TAASISI
 ya Maridhiano inatarajia kuwasilisha ujumbe kwa Spika wa Bunge Job 
Ndugai kuomba kuyakutanisha makundi mawili yanayosigana bungeni ili 
kuleta muafaka wenye tija kwa taifa.
Mwenyekiti wa taasisi hiyo Sheikh
 Sadick Godigodi jana alisema kumeguka kwa Bunge kunakosababishwa na Kambi ya
 Upinzani kuona inaonewa na maamuzi ya Naibu Spika, Dk. Tulia Akson 
kunahitaji viongozi wa dini kuingilia kati na kupata suluhu.
"Tunatarajia
 katika Bunge lijalo litakaloanza Septemba kuwasilisha ujumbe kwa Spika 
ili tupewe nafasi ya kutatua mgogoro huu kwa maana wabunge wote 
wanatakiwa kuwepo bungeni kuwakilisha matatizo ya wananchi," alisema 
Sheikh Godigodi.
"Haiwezekani kundi moja likawa nje na jingine likaendelea, tunahitaji maridhiano ya pande zote mbili za muhimili huo.”
Kambi ya Upinzani Bungeni ilisusia vikao vya Bunge la Bajeti kwa zaidi ya siku 70 kupinga kile kilichoita kuburuzwa na
Naibu Spika katika uendeshaji wa chombo hicho cha kutunga sheria.
Kambi hiyo, ilianza kutoka nje Mei 30 baada ya Naibu Sika kukataa hoja ya Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua 
Nassari
 (Chadema), ya kutaka Bunge likatize shughuli zake na kujadili hoja ya 
kufukuzwa kwa wanafunzi zaidi ya 700 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom).
Ingawa
 kitendo hicho cha Naibu Spika kiliwaudhi wabunge wa chama tawala (CCM) 
na Upinzani, kambi hiyo haikurudi ndani mpaka Bunge lilipoahirishwa na 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa katikati ya wiki iliyopita.
Mshauri 
wa mambo ya kisheria na kidiplomasia wa taasisi hiyo ya Maridhiano, 
Agustino Matefu alisema mbali na kusuluhisha migogoro chochezi ya kidini
 kwa kutoa elimu sahihi kwa umma, pia wamejikita katika kusuluhisha 
migogoro sugu kati ya wakulima na wafugaji nchini.
“Tumetoa 
mchango mkubwa wa kuleta suluhu ya migogoro ya ardhi baina ya wafugaji 
na wakulima mkoani Morogoro katika wilaya za Mvomero, Kilombero na 
Kilosa (na) ndio maana watanzania wanaona hali ni kama sasa imekuwa 
shwari,” alisema Matefu.
Matefu alisema wamepata mualiko rasmi kwa
 uongozi wa Mkoa wa Iringa na wanatarajia kwenda huko baada ya uzinduzi 
rasmi wa taasisi hiyo utakaofanyika Julai 13 jijini Dar es Salaam.
Katibu
 wa taasisi hiyo, Mchungaji Oswald Mlay alisema kuwa uzinduzi na 
utambulisho wa taasisi hiyo utaendana na utoaji tuzo ya amani kwa 
viongozi na watu mbalimbali waliojitoa kuhamasisha udumishwaji wa amani 
nchini.
Wanaotarajiwa kupewa tuzo ni Mama Maria Nyerere kwa niaba 
ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere ambae atatunukiwa tuzo ya Amani
 uasisi wa amani ya taifa.













































