ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Alhamisi, 14 Julai 2016

Magazeti 473 Yafutiwa Usajili

  https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEg_krua7f-rgEnFiezLeJxR-HMBwTXaIEUmZUT-Ez8cJs77x-uqKEAJupQBDmXP_NnoaWTvujV-G8Az5Fz5uzbvIdlVQ4KL8gxxNZSwir6ngPOA2NHlD6UzXMUZDosZczE1I1WHlFJR5HA/s1600/1.jpg
SERIKALI imefuta usajili wa magazeti 473 kutokana na kutochapishwa kwa muda wa miaka mitatu mfululizo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye alisema magazeti hayo yamefutwa kupitia tangazo lake lililochapishwa katika Gazeti la Serikali lenye namba 195 la Juni 10, mwaka huu.

Aliyataja baadhi ya magazeti yaliyofutiwa ni Alasiri, Dar Leo, Femina Magazine, Sauti ya Wakulima (KCU 1990) Ltd, Utamu, Raha, Starehe, Muongozo, Motomoto, Daily Times, Financial Times, Sauti ya Siti, Wakati, Hali Halisi na Mkombozi. Pamoja na magazeti hayo, pia yapo magazeti yaliyokuwa yanatolewa katika mikoa maalumu kama vile Mbeya Leo, Kilimanjaro Leo, Arusha Leo, Kigoma Yetu, Karatu Yetu, Tanga Yetu, Sauti ya Jimbo Kuu Mwanza.

Waziri Nape alisema kutokana na kufutwa kwa viapo vya usajili wa magazeti hayo, mtu yeyote atakayechapisha au kusambaza magazeti hayo kwa njia ya nakala ngumu au kielektroniki atakuwa anakiuka sheria ya magazeti hivyo atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

“Iwapo kuna mmiliki wa gazeti ambaye angependa kuendelea na biashara hii baada ya kufungiwa, milango ipo wazi kwa ajili ya kuwasilisha maombi mapya ya usajili kwa kufuata taratibu zilizopo, ni imani yangu kuwa kwa wale wenye nia njema wameyaelewa maelezo haya,” alisema Nape.

Pia amewataka wamiliki wa magazeti hayo yaliyofutiwa viapo wahakikishe kwamba hawavunji sheria kwa kuanza biashara bila kufuata taratibu za usajili upya na endapo watakiuka maelezo hayo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Mbunge wa Afrika Mashari Auawa Kikatili Burundi

  https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjPTi0vvvcfQf36WCHX2g0AQu-NeoM-HeKj2aWeO_-Lx1-OkRaW1kpNzo3MCZ47B10oXCeVxQh1k68kOWO4MyOt6UbcpXfjiKHAiftHp6A1jXO1Y1b0SOKU4-2QEHprJtQsPAbyAsQvocM/s1600/1.jpg
MBUNGE wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kutoka nchini Burundi, Hafsa Mossi, ameuawa na watu wasiojulikana kwa kupigwa risasi katika mji mkuu wa Bujumbura.

Mossi aliyewahi kuwa Waziri wa Masuala ya Afrika Mashariki katika serikali ya nchi hiyo, aliuawa jana katika barabara ya Gihosha eneo la Nyankoni.

Taarifa zilizothibitishwa na Msemaji wa Polisi wa nchi hiyo, Pierre Nkurikiye zilisema kuwa mauaji hayo yalifanyika saa 4:00 asubuhi. Nkurikiye alisema mbunge huyo alipigwa risasi kifuani kwenye moyo na kukimbizwa katika Hospitali ya Jeshi ya Kamenge ambako baadaye alipoteza maisha.

EALA ni chombo cha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ambacho wanachama wake ni Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini, ukiwa ni umoja wa kikanda wenye ushirikiano wa kibiashara huku ukikusudia kuwa na sarafu moja na shirikisho moja la kisiasa.

Mkazi wa eneo alikouawa Mbunge huyo, Achel Majabuka alisema kuwa alisikia mlio wa risasi na baadaye kuona watu wawili wakiondoka katika gari baada ya kuwatishia kwa silaha wakazi wa eneo hilo.

Kwa upande wake, Bunge la Afrika Mashariki katika taarifa yake iliyotolewa Kampala nchini Uganda, ilisema kuwa Mossi ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Wabunge wa Burundi katika EALA, alipigwa risasi katika eneo la Mulanga Mashariki mwa Bujumbura.

Alimkariri msemaji huyo wa Polisi akieleza kuwa Mossi aliuawa karibu na nyumbani kwake, huku Mbunge mwingine wa Burundi katika EALA, Emerence Bucumi akithibitisha kifo hicho.

Spika wa Bunge la Afrika Mashariki, Daniel Kidega alilaani mauaji hayo na kumuelezea Mossi kuwa ni mchapakazi aliyekuwa amejikita kusimamia na kutetea utengamano wa ukanda huo.

Spika huyo ambaye yuko Uganda kwa ziara ya kikazi, ameishauri Serikali ya Burundi kuwatia nguvuni mara moja wauaji wa Mossi ambaye pia aliwahi kuwa Mtangazaji wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).

“Ninatoa salamu za rambirambi kwa serikali, familia, marafiki na wananchi wa Burundi. Ninawaomba wawe watulivu katika wakati huu mgumu na ninaamini mamlaka husika zitafanya kazi kwa haraka kuhakikisha waliohusika na tukio hilo la kinyama wanatiwa nguvuni mara moja,” alisema Spika Kidega.

Kwa upande wake, Rais wa Burundi, Pierre Nkurunziza alikielezea kifo cha mwanasiasa huyo kuwa ni cha kudharauliwa kwa serikali yake. Naye Katibu Mkuu wa EAC, Balozi Liberat Mfumukeko, alisema amesikitishwa na kifo hicho cha Mbunge huyo aliyeeleza alikuwa rafiki na dada na kuwa jumuiya imepoteza mwakilishi aliyekuwa akifanya kazi bila kuchoka.

Mwaka jana, Mossi alitembelea wakimbizi wa Burundi nchini Rwanda na kulia, ameuawa wakati mazungumzo kuhusu mgogoro wa Burundi yakiwa yanaendelea kufanyika jijini Arusha.

Alikuwa na Shahada ya Uandishi wa Habari na aliwahi kufanya kazi katika BBC na alikuwa Waziri wa Burundi wa Masuala ya Afrika Mashariki hadi Juni 2012 alipochaguliwa kuwa Mbunge wa EALA.

Pia, aliwahi Waziri wa Mawasiliano, Habari, Mahusiano na Bunge na Msemaji wa Serikali ya Burundi kuanzia mwaka 2005 hadi 2007.

Burundi, taifa katika Afrika Mashariki imekumbwa na ghasia na vifo kwa zaidi ya mwaka sasa.

Mgogoro huo wenye kuendana na umwagaji damu, umesababisha watu 1,500 kuuawa, huku ukiwahusisha wafuasi wa Rais Nkurunziza na wale wanaopinga ushindi wake wa uchaguzi wa Julai, 2015 kwa mara ya tatu, wakidai kuwa ulikiuka Katiba ya nchi hiyo.