Jumamosi, 30 Julai 2016
Ijumaa, 29 Julai 2016
Lowassa Akoleza Moto CCM
Aliyekuwa
mgombea urais kwa tiketi ya Chadema na Ukawa, Edward Lowassa ana
uhakika kuwa bado kuna wanachama wanaomuunga mkono ndani ya CCM na sasa
anawataka waendelee kushikamana naye, kauli ambayo inaweza kuchochea
moto ndani ya CCM.
Katika
taarifa yake fupi kwa vyombo vya habari aliyoitoa jana, Lowassa
amewahakikishia wananchi kuwa kwa sasa ana “ari, nguvu na hamasa kuliko
wakati mwingine wowote”.
Lowassa,
ambaye alikuwa waziri mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne,
alijiondoa kwenye chama tawala Julai 28 mwaka jana baada ya jina lake
kuondolewa kwenye orodha ya wagombea urais kwa tiketi ya CCM.
Kuondoka
kwake kulisababisha mawaziri wa zamani, wabunge, wenyeviti wa mikoa,
madiwani na wanachama wengine wa CCM, wakiongozwa na waziri mwingine
mkuu wa zamani, Frederick Sumaye kukihama chama hicho, hali
iliyosababisha ushindani kuwa mkubwa kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita, huku
CCM ikilalamikia kusalitiwa.
Wakati
CCM ikifikiria hatua za kuchukua dhidi ya wasaliti wa chama
wanaotuhumiwa kuunga mkono harakati za upinzani wakati wa Uchaguzi Mkuu
uliopita, Lowassa ameongeza petroli kwenye moto ulioanza kuwaka.
“Kwa wale wenzangu waliobaki CCM na wanaoniunga mkono, tuendelee kushikamana na kunipatia taarifa kwa hatima ya nchi yetu,” amesema Lowassa ambaye kwa sasa ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema.
“Nawashukuru Watanzania kwa kuendelea kuniunga mkono mimi na wenzangu ndani Chadema.”
Kauli
hiyo kuwa kuna watu ndani ya CCM ambao wanampatia taarifa mbunge huyo
wa zamani wa Monduli na ombi lake la kutaka waendelee kumpa taarifa,
inaweza kusababisha hali ngumu zaidi kwa chama hicho, ambacho kinaamini
kuwa makada wake walikihujumu wakati wa uchaguzi kwa kumfanyia kampeni
kisiri.
Katika uchaguzi huo, Rais John Magufuli alishinda kwa kupata asilimia ndogo ya kura kulinganisha na watangulizi wake.
Ingawa
alipata kura milioni 8.8 na Lowassa kufuatia kwa kupata kura milioni
6.07, ushindi huo ni wa asilimia 58.46 dhidi ya asilimia 39.67
kulinganisha na ushindi wa asilimia 61.17 aliopata Kikwete mwaka 2010
dhidi ya asilimia 26.34 alizopata Dk Willibrod Slaa wa Chadema.
Tangu
Januari mwaka huu, CCM imekuwa ikijadili wasaliti hao katika ngazi ya
wilaya na taarifa za mapendekezo ya hatua dhidi yao kutumwa Halmashauri
Kuu kwa ajili ya uamuzi wa mwisho.
Katika
hotuba yake ya kuaga, Jakaya Kikwete alimkabidhi mwenyekiti mpya wa
CCM, Rais Magufuli ripoti ya hali ilivyokuwa kwenye uchaguzi, akisema
yeye ndiye atakayeamua adhabu dhidi ya wale wote walioonekana kufanya
makosa. CCM imeshasema kuwa wasaliti wote ni lazima washughulikiwe.
Katika taarifa yake ya jana, Lowassa ameeleza kuwa uamuzi alioufanya wa kuihama CCM na kujiunga na Chadema “haukuwa
rahisi, lakini kwa ushupavu, ujasiri na mwongozo wa Mungu nilifanya
hivyo” na kwamba huo ni “uamuzi wa kihistoria katika nchi yetu.
“Najivunia
kwa uamuzi ule, kwani umewafungua macho Watanzania wengi na kuimarisha
demokrasia. Nimeingia Chadema nimewakuta viongozi na wanachama walio na
moyo wa dhati wa kuliletea maendeleo Taifa lao kivitendo,” anasema Lowassa katika taarifa yake fupi.
“Watanzania
bado wanataka mabadiliko na imezidi kuthibitisha kuwa hawawezi kuyapata
ndani ya CCM. Watanzania wanataka sera na mtu mbadala wa kuongoza
mabadiliko hayo. Vyote hivyo watavipata ndani ya Chadema na Ukawa kwa
jumla.”
Alhamisi, 28 Julai 2016
Rais Magufuli kuhutubia mkutano wa hadhara Jumapili Wilayani Kahama
Rais John Magufuli anatarajia kufanya ziara wilayani Kahama mkoani Shinyanga ambako atafanya mkutano wa hadhara kuwashukuru wananchi kwa kumpigia kura nyingi katika Uchaguzi Mkuu uliopita.
Mkuu
wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulu alisema jana kwamba Rais Magufuli
atawasili hapa Jumamosi jioni kabla ya kufanya mkutano wa hadhara
Jumapili.
Nkulu
aliwataka wananchi wa Kahama na maeneo jirani kujitokeza kwa wingi
kumlaki kiongozi huyo katika ziara hiyo ambayo alisema: “Lengo lake ni kuwapongeza wananchi wa Kahama kwa kumpa kura nyingi katika Uchaguzi Mkuu uliomalizika mwaka jana.”
Alisema ziara hiyo ni muhimu kwa kuwa ni ya kwanza mkoani Shinyanga akianzia na Kahama.
“Tujipongeze wananchi kutokana na kupata bahati ya wilaya chache zilizotembelewa na kiongozi huyu, Kahama imekuwa mojawapo,” alisema Nkulu.
Alisema
kwa kuwa Jumamosi ni siku ya usafi kitaifa, kila mmoja wilayani humo
ahakikishe anaweka mazingira katika hali ya usafi na kuwaonya
wafanyabiashara kuwa atakayeshindwa kufanya hivyo hataruhusiwa kufungua
biashara.
“Nitafanya
ukaguzi Jumamosi kuhakikisha kila mtu anashiriki usafi. Hilo ni agizo
la kitaifa kwa sasa lazima kila mmoja awajibike, nimewaagiza watendaji
wote wa kata kusimamia hilo,” alisema Nkulu.
Picha ya Mtanzania anayeteswa na Mchina yampeleka Mwigulu Geita
Waziri
wa mambo ya ndani ya nchi, Mwigulu Nchemba amewasili mkoa wa Geita kwa
ziara ya kikazi, kubwa ikiwa ni kufuatia taarifa za mateso na mauaji
yaliyodaiwa kufanywa na raia wa China wanaomiliki sehemu ya mgodi wa
Nyamhuna uliopo Katoro, Geita dhidi ya wafanyakazi/vibarua ambao ni
Watanzania.
Takribani wiki moja sasa kumekuwa na hali ya sintofahamu dhidi ya picha zinazoenezwa mitandaoni na kwenye vyombo vya habari zikionesha raia wa Tanzania anayefanya kazi kwenye mgodi tajwa akiteswa na kufanyiwa vitendo ya kinyama na mwajili wake ambaye ni raia wa china.
Ilimlazimu
Waziri mwenye dhamana na usalama wa raia na mali zao kupitia Wizara ya
Mambo ya Ndani ya Nchi kufika eneo la mgodi kujiridhisha kwa taarifa
zilizotapakaa na kubeba simanzi kwa Watanzania.
Mwigulu
Nchemba amejiridhisha kuwa kulikuwepo na tukio hilo la Mtanzania
kuteswa na mwajiri wake, kipigo kilichosababisha kupoteza fahamu na siyo
kifo.
Hatua
za awali Waziri Nchemba alizozifanya ni kwenda gereza la Geita mjini
alikohifadhiwa kijana huyo kwa madai ya kushitakiwa na mwajiri wake kwa
kosa la wizi lililosababishwa apigwe.
Katika
mahojiano ya Waziri Mwigulu Nchemba na kijana huyo, Mwigulu alibaini
kuwa kijana huyo aliyepo gerezani ndiye mhusika hasa wa tukio lile kwa
uthibitisho wa makovu yaliyopo mwili mwake na mavazi aliyovalia wakati
anateswa na akiwapo gerezani.
Katika
hali hiyo, ilimlazimu, Mhe. Mwigulu kwenda mgodini akiwa ameambatana na
kijana huyo kwa ajili ya kutambua waliofanya vitendo hivyo vya
kinyama.
Katika
oparesheni hiyo, kijana aliyeteswa na kujeruhiwa aliwabaini Watanzania 5
ambao ni walinzi wa eneo hilo na Mchina mmoja walioshirikiana kumpiga,
kumtesa na kumjeruhi.
Kufuatia
utambuzi huo na maelezo ya wahusika, Nchemba akaagiza wahusika
wakamatwe mara moja na akaondoka nao kwa hatua zaidi za kisheria.
Katika
hali nyingine ya kusikitisha, Waziri Nchemba amebaini uwepo wa
wahamiaji haramu raia wa China katika mgodi huo ambapo nyaraka za
uhamiaji mkoa wa Geita zinaonesha raia 28 wenye vibali ndio waliruhusiwa
kukaa kwenye mgodi huo, lakini katika operasheni ya kushitukiza
aliyoifanya Mhe. Nchemba amebaini uwepo wa raia wa china zaidi ya 50
wanaoishi katika mgodi huo kinyume na sheria.
Hivyo
amemuagiza Mkuu wa Mkoa na timu yake ya uhamiaji kuhakikisha wote wasio
na vibali wanakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT) Chakanusha vyuo vyake kuzuiwa Kudahili
CHUO
Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT), kimetoa ufafanuzi wa taarifa
zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa vyuo vyake vishiriki
vimezuiwa na Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU) kufanya udahili wa
wanafunzi.
Taarifa
hizo zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zimedai kuwa vyuo
vishiriki vya SAUT ambavyo ni Stella Maris Mtwara University College
(STEMMUCO) na Archbishop James University College (AJUCO) vimefungiwa na
TCU kufanya udahili wa wanafunzi kwa mwaka wa masomo 2016/2017.
Kwa
mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Makamu Mkuu wa
Chuo cha SAUT, Dk Thadeus Mkamwa, taarifa hizo ni za upotoshaji na kuwa
hawajapokea taarifa kutoka TCU ikivizuia vyuo hivyo viwili kufanya
udahili.
Aidha,
Dk Mkamwa aliiomba jamii na wadau wa elimu kwa ujumla kupuuzia taarifa
hizo kwa kuwa zina uwezekano wa kuwa ni mbinu chafu zinazofanywa na
baadhi ya watu kuuhadaa umma hasa katika kipindi hiki ambacho ni muafaka
kwa waombaji kufanya maombi katika vyuo vikuu.
“Tunauomba
umma wa Watanzania kufahamu kuwa, Chuo Kikuu cha SAUT na vyuo vyake
vikuu vishiriki vilivyotajwa hapo juu vinaendelea na udahili wa
wanafunzi kwa mwaka wa masomo 2016/2017,” alisema Dk Mkamwa.
Alisema
SAUT ni Chuo Kikuu kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki Tanzania, na
kwamba kimepiga hatua kubwa katika kujiendeleza na kufanikiwa kuanzishwa
kwa vyuo vingine vikuu vishiriki vya SAUT ambavyo ni STEMMUCO kilichopo
Mtwara, AJUCO kilichopo Songea na Jordan University College (JUCO)
kilichopo Morogoro.
Vyuo
vingine ni St. Francis University College of Health and Allied Sciences
(SFUCHAS)- Morogoro, Archbishop Mihayo University College (AMUCTA)-
Tabora, na Cardinal Rugambwa Memorial University College (CARUMUCO)
kilichopo Bukoba, Marian University College (MARUCO) kilichopo Bagamoyo.
Dk Mkamwa aliongeza kuwa, chuo kimeweza kuanzisha vituo vingine vitatu vya SAUT vilivyoko Mbeya, Arusha na Dar es Salaam.
Jumatano, 27 Julai 2016
IRINGA: Mahakama Kuu imemhukumu kwenda jela miaka 15
#PUNDE. Habari za Punde, Koti Kuuu Kanda ya Iringa Imemuhukumu Kifungo cha Miaka 15 Askari wa Zamani wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia cha Mkoa Huo kwa Kosa la Mauaji ya Pasipo Kukusudia ya Mwandishi wa Habari wa Kituo cha Televisheni cha Mashariki mwa Nchi, Dar es Salaam, Chanel Ten Daudi Mwangosi
Jisajili kwenye:
Machapisho (Atom)