ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumanne, 5 Aprili 2016

Magufuli afuta maadhimisho ya muungano aokoa bilion mbili

Rais Dkt John Magufuli
magufuli

RAIS John Magufuli ameahirisha shamrashamra za maadhimisho ya siku ya Muungano na hivyo kuwezesha kuokoa zaidi ya Sh bilioni mbili, alizoagiza zikaanzishe upanuzi wa barabara inayokwenda Uwanja wa Ndege wa Mwanza.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu kwa vyombo vya habari kutoka Chato mkoani Geita ambako Dk Magufuli yuko mapumzikoni nyumbani kwake, Rais ameelekeza siku hiyo itakuwa ya mapumziko kama kawaida, na Watanzania waiadhimishe wakiwa majumbani kwao ama katika shughuli zao binafsi.
Sherehe za Muungano huadhimishwa kila Aprili 26 kusherehekea kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ilianzishwa Aprili 26, 1964 baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
“Kufuatia kuahirishwa kwa shamrashamra hizo, Rais Magufuli ameelekeza kuwa fedha zilizopangwa kutumika kwa ajili ya kugharamia vinywaji, vyakula, gwaride, halaiki, burudani mbalimbali na hafla ya usiku ambazo ni zaidi ya shilingi bilioni mbili, zitumike kuanzisha upanuzi wa barabara ya “Mwanza - Airport” katika eneo linaloanzia Ghana Quaters hadi Uwanja wa Ndege wa Mwanza,” ilieleza taarifa ya Ikulu kutoka Chato.
“Barabara hiyo inafanyiwa upanuzi ili kukabiliana na kero ya msongamano mkubwa wa magari ambao unaathiri shughuli za kila siku za wananchi,” ilifafanua taarifa hiyo ya Ikulu.
Tangu aingie madarakani, Rais Magufuli alieleza azma ya Serikali yake ya Awamu ya Tano kubana matumizi na katika hatua alizochukua ni kufuta safari za nje ya nchi zisizo na tija, mikutano na makongamano, pamoja na kuahirisha sherehe mbalimbali na kuelekeza fedha zake katika masuala ya huduma za jamii.
Aliahirisha sherehe za Siku ya Uhuru, Desemba 9, mwaka jana na kutangaza siku hiyo kuwa ya kufanya usafi nchi nzima ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu katika dhana ile ya Uhuru ni Kazi.
Rais Magufuli aliagiza fedha zilizokuwa zitumike kwa sherehe hizo, Sh bilioni nne zikatumike kwa ajili ya upanuzi wa Barabara ya Bagamoyo kutoka Mwenge-Morocco, Dar es Salaam yenye urefu wa kilometa 4.3.
Aidha, Rais Magufuli alisitisha maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Kitaifa, ambayo yalikuwa yafanyike kitaifa mkoani Singida, Desemba mosi, mwaka jana.
Badala yake, aliagiza fedha zote ambazo zilitengwa na serikali pamoja na wahisani mbalimbali kwa ajili ya maadhimisho hayo, zielekezwe kununua vifaa tiba na vitendanishi. Serikali ilitenga kiasi cha Sh milioni 18 kwa ajili ya maadhimisho hayo huku kila mshiriki katika maonesho hayo akichangia kiasi cha Sh 500,000.
Awali Rais Magufuli aliagiza fedha zilizotengwa kwa ajili ya hafla ya uzinduzi wa Bunge zaidi ya Sh milioni 225, ziende kununulia vitanda kwa ajili ya wagonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu mstaafu wa Kenya, Raila Odinga amerejea nchini Kenya baada ya kumaliza mapumziko yake ya siku tatu Lubambangwe katika Kijiji cha Mlimani, Wilaya ya Chato mkoani Geita alikomtembelea Rais Magufuli aliyepo mapumzikoni.
Akizungumza kwenye Uwanja wa Michezo wa Shule ya Sekondari ya Chato kabla ya kuruka kwa helikopta, Raila alimshukuru rafiki yake Rais Magufuli kwa kumpokea na pia aliwashukuru wananchi wa Chato kwa ukarimu wao kwa wageni.
Pia alisema ana imani kuwa Rais Magufuli ataisaidia Tanzania kukabiliana na changamoto mbalimbali, ikiwemo umasikini unaowakabili wananchi wake. “Lakini mimi najua yeye mwenyewe ana maono, anaona mbele na anajua yale ambayo yanatakiwa yafanyike ili Tanzania iinuke, itoke katika hali ya ufukara na kuwa katika hali ya maendeleo zaidi,” alisema Raila.
Raila na mkewe, Mama Ida Odinga waliwasili Chato, Jumamosi iliyopita kwa mapumziko na kuisalimia familia ya Rais Magufuli ambayo ni familia rafiki.
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli ameahidi kutoa madawati na vitabu kwa wanafunzi wa shule tatu za msingi zilizopo Chato, ambao walijitokeza Uwanja wa Sekondari wa Chato wakati Rais Magufuli akimuaga mgeni wake Waziri Mkuu mstaafu wa Kenya, Raila Odinga.

Jumamosi, 2 Aprili 2016

MAKALA YA LEO: JE MISAADA INAYOTOLEWA NA CAMFED INA TIJA?


kuna mashirika mbalimbali ambayo yameamua kwa namna moja kusaidia jitihada za elimu hasa kwa wafunzi wa kike katika shule za misingi lakini leo tunajiuliza je misaada inayotolewa ina tija kwa wanafunzi wenyewe?
au ndo inasaidia kuwafaidisha baadhi ya wadau waliopo katika mashirika hayo kama wakurugenzi wa mashirika, walimu na viongozi mbalimbali wa shule?
Kupitia maswali haya ndipo tulipoamua kutuma watafiti wetu katika shule mbalimbali hasa katika shule za sekondary za wilaya ya kilolo na kubaini uwepo wa madudu makubwa hasa kwa walimu wanaohusika na utoaji wa pesa mbalimbali kwa wanafunzi waliofadhiliwa na mradi huu wa CAMFED;
- Pesa nyingi zinazotolewa na wafadhili zimebainika kuishia kwa walimu walezi na kile kidogo kinachobaki ndicho wanafunzi hudanganywa kwa kununuliwa daftali au kupewa vifaa vya kujifunzia wafadhiliwa katika mradi huu kutoka shule fulani walisema" ni kwel CAMFED ina tufadhili kwa kutulipia ada na mahitaji mbalimbali ila hapa shuleni kwenu anaefaidi sana ni mwalimu wetu maana mara nyingine huwa wanatulazimisha tusaini hela elfu 80,000/= afu si tunapewa elfu thelathini (30,000/=) tukiuliza wanasema wanakata hela kwaajili ya matumizi ya shule".
mwandishi wetu hakuishia hapo alijaribu kuwadodosa baadhi ya walimu wanaohusika na mradi huo ambao walishindwa kabisa kujieleza na kutoa ushirikiano kwa kudai hayo ni mambo ya kitaasisi" haya ni mambo ya kitasisi sisi kama shule tuna utaratibu wetu wa kutoa pesa ambao humwekea akiba mwanafunzi" alisema mwalimu.

vile vile CAMFED hutoa misaada mbalimbali ya vitabu vya kujifunzia kwa wanafunzi ambavyo mara nyingi hufanya wakuu wa shule watumie vitabu hivyo kana kwamba wametumia bajeti ya shule

JE MISAADA HII INAMANUFAA KWA JAMII HUSIKA TUPE MAONI YAKO HAPO CHINI :misaelkikoti.blogspot.com

Hiyo ni baadhi ya vitabu vilivotolewa na CAMFED kwa shule mbalimbali wilaya ya kilolo
 

 Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi akizungumza na baadhi ya wakuu wa shule za sekondari zilizoko katika wilaya ya kilolo baada ya kukabidhi vitabu katika shule hizo. Kushoto kwake Mwalimu mkuu wa shule ya Sekondari Ilula
Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi akionyesha moja ya vitabu ambavyo amekibadhi kwa shule 22 za wilaya ya Kilolo halfa zilizofanyika katika ukumbi wa shule ya sekondari Ilula.  Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi akimkabidhi Mwenyekiti Huduma za Jamii wa Halmashauri ya wilaya Kilolo, Anna Kulanga moja ya mfano wa vitabu walivyokabidhi katika shule za sekondari wilaya ya Njombe.  Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Ilula.
Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi mwenye nguo ya njano akiwa na walimu wa shule za sekondari zilizopatiwa msaada wa vitabu kutoka shirika la CAMFED.(Picha zote na Denis Mlowe)
 Baadhi ya Maboksi ya Vitabu yaliyokabidhiwa kwa shule 22 zilizoko wilaya ya kilolo.

Na Denis Mlowe,Ilula
Katika kuhakikisha kiwango cha elimu nchini kinakua,shirika lisilo la Kiserikali la Campaign for Female Education (CAMFED)  chini  ya mpango wake kuwasomesha watoto wa kike kilitoa misaada ya vitabu 54,935 kwa shule 22 za sekondari zilizoko katika wilaya ya Kilolo mkoani Iringa vyenye thamani ya shilingi milioni 55.
Alipoongea  wakati wa halfa ya kukabidhi vitabu iliyofanyika katika Shule ya Sekondari Ilula mwishoni mwa mwaka juzi mgeni rasmi Mwenyekiti Huduma za Jamii wa Halmashauri ya wilaya Kilolo, Anna Kulanga alilishukuru shirika hilo kwa msaada huo kwa kuweza kuwafikia wanafunzi wa shule za Iringa vijijini.
 “Tumefurahi sana kupata vitabu mbalimbali kwani shule ya sekondari za hapa zina  changamoto ya upungufu wa vitabu hasa vya sayansi na kulifanya somo hilo kuwa na wanafunzi wa chache, lakini hivi sasa kutokana na msaada wa vitabu vilivyo tolewa vitaongeza ufaulu kwa wanafunzi wetu kutokana na uwingi wa vitabu wenyewe kwa shule zilizofaidika na msaada huo” alisema Kulanga
Aliwataka walimu na wanafunzi  wavitumie vitabu hivi vizuri kwa kuvitunza kwa lengo la kutumika kwa muda mrefu wakati wa masomo yao na kuamini kwamba vitabu vivyo vitaleta ufanisi  katika kukuza uelewa wa mwanafunzi katika matumizi sahihi ya lugha ya kiingereza.
Aidha alisema vitabu hivyo vitumike kwa wanafunzi wote kwa wa shule husika na kuwaasa wanafunzi wa shule zilizofaidika na msaada huo kuacha tabia mbaya ya kuuza vitabu na kuwataka walimu wa shule hizo kufatilia kwa makini wanafunzi wote watakaopatiwa vitabu hivyo.
Naye Mwalimu mkuu aliekuwa  wa sekondari ya Irole Laurence Maluka alipongea kwa niaba ya wakuu wa sekondari 22 zilizofaidika na msaada huo wa vitabu alisema msaada huo wa vitabu utaweza kuwa saidia wanafunzi kuwa na uweza wa kujisomea zaidi na kuwawezesha kufaulu hadi kwenda chuo kikuu,kwani hapo awali kulikuwa na changamoto kubwa katika shule zetu ambapo uwiano ulikuwa kitabu kimoja wanafunzi  5 lakini kwa sasa ni vitabu 5 kwa mwanafunzi mmoja.
“Ni jambo la kulishukuru sana shirika la CAMFED kwa msaada huu utapunguza zaidi, kwa kweli huu ni msaada mkubwa katika kuboresha taaluma na kuinua ufaulu hivyo tunaomba program hii ya shule zetu iendelee ili kuwafikiwa wanafunzi wengi zaidi katika wilaya ya Kilolo” alisema Maluka
Kwa upande wake Afisa Miradi wa CAMFED Tanzania, Christina Kyaruzi amewataka wanafunzi wa sekondari zote wilaya ya Kilolo mkoani Iringa kuongeza uwezo wa kujisomea ufaulu wa wanafunzi unaongezeka kupitia msaada unatolewa na shirika hilo.
Alisema  vitabu hivi vitunzwe ili viweze kuwafaidisha wanafunzi wengi kwa kuwa  vitaleta faida kwa wanafunzi wengi zaidi katika kujisomea na kuwataka walimu wakuu wawapatie wanafunzi kila mmoja vitabu vitano na kwenda navyo nyumbani hadi amalizapo elimu ya sekodari na kuweza kuvirudisha. Alizitaja shule zilizofaidika na msaada huo ni shule ya sekondari Ilula, Nyalumbu, Mazombe, Irole,Lundamatwe, Selebu, Ngangwe, Uhambingeto, Lukosi, Mlafi Na Ndekwa.
Shule nyingine ni shule za za sekondari za Mtitu, Kilolo, Lulanzi,Ukwega, Udzungwa, Dabaga, Kitowo, Mawambala, Masisiwe, Madege na Makwema.

Mkwasa kuongeza nguvu yanga

KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Charles Mkwasa ameitwa kuongeza nguvu katika benchi la ufundi la Yanga kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri wiki ijayo.
Habari zilizopatikana jana kutoka Yanga, zilieleza kuwa tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeshatoa ruhusa ili aweze kuisaidia Yanga kipindi hiki cha kuelekea mchezo huo. “Ni kweli Mkwasa ameitwa kuongeza nguvu, unajua Kocha wa Yanga (Hans Pluijm), anamkubali sana Mkwasa, hivyo wameona aje asaidie wakati huu ambapo hana majukumu Taifa Stars,” kilisema chanzo chetu na kusisitiza kwamba Mkwasa haina maana amejiondoa Taifa Stars.
Mkwasa hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo, wala Ofisa Habari wa Yanga, Jerry Muro na hata Ofisa Habari wa TFF, Baraka Kizuguto. Hata hivyo, TFF iliwahi kutoa taarifa kwamba timu za Yanga na Azam zipo huru kuwatumia makocha wa Taifa Stars, Mkwasa na Hemed Morocco katika maandalizi yao kwa ajili ya michezo ya kimataifa inayowakabili.
Mkwassa alikuwa Kocha Msaidizi wa Yanga kabla ya kuteuliwa kuwa kocha muda wa Taifa Stars katikati ya mwaka uliopita akirithi mikoba ya Mholanzi Mart Nooij aliyetimuliwa baada ya matokeo mabaya ya Stars.
TFF ilisaini naye mkataba wa miezi 18 Oktoba mwaka jana baada ya kuridhishwa na kazi yake, ambapo mkataba huo utamalizika Machi 31 mwakani. Wakati huohuo, Mohammed Akida anaripoti kuwa Pluijm amesema ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ndanda FC juzi utachangia kukiimarisha kikosi chake kwa mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly mwishoni mwa wiki ijayo.
Yanga juzi ilishinda mabao 2-1 katika mchezo wa robo fainali Kombe la Shirikisho, lakini haikuonesha kiwango cha kuvutia kiasi cha mashabiki kuingiwa na hofu kuhusu mchezo wao na Ahly.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Pluijm alikiri timu yake kucheza vibaya, lakini alisema hiyo ni moja ya mikakati yao kuhakikisha wanatunza nguvu za kucheza mechi zingine tatu zinazowakabili ikiwemo ya Al Ahly.
Pluijm alisema huo ni ushindi mkubwa kwao na sasa wanajipanga kushinda michezo miwili ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar na Mtibwa Sugar kabla ya kuikabili Al Ahly Jumamosi ijayo.
Kwa upande wake kocha wa Ndanda FC, Abdul Mingange, alisema kilichosababisha timu yake kupoteza mchezo huo ni kukosa uzoefu kwa wachezaji wake, ambao walitengeneza nafasi nyingi lakini walishindwa kuzitumia. Mingange alisema timu yake ilicheza vizuri na kuutawala mchezo, lakini tatizo kubwa ilikuwa ni umaliziaji ambao ulikuwa kikwazo.
Bingwa wa michuano hiyo inayojulikana pia kama Kombe la FA, atawakilisha nchi katika mashindano ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika (CAF CC) mwaka 2017. Kutokana na ushindi huo, Yanga na Azam sasa zinaungana na Mwadui ya Shinyanga, ambayo Jumamosi iliifunga Geita Gold Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza mabao 3-0 na kufuzu nusu fainali.

KATILYA NA WENZAKE WAWILI WAKUTANA KIZIMBANI

Kitilya, wenzake wawili kortini

SAKATA la rushwa ya Dola za Marekani milioni 600, linalohusisha Benki ya Standard ya London Uingereza, jana lilichukua sura mpya baada ya kufikishwa mahakamani kwa aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya, akikabiliwa na mashitaka mbalimbali, ikiwemo utakatishaji wa fedha.
Washitakiwa wengine waliounganishwa katika kesi hiyo ni pamoja na mrembo wa zamani wa Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Uwekezaji wa Benki ya Stanbic, Shose Sinare na aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Sheria wa benki hiyo, Sioi Graham Solomon. Mashitaka mengine yanayowakabili katika kesi hiyo mbali na kutakatisha fedha, ni pamoja kutumia nyaraka za kughushi na za uongo kujipatia isivyo halali Dola za Marekani milioni 6, sawa na Sh bilioni 12 za Tanzania.
Mbele ya Hakimu Mwandamizi, Emilius Mchauru washitakiwa hao walikana mashitaka hayo na kurudishwa rumande mpaka Aprili 8 mwaka huu, wakati mahakama itakapokutana kusikiliza shauri kuhusu dhamana yao. Upande wa utetezi, ukiwakilishwa na mawakili Dk Ringo Tenga na Semu Anney, waliomba mahakama itoe dhamana kwa wateja wao.
Hata hivyo, upande wa Mashitaka ukiwakilishwa na wanasheria waandamizi wa Serikali; Oswald Tibabyekomya na Christopher Msigwa pamoja na Mwanasheria wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru), Stanley Luwoga walipinga dhamana hiyo kwa madai kuwa kesi za utakatishaji fedha hazina dhamana.
Awali upande wa mashitaka uliieleza mahakama kwamba, katika tarehe tofauti kati ya Agosti 2012 na Machi 2013, katika Jiji la Dar es Salaam, washitakiwa hao watatu walipanga pamoja kwa kushirikiana na watu wengine ambao hawakufikishwa mahakamani hapo, kutenda kosa la kujipatia fedha kwa udanganyifu kutoka serikalini.
Ilidaiwa kuwa kati ya Agosti 2, 2012 katika Makao Makuu ya Benki ya Stanbic Tanzania Limited yaliyopo wilayani Kinondoni, mshitakiwa Sinare akiwa na nia ovu, alighushi taarifa ya maombi ya fedha ya Benki ya Standard ikiwa na tarehe ya Agosti 2, 2012.
Kwa mujibu wa madai hayo, Sinare alieleza katika maombi hayo kuwa Benki ya Standard ya London kwa kushirikiana na Benki ya Stanbic ya Tanzania, watatoa mkopo unaofikia Dola za Marekani milioni 550 kwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa gharama ya asilimia 2.4 ya mkopo huo, wakati akijua kuwa gharama hiyo si kweli.
Mahakama ilielezwa kuwa Agosti 13, 2012, mrembo huyo wa zamani wa Tanzania, aliwasilisha taarifa hiyo ya kughushi katika Wizara ya Fedha iliyopo Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam. Imedai kuwa Septemba 20, 2012 katika Benki ya Stanbic, Sinare alitengeneza barua ya uongo ya kuelezea mkopo huo wa Dola za Marekani milioni 550, ikieleza kuwa Benki ya Standard PLC kwa kushirikiana na Benki ya Stanbic, zitatoa mkopo huo kwa Serikali kama wakikubaliwa.
Upande huo wa mashitaka uliendelea kudai kuwa, Sinare aliwasilisha barua hiyo ya uongo katika Wizara ya Fedha kwa lengo hilo hilo. Kwa mujibu wa madai hayo, Novemba 5, 2012 katika Benki ya Stanbic jijini Dar es Salaam, washitakiwa wote watatu, wakiwa na nia ovu, walitengeneza makubaliano ya uongo kwa lengo la kuonesha kuwa benki imeipa kampuni ya Enterprise Growth Market Advisors (EGMA) Limited, kazi ya kushughulikia mkopo huo.
Lengo la washitakiwa hao kwa mujibu wa madai hayo, lilikuwa kufanikisha mkopo huo wa Dola za Marekani milioni 550 kwa Serikali ya Tanzania, ambapo EGMA alitarajiwa kuonekana kuwa muongozaji wa mazungumzo ya kupata mkopo huo. Upande huo wa mashitaka ulidai kuwa Machi 2013 jijini Dar es Salaam, Kitilya, Sinare na Sioi, wakiwa na lengo ovu walifanikiwa kupata Dola za Marekani milioni 6, sawa na Sh bilioni 12, wakidai kuwa fedha hizo ni malipo ya kazi iliyofanywa na EGMA Limited.
Utakatishaji fedha Watatu hao pia wameshitakiwa kwa utakatishaji fedha unaodaiwa kufanyika kati ya Machi 13 na Septemba mwaka jana. Wanadaiwa kushiriki kutakatisha Dola za Marekani milioni sita kwa kuzihamisha kwenda katika akaunti tofauti, kuzitoa katika akauti hizo na kuziweka katika akauti zingine tofauti zinazomilikiwa na EGMA Limited katika Benki ya Stanbic Tanzania Limited na Benki ya KCB Limited.
Mahakama imeelezwa kuwa hivi karibuni Benki ya Standard imelipa Dola za Marekani milioni 33 baada ya kukiri kushindwa kuzuia rushwa katika suala hilo. Mbunge kortini Katika hatua nyingine, Takukuru jana ilimfikisha Mahakamani Mbunge wa Sumwe, Richard Ndassa (pichani), ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Mtaji na Uwekezaji kwa kosa la kushawishi na kuomba rushwa ya Sh milioni 30, kinyume na Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya mwaka 2007 kifungu cha 15 (i)(a) na (2).
Taarifa ya Takukuru kwa vyombo vya habari, imedai kuwa Mbunge huyo akiwa mjumbe wa Kamati hiyo, alimwomba rushwa hiyo Mtendaji Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Felchesmi Mramba ili amsaidie kuwashawishi wajumbe wengine wa Kamati Mtaji na Uwekezaji kupitisha bila kipingamizi taarifa ya Tanesco kwa mwaka 2015/16.
Mbunge huyo amefunguliwa kesi namba 118/2016 na alisomewa mashitaka hayo na Wakili wa Takukuru, Dennis Lekayo akishirikiana na Emmanuel Jacob katika Mahakama ya Kisutu mbele ya. Hakimu Emirius Mchauro.
Mshitakiwa yupo nje kwa dhamana baada ya kupata mdhamini mmoja na kulipa Sh milioni 10 na uchunguzi wa shauri hilo bado unaendelea huku kesi ikitarajiwa kutajwa tena Aprili 18, 2016.

BEI YA UMEME YAWA NAFUU

MAMLAKA ya Udhibiti ya Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imepunguza bei ya umeme baada ya kupokea ombi la Shirika la Umeme (Tanesco). Katika maombi yake, Tanesco waliomba kupunguza umeme kwa asilimia 1.1 lakini baada ya Ewura kupitia maombi hayo imepunguza kwa asilimia 1.5 hadi 2.4 kutoka bei ya sasa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi alisema bei hiyo mpya ya umeme, imeanza kutumika jana. Kwa mujibu wa Ngamlagosi, Ewura walifikia hatua hiyo ya kupunguza zaidi ya maombi ya Tanesco, baada ya kukaa na wadau.
Mbali na kushusha bei ya umeme, Ngamlagosi alisema pia baadhi ya gharama ambazo ni tozo ya kuwasilisha maombi ya kuunganishiwa umeme ambayo ilikuwa Sh 5,000 na tozo ya huduma ya mwezi (service charge) iliyokuwa Sh 5,520 kwa wateja wa majumbani ambao wapo katika kundi la T1, pia vimefutwa Ngamlagosi alisema hata marekebisho ya bei za umeme kwa mwaka 2017, yameahirisha mpaka Tanesco itakapowasilisha upya maombi hayo kabla ya Agosti 31, mwaka huu.
“Kutokana na kifungu cha Sheria ya Umeme ya mwaka 2008, kifungu cha 23 (2) na 23 (3), yatakuwepo marekebisho ya bei za umeme kutokana na mabadiliko ya bei za mafuta, thamani ya fedha na mfumuko wa bei. Marekebisho hayo yatafanyika kwa mujibu wa kanuni ya 7 ya urekebishaji wa bei za umeme ya mwaka 2016,” alisema.
Aliongeza kuwa kundi la wateja wadogo wa nyumbani wale wa kipato kidogo ambao wanatumia uniti moja hadi 75, wanatakiwa kwa mwezi kulipa Sh 350 kwa kila uniti inayozidi.
Pia, kwa watu wa majumbani wenye matumizi makubwa wana punguzo la Sh 6 kutoka Sh 298 kwa uniti hadi 292. Kundi jingine lililonufaika na punguzo hilo, limetajwa kuwa ni wafanyabiashara wa kati ambao ni wenye mitambo, hoteli na migahawa ambao wana punguzo la Sh 5 kutoka Sh 200 hadi 195.
Ngamlagosi alifafanua kuwa wateja wa viwandani wamepunguziwa Sh 2 kwa uniti toka Sh 159 hadi 157 na wateja wanaotumia msongo mkubwa wa umeme wana punguzo la Sh 4 kutoka Sh 156 hadi 152 kwa uniti.
Alisema pia Tanesco ilipeleka ombi la punguzo la umeme la mwaka 2017 ambalo walipendekeza bei ya umeme ipungue kwa asilimia 7.9, lakini pendekezo hilo limeahirishwa mpaka hapo watakapowasilisha upya maombi kabla ya Agosti 31, mwaka huu.
Alitaja masharti waliyopewa Tanesco ili watekeleze kuwa ni pamoja na kuwasilisha taarifa kila mwezi Ewura ili kujua hali halisi ya uzalishaji. Tanesco pia imetakiwa ifikapo Juni 30, iwasilishe Mpango wa Uwekezaji (CIP), unaoendana na kiasi cha Sh bilioni 351.4, kilichoruhusiwa kulingana na mapato ya uchakavu wa miundombinu na mapato yatokanayo na faida ya uwekezaji.
Ngamlagosi alisema katika kipindi cha miezi sita, Tanesco imetakiwa iwasilishe mpango wa utekelezaji wa kuimarisha mfumo wa mita katika mtandao kwa usambazaji umeme kwa lengo la kupima kwa usahihi nishati ya umeme na kukokotoa kiwango cha upotevu wa umeme kwa ufasaha.
Katika kipindi hicho, alisema Tanesco imetakiwa ibuni mikakati ya kupambana na uunganishaji wa umeme usio halali na ucheleweshaji usiokuwa wa lazima, kama ulivyoainishwa katika mkataba wa huduma kwa wateja.
Kwa mujibu wa Ngamlagosi, shirika hilo limetakiwa lihakikishe linawasilisha ripoti ya ukusanyaji madeni kutoka kwa wateja wanaodaiwa na malipo yaliyofanyika kwa watoa huduma wanayoidai Tanesco kila baada ya robo mwaka.
Pia limetakiwa litoe taarifa ya fedha za ruzuku au msaada zilizopokelewa kutoka serikalini au kwa wadau wa maendeleo kwa ajili ya marekebisho stahiki ya umeme.

Jumatano, 30 Machi 2016

Breaking news: Ajira za walimu kutolewa baada ya bajeti kupitishwa

 

Waziri wa TAMISEMI amesema ajira mpya za walimu mwaka huu zitatoka pale bajeti hiyo itakapopitishwa ili kuepuka usumbufu ameyasema hayo alipokuwa katika mahojiano na clouds tv leo tar 30/03/2016

Jumamosi, 26 Machi 2016

Kificho ang’oka uspika

ALIYEKUWA Spika wa Baraza la Wawakilishi kwa zaidi ya miaka 20 sasa, Pandu Ameir Kificho, ameng’olewa katika nafasi hiyo baada ya kushindwa katika kura za kuwania awamu nyingine ya uongozi wa baraza hilo.
Badala yake wajumbe wateule wa Baraza la Wawakilishi, wamemchagua Zubeir Ali Maulid, kuwa Spika mteule wa baraza hilo, baada ya kupata kura 55 na kumuacha kwa mbali Kificho aliyeambulia kura 11 katika uchaguzi uliofanyika jana katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui, Zanzibar.
Aidha katika uchaguzi huo ambao wawakilishi 72 walipiga kura, Janeth Nora Sekihola ambaye ni hakimu mstaafu akipata kura 4 wakati kura mbili ziliharibika.
Hata hivyo, akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuangushwa katika uchaguzi huo, Kificho alisema amekubali kushindwa na yupo tayari kutoa ushirikiano akitakiwa kufanya hivyo.
“Hiyo ndiyo demokrasia, nimekubali kushindwa na nipo tayari kutoa ushirikiano mkubwa nikitakiwa kufanya hivyo kwa sababu ni ukweli kwamba ninao uzoefu mkubwa katika nafasi hiyo kwa zaidi ya miaka 20,” alisema.
Naye Spika mteule wa baraza hilo, Maulid alisema anakabiliwa na changamoto kubwa ya kuleta maendeleo na mabadiliko makubwa katika chombo hicho ambacho ni moja ya mihimili ya dola katika utekelezaji wa majukumu yake.
Amesema atatumia uzoefu alioupata kufanya kazi katika taasisi za kutunga sheria, kwa ajili ya kuleta mabadiliko hayo kwa kuhakikisha kwamba Baraza la Wawakilishi linafanya kazi inayotakiwa ya kuisimamia Serikali kwa mujibu wa Katiba.
“Nimekuwa Mwakilishi Shauri Moyo na Waziri mwaka 2000, pia nimekuwa Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa miaka miwili na nusu kwa hivyo uwezo wa kufanya kazi katika mabunge ya Jumuiya ya Madola ninao mkubwa,” alisema.
Aliwaomba wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wateule kumpa kila aina ya ushirikiano utakaomwezesha kutekeleza na kutimiza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba, kwani chombo hicho ni moja ya mihimili ya dola.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliozungumza na gazeti hili, wamesema kwamba mabadiliko hayo ni ishara na ujumbe tosha kwa Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kwamba wawakilishi wanataka mabadiliko makubwa kwa Serikali kwa ajili ya kuwatumikia wananchi.
“Mabadiliko makubwa tuliyoyafanya sisi wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa kumchagua Zubeir Ali Maulidi kuwa Spika mteule mpya, ni dalili tosha kwamba sasa tunataka mabadiliko makubwa ndani ya Serikali kwa kuwa na viongozi watakaowatumikia wananchi moja kwa moja,” alisema Rashid Ali Juma mwakilishi mteule wa jimbo la Amani.
Kificho ameweka historia kuwa Spika wa Kwanza katika Baraza la Wawakilishi la mfumo wa vyama vingi kuanzia mwaka 1995, ambapo kabla ya kuchaguliwa kushika wadhifa huo, alikuwa mwakilishi wa Jimbo la Makunduchi kuanzia 1988.
Zubeir Ali Maulid mwaka 2000 alichaguliwa kuwa Mwakilishi wa Shauri Moyo kwa tiketi ya CCM na kuteuliwa kuwa Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi, chini ya Serikali ya Rais mstaafu Amani Abeid Karume, ambapo alidumu katika wadhifa huo kwa miaka mitatu.
Mwaka 2005, Zubeir alichaguliwa kuwa Mbunge wa Kwamtipura kwa tiketi ya CCM ambapo akiwa bungeni katika kipindi cha miaka miwili na nusu, alikuwa Mwenyekiti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na kuongoza vikao mbali mbali kwa kusaidiana na spika na naibu spika.
Katika hatua nyingine, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein, amemteua Said Hassan Said, kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ). Uteuzi huo ndio wa kwanza kufanyika, tangu Rais Shein alipokula kiapo cha kuongoza Zanzibar kwa miaka mitano ijayo Alhamisi ya wiki hii.