabu bingwa, Etoile du Sahel waliondolewa mashindanoni baada ya mashabiki wake kufanya vurugu kwenye mechi ya hatua ya makundi.
Adhabu hiyo huenda ikaikumba pia Yanga, na jana Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alisema Yanga wakiwa na wawakilishi wao katika mkutano wa maandalizi wa Alhamisi Juni 23 kwenye Ukumbi wa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam walitangaza juu ya kuchapisha tiketi 40,000 na wakatangaza na viingilio.TFF baada ya kikao hicho iliwajulisha CAF juu ya jambo hilo kama ilivyo ada.
Mkutano wa kawaida wa maandalizi ya mechi (pre-match meeting) baina ya timu zote mbili,yaani Yanga na TP Mazembe ulifanyika Juni 27 katika ukumbi wa hoteli ya Coral Beach, Masaki jijini Dar es Salaam na uliendeshwa na Mratibu Mkuu wa CAF wa mchezo huo, Sidio Jose Magadza – Raia wa Msumbiji, ambapo katika kikao hicho, Yanga walitamka kuwa mchezo wao utakuwa bure.
Malinzi alisema kuwa msimamizi wa CAF alikiambia kikao kuwa kama hayo ndiyo maamuzi ya Yanga watambue kuwa itakuwa ni kwa gharama zao.
Aidha, aliagiza watazamaji 40,000 tu ndio waruhusiwe kuingia uwanjani hata kama ni bure, hii ni kwa sababu za kiusalama, “Hilo halikufanyika na badala yake uwanja ulijaa watu 60,000 na kutokana na pilika pilika za watu kutaka kuingia uwanjani zilitokea vurugu, ambazo zilisababisha wana usalama kutumia nguvu. “Hili nalo lilishuhudiwa na wawakilishi wa CAF na hatujui wameripoti vipi tukio hili, ikumbukwe wajibu wa TFF, CAF na FIFA ni kuhakikisha mashindano yao yanafanyika kwa utulivu na amani bila kuathiri maisha ya watu, mali zao na miundombinu ya michezo,”alisisitiza Malinzi.
Alisema kutokana na suala hilo TFF inafuatilia kwa karibu kujua nini yatakuwa maamuzi ya CAF baada ya ripoti za msimamizi na kamisaa wa mchezo kuhusu matukio yaliyotokea nje ya uwanja kabla na wakati wa mechi.
“Siku zote TFF imekuwa ikifanya kila jitihada kuhakikisha mchezo wa mpira unachezwa katika eneo salama, hivyo kuanzia sasa jukumu la kusimamia michezo ya kimataifa litakuwa linaratibiwa kwa karibu zaidi na TFF, ikiwa ni pamoja na mapokezi ya timu.” “Kingine litakachoratibiwa na TFF ni kuwapokea maofisa, kuangalia malazi kama yako sahihi, usalama, maamuzi kuhusu viingilio na uuzaji wa tiketi, usafiri wa ndani, viwanja vya mazoezi.”
Alisema mamlaka ya TFF katika mashindano ya ndani na ya kimataifa ni pamoja na usimamizi wa maandalizi ya mchezo, usimamizi wa mapato,usimamizi na uhakiki wa haki za matangazo, usalama ndani na nje ya uwanja, usimamizi wa upelekaji taarifa CAF na FIFA.
Alisema kwa yeyote anayetaka kucheza mpira unaotambuliwa na FIFA, CAF, CECAFA na TFF ni sharti akubaliane na kutii mamlaka hizo. Kauli hiyo ya Malinzi imekuja, ikiwa ni siku moja baada ya uongozi wa Yanga kudai kuwa hailipi chochote kwa TFF wala CAF na badala yake italipa gharama za uwanja na ulinzi pekee kwa kuwa hawajaingiza mapato yoyote katika mchezo huo, ambao waliingiza mashabiki bure.
Katika mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa na Yanga kunyukwa bao 1-0, wametakiwa kulipa makato yote yanayohitajika, ikiwemo asilimia tano ya makato za CAF, asilimia 10 gharama za mchezo, nyingine gharama ya uwanja asilimia 15, TFF asilimia tano, Baraza la Michezo la Taifa (BMT), asilimia 10, DRFA asilimia tano pamoja na makato ya TRA asilimia 18.
Tayari Yanga ilikuwa imechapisha tiketi 31,000, ambazo zingeuzwa Sh 7,000 ambazo zingeingiza Sh 217,000,000 huku zile za Sh 25,000 zilikuwa zimechapishwa tiketi 8,200 zilitarajiwa kuingiza Sh milioni 205 huku VIP zilikuwa tiketi 5,000, ambazo zingeingiza Sh milioni 150.
Jumla ya fedha zote ambazo zingepatikana katika mchezo huo zilitarajiwa kuwa Sh milioni 572. Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdetit alisema jana kuwa hawapo tayari kulipa fedha hizo kwa vile mchezo ulikuwa bure na kwamba watalipa gharama za uwanja, ulinzi na Msalaba Mwekundu pekee, CAF, TFF na makato mengine wawasemehe.
Kwa mujibu wa kanuni za CAF, katika hatua ya makundi shirikisho la soka la nchi husika inalazimika kuilipa CAF dola 2,000 sawa na Sh 420,000 katika mauzo tiketi ya mechi za makundi.
“Sasa tiketi hatujauza, watu wameingia bure hizo fedha za kulipa TRA, CAF, TFF na wengineo zingepatikana kwenye mapato, tulimuliza mratibu wa CAF kuhusu kuingiza watu bure akasema ni sahihi, kwa hiyo watusamehe tu,” alisema Baraka.
Hata hivyo, kwa upande wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), umesema kuwa wanachofahamu Yanga walichapisha tiketi 40,000 na taratibu wanazijua na walielezwa sasa kama wao wanasema hawalipi, basi hatua za kisheria zitachukuliwa.
Aidha, Malinzi amewaangukia mashabiki wa mpira kwa kuwaomba radhi kwa kadhia yote iliyotokea kutokana na kitendo cha klabu hiyo ya Jangwani kuruhusu watazamaji kuingia bure na kusababisha vurugu. Malinzi amevishukuru vyombo vya vya ulinzi na usalama kwa hatua walizochukua ili kuepusha maafa, ambayo yangeweza kutokea.

Mjadala wa Sakata la Lugumi WAZIKWA Rasmi.......Naibu Spika Aipa Serikali Miezi Mitatu

Kiu ya wabunge kujadili sakata la utekelezwa mbovu wa mkataba baina ya Jeshi la Polisi na kampuni ya Lugumi Enteprises Limited, imezimwa baada Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kuiagiza Serikali kukamilisha utekelezaji wa mradi huo ndani ya miezi mitatu ijayo. 
Kwa muda mrefu, wabunge walikuwa wakisubiri ripoti ya uchunguzi kutoka Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (PAC) ili waweze kujadili kwa kina sakata hilo linalohusisha mradi wa Sh37 bilioni wa kufunga vifaa vya kielektroniki vya kuchukua alama za vidole (AFIS). 
Mapema Aprili mwaka huu, wakati PAC ikipitia taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka ulioshia Juni 30, 2014 ilibaini kuwa Lugumi ilikuwa imefunga mashine katika vituo 14 tu kati ya 108 ilivyotakiwa kuvifunga wakati ikiwa imeshapokea asilimia 99 ya malipo yote.
 PAC ilimuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani apeleke taarifa ya utekelezaji wa mradi huo ambayo aliipeleka Aprili 18 na kubaini kuwa vifaa hivyo vilifungwa katika vituo 153 pamoja na makao makuu ya polisi. 
Kutokana na utofauti wa takwimu za CAG na PAC iliunda kamati ndogo kufanya uhakiki wa vifaa vya AFIS na sababu za kuchelewa kutekelezwa kwa mradi, huku wengi wakitarajia ripoti hiyo ingejadiliwa bungeni. 
Katika sakata hilo, wabunge walimtuhumu aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Charles Kitwanga kuwa na masilahi kwa madai kuwa alikuwa mmoja wa wanahisa wa kampuni ya Infosys iliyoshirikishwa kwenye mradi huo na kushinikiza ajiuzulu kupisha uchunguzi. 
Hata hivyo, Kitwanga alitimuliwa kazi kwa kosa jingine la kuingia bungeni kujibu maswali ya wizara yake akiwa amelewa. 
Jana, Dk Tulia alitumia kanuni 117(17) kukabidhi matokeo ya uhakiki huo kwa Serikali, yakiwemo maoni, ushauri, mapendekezo ya namna ya kutatua changamoto zilizoanishwa na taarifa ya kamati ya PAC na kutoruhusu mjadala kwa wabunge
Dk Tulia alieleza kuwa amefanya uamuzi huo baada ya kupokea taarifa hiyo na kuangalia maudhui yake, kuzingatia matokeo ya uhakiki huo uliofanywa na kamati ndogo na PAC kujiridhisha uwepo wa vifaa hivyo, ukiacha kasoro zilizojitokeza. 
Pia, alisema suala hilo si jipya kwa kuwa linatokana na hoja ya ukaguzi wa miaka ya nyuma na kilichokuwa kimebaki ni vifaa hivyo kufanya kazi.

“Naagiza sasa kwamba Serikali ihakikishe mfumo huu unafanya kazi ndani ya miezi mitatu kuanzia leo (jana) ili kuboresha uwezo wa Jeshi la Polisi kuwa na utambuzi wa haraka wa wahusika wa matukio ya kihalifu katika vituo vyote nchini,” alisema huku akishangiliwa. 

Dk Tulia aliitaka pia Serikali kuyapatia ufumbuzi haraka masuala yote yaliyobainika kuwa na dosari za kiutendaji. 
Alisema ameielekeza kamati ya PAC kuhakiki maagizo aliyoyatoa kwa Serikali na baada ya uhakiki huo itoe taarifa bungeni wakati ikiwasilisha taarifa yake ya mwaka. 
“Natarajia kuwa suala hili sasa litafikia mwisho na CAG atafunga hoja yake baada ya kujiridhisha na utekelezaji wa maagizo niliyoyatoa,” alisema Dk Tulia. 
Mwenyekiti wa PAC, Aeshi Hilaly alisema walishamaliza kazi yao baada kumkabidhi Naibu Spika ripoti hiyo, kama kanuni zinavyotaka na kwamba yeye ndiye mwenye uamuzi wa mwisho. 
Aliyekuwa mwenyekiti wa kamati hiyo ndogo ya kuchunguza suala hilo, Japhet Asunga alisema baada ya uchunguzi, walibaini vituo 15 tu kati ya 153 ndivyo vimeunganishwa na mfumo wa taarifa za polisi. 
Asunga, ambaye ni mbunge wa Vwawa (CCM), alimwambia mwandishi wetu kuwa kamati ilibaini kuwa vifaa vyote vya AFIS vilivyokuwapo katika vituo vimetelekezwa bila kuunganishwa katika mfumo wa mtandao.
Alisema sehemu nyingine walikuta vifaa vimetupwa huku vingine vimeharibika kwa sababu vimekaa muda mrefu kama wino wa printa umeisha muda wake. 
“Tumeagiza Serikali ichukue hatua stahiki kuhakikisha vifaa vinatumika na kuwaadhibu wote waliochelewesha na nani hakufanya kazi ipasavyo.
“Ndiyo maana Naibu Spika baada kupima maagizo yaliyotolewa ameona Serikali ianze kuyafanyia kazi mapungufu badala ya kusubiri kuyawasilisha Septemba. Naona busara imetumika,” alisema Asunga. 
Alisema kamati haina tatizo na maazimio ya miezi mitatu aliyotoa Spika kwa kuwa ndiyo mapendekezo yao na kwamba PAC wao awali walipendekeza miezi sita.

Kodi ya Miamala ya Tigopesa, M-Pesa, Benki na Airtel Money kuanza Kutozwa Rasmi Leo


Leo ndiyo mwanzo wa utekelezaji wa Sheria Fedha (Finance Act, 2016) iliyopitishwa katika Bajeti ya 2016/17 ambapo Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) itatozwa katika huduma za mitandao ya simu, benki na taasisi za fedha.

Akisoma hotuba ya bajeti bungeni hivi karibuni, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango pamoja na mambo mengine, alipendekeza kuongeza kodi hiyo katika huduma za  kibenki zinazotozwa na benki hizo ili kupanua wigo wa kodi isipokuwa riba kwenye mikopo.

Vilevile, Waziri Mpango alieleza azma ya Serikali kutoza ushuru wa bidhaa wa asilimia 10 kwenye ada zinazotozwa na watoa huduma katika kutuma na kupokea fedha badala ya ushuru huo kutozwa tu kwenye kutuma fedha pekee.

Akizungumzia uamuzi huo, mtaalamu wa kodi wa kujitegemea, Deogratias Peter alisema ongezeko hilo litawakatisha tamaa wateja wa benki na watumiaji wa miamala ya simu.

“Kwa zaidi ya miaka 10 sasa, Serikali inafanya jitihada za kuongeza watumiaji wa benki kwani katika nchi za Afrika Mashariki ilikuwa nchi ya nne mbele ya Burundi kwa kuwa na idadi ndogo ya watu wanaotumia benki. Lakini hatua hii inaweza kurudisha nyuma jitihada hizo,” alisema Peter.

Alisema Serikali ilianzisha utaratibu wa Saccos, Vicoba na kulegeza masharti ya kuwa na akaunti ya benki ili kuwawezesha wananchi wa kawaida kumudu kuweka fedha kwenye taasisi za fedha na ilianzisha Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB), Benki ya Wanawake Tanzania (TWB), wakala wa benki na miamala ya simu ili kuongeza watumiaji wa benki.

“Watanzania wengi wasio na utamaduni wa kuweka fedha benki watakubali kukatwa fedha zao kiasi hicho?” alihoji.

Alisema mfumo huo kwa sasa haueleweki hasa kwa watumiaji wa miamala ya simu kwa kuwa mawakala wake hawatoi risiti kama ilivyoagizwa na Serikali.

Aliongeza kuwa hata katika mashine za ATM, hakuna mashine za kukata kodi ya VAT hivyo hakuna maandalizi ya kukokotoa kodi hizo.

Mkurugenzi wa Elimu na Huduma kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Richard Kayombo alipoulizwa kuhusu makato hayo, asisitiza azma ya Serikali kukusanya mapato kwa njia yoyote ile, bora tu iwe ni ya kisheria.

“Sina tafsiri yoyote ya kodi hiyo. Sisi kazi yetu ni kukusanya tu mapato… Sheria zinaruhusu kuwa na mabadiliko ya kodi kama hayo, kwa hiyo sisi tunatekeleza maagizo tu ya Serikali, haturuhusiwi kutafsiri kwa njia yoyote,” alisema Kayombo.

Jana, benki za CRDB,NMB na Standard Chartered zilitoa maelekezo kwa wateja wake juu ya kuwapo kwa makato hayo zikisema kuwa kutakuwa na ongezeko la asilimia 18 litakalotozwa katika gharama za huduma za benki kunzia leo, zikiungana na NBC ambayo ilitangaza azma hiyo wiki iliyopita.

“Kufuatana na Sheria ya Fedha (Finance Act, 2016) ongezeko la asilimia 18 litatozwa katika gharama za huduma za benki kuanzia Julai 1, 2016. Ongezeko hili (VAT) litakatwa kutoka katika akaunti na kama muamala hautapia kwenye akaunti, mteja atalipa kwa fedha taslimu,” ilisema sehemu ya taarifa ya Benki ya CRDB.

Hata hivyo, kama zilivyo taarifa za benki nyingine, ilisema ongezeko hilo halitahusika katika riba kwenye mikopo. Benki ya NMB, ilisema katika taarifa yake kuwa ongezeko hilo litakuwa katika gharama zote za miamala ya kibenki kuanzia leo.

Hata hivyo, Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa NMB, Vicent Mnyanyika alipoulizwa kuhusu taarifa hiyo hasa kiasi ambacho wateja watakatwa alijibu kupitia ujumbe mfupi wa simu: “Sipo ofisini ila nahisi tangazo linajitosheleza.

Magazeti ya Leo ijumaa ya tarehe 01/07/2016
















Alhamisi, 30 Juni 2016

NEC yaanza mkakati wa kuhamia Dodoma



Imeandikwa na Sifa Lubasi, Dodoma


Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji mstaafu Damian Lubuva

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetekeleza kwa haraka agizo la Rais John Magufuli la kujenga Ofisi Kuu ya Tume baada ya jana kuoneshwa kiwanja katika eneo la Iyumbu katika Manispaa ya Dodoma.
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji mstaafu Damian Lubuva, amesema katika uchaguzi zijazo wataanza shughuli za usimamizi wakiwa Dodoma.
“Katika Uchaguzi Mkuu ujao, wapambe wa wagombea watakaa nje ya viwanja hivi wakiwasubiri watu wao wachukue fomu, huu ni mwanzo wa safari yetu ya kuhamia rasmi mjini Dodoma,” alisema Jaji Lubuva akionesha kiwanja hicho ambacho kimenunuliwa kutoka Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA).
Akizungumza baada ya kukagua eneo la ekari 10 litakalotumika kujenga ofisi hizo, Lubuva alisema huo ni mwanzo wa safari ya kuhamia Dodoma na katika chaguzi zinazokuja wataanzia shughuli za usimamizi wa uchaguzi hapo.
“Uchaguzi zijazo tutaanza shughuli za usimamizi wa uchaguzi kutoka Dodoma...Mimi na makamishna wa Tume tumefika hapa kukiona kiwanja ni kizuri tumekinunua kwa shilingi milioni 470 kwa upande wa tume tumeridhika,” alisema Lubuva.
Alisema lengo hilo lilikuwa la muda mrefu kuwa na jengo la kutosheleza mahitaji kwani sasa ofisi ya tume hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam ina ofisi tatu maeneo matatu tofauti lakini sasa wanatakiwa kufanya kazi eneo moja.
“Wale wa mwanzo kuhamia Dodoma tutakuwa ni sisi na huko mbele chaguzi zijazo tutakuwa katika majengo yetu,” aliongeza Mwenyekiti huyo wa NEC siku chache baada ya Rais Magufuli kuwataka kutafuta eneo la kujenga ofisi yao baada ya kuwapa Sh bilioni 12 ambazo ni bakaa la Uchaguzi Mkuu uliopita.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume hiyo, Kailima Ramadhani alisema katika Uchaguzi Mkuu uliopita walibakiza fedha kiasi cha Sh bilioni 12 ambazo walimrudishia Rais Magufuli kwa ajili ya matumizi mengine na rais aliwarudishia huku akiwataka wajenge jengo lao.
Kailima alisema eneo hilo lina miundombinu yote na wameanza mazungumzo la Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) ili ifikapo Oktoba ujenzi uanze na baada ya mwaka mmoja tume iwe na jengo lake.

UKAWA wamaliza bunge kwa upekee


 


 

Wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani leo asubuhi wameingia bungeni wakiwa wote wamevalia nguo nyeusi walipohudhuria kikao cha 54 cha Bunge la Bajeti mjini Dodoma.

Baada ya Naibu Spika Dk Tulia Ackson kuingia bungeni na kuongoza dua ya kuliombea Bunge, walianza kunyanyua mabango mbalimbali na kutoka nje.
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjL5W1Q8U2SzsCZDYkpJAUrA3W6owh1kPMghddzx2mFuQnz1PE7mX32sC8C_-WKTnd_ThxVo_w0CFipaYvSfiX0kKYymhlzRN0KhnkfPf7f8l5-5lve8f5XQiNnMV3rXJ6uz1wXsf55Z4c/s1600/4.jpeg