RAIS John Magufuli ameungana na mamia ya waombolezaji kuaga mwili wa
Mbunge mstaafu wa Mkoa wa Singida, Marehemu Christina Lissu Mughwai
katika ukumbi wa Karimjee, Jijini Dar es Salaam.
Mughwai aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida katika
kipindi cha kuanzia mwaka 2010 hadi 2015, aliagwa jana kabla ya
kusafirishwa kwenda kijiji cha Mahambe mkoani Singida kwa maziko.
Pamoja na Rais Magufuli na mkewe Mama Janeth, viongozi wengine
waliohudhuria shughuli ya kuaga ni Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Akson
na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bunge, Freeman Mbowe.
Akitoa salamu kwa niaba ya Rais Magufuli, Waziri wa Nchi Ofisi ya
Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George
Simbachawene aliwapa pole familia ya marehemu. Alisema katika kipindi
chake cha ubunge, Mughwai alitoa mchango mkubwa kama mbunge na kama
mtaalamu wa Uchumi.
KUTENGULIWA kwa uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anne Kilango
Malecela kumeendelea kuwa gumzo huku viongozi wengine wakiambiwa wawe
macho kwa kuchukulia uamuzi huo wa Rais Magufuli, kama funzo la kutambua
aina ya uongozi anaoutaka katika Serikali yake ya Awamu ya Tano.
Wakati viongozi hususani wa kuteuliwa wakitakiwa kuzingatia ukweli
kwamba serikali ya awamu hii haihitaji wanaoficha mabaya wakitaka mazuri
ndiyo yaonekane, baadhi wameshauri mfumo uliopo, hususani wa kupeana
taarifa uangaliwe kwa kuwa una tatizo linalohitaji kufanyiwa kazi.
Miongoni mwa watu ambao gazeti hili lilizungumza nao jana kuhusu
hatua hiyo ya Rais kutengua uteuzi wa Kilango, ni mwanasiasa mkongwe
nchini, Paul Kimiti aliyetaka viongozi wengine kutambua kwamba, Magufuli
ni kiongozi asiyependa unafiki.
“Uongozi wake tangu mwanzo umejidhihirisha wazi kuwa ni kiongozi
anayependa uwazi na ukweli hataki short cut (njia za mkato),” alisema
Kimiti. Kimiti aliyewahi kushika uwaziri katika Serikali zilizopita,
alisema hatua hiyo ya Rais ni ishara na funzo kwa viongozi wengine hasa
wale walio madarakani kuhakikisha kuwa wanawajibika ipasavyo kwa kufuata
misingi ya uwazi na kutokimbilia njia za mkato.
Alisema kwa hali ilivyo, ni vyema viongozi waliopo wakaanza kufuata
heshima na taratibu za kiongozi aliyewaweka madarakani, hali ambayo
itawasaidia kutowajibishwa.
Mwanasiasa huyo ambaye alionesha kuguswa kwa mtazamo chanya na hatua
anazochukua Rais, alisema kumekuwa na utaratibu wa watendaji kutoa
taarifa zisizo sahihi na zisizo kamili kwa wakuu wao wa kazi kwa lengo
la kuonesha kuwa mambo ni mazuri.
Alisema jambo hilo ni tatizo kubwa linalopaswa kukemewa. Utendaji wa
kujikomba “Hii ni kero kubwa, watendaji wengi wanaficha taarifa za
ukweli kwa wakuu wao ili kuonesha mambo ni mazuri, hili ni jambo baya
kabisa kwani matokeo yake ndiyo haya; anakuja kuwajibishwa mtu mwingine
ambaye huenda hakuhusika na taarifa hizo,” alisisitiza.
Alisema utendaji wa aina hiyo ni sawa na utendaji wa kujikomba ambao
hauna tija, kwani pamoja na kuficha ukweli na uhalisia wa mambo, mwisho
wake siku wananchi ndio waathirika na baadaye ukweli hufichuka.
Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Haji
Semboja alisema kilichotokea ni funzo kubwa kwa viongozi wengine
kuhakikisha kuwa kila taarifa wanayopatiwa lazima wanaifanyia kazi na
kujiridhisha kabla ya kuitoa kwa umma.
“Mama Kilango kwa vyovyote vile bado ndio alikuwa anaanza kazi ya
ukuu wa mkoa, hivyo lazima atakuwa amepatiwa taarifa aliyoitoa kwa umma
na watendaji wake. Hii ilikuwa ni kawaida, viongozi wengi huuamini mfumo
unaowapatia taarifa,” alisema Semboja.
Hata hivyo, alisema kiongozi huyo alipaswa baada ya kupatiwa taarifa
ya awali, angewasiliana na vyanzo mbalimbali kupata uhakika kwa kutumia
madaraka aliyonayo wakiwemo waajiri na wanaofanya malipo kujiridhisha.
Alisema anaamini hatua aliyoichukua Dk Magufuli ni ishara na njia
yake ya kutambulisha kwa umma mtindo wa uongozi unaozingatia uwazi na
uwajibikaji. “Hiki kwetu ni kitu kipya hatujakizoea, lakini sasa ni
vyema kila kiongozi awe makini na kutambua kuwa akikosea lazima
awajibike,” alisisitiza.
Mfumo uangaliwe
Pamoja na hayo, alimuomba Rais Magufuli awe mvumilivu na atambue kuwa
huenda tatizo kubwa bado lipo kwenye mfumo uliopo wa kupeana taarifa
ambao utahitaji kuangaliwa kwa umakini na kuchukuliwa hatua stahiki.
Alisema Dk Magufuli ni kiongozi anayefuata mfumo wa kisheria na
kwamba hatua zote alizochukua zinatokana na nia njema aliyonayo kwa
watanzania. “Huyu ni mtakatifu baada ya Mungu, ana moyo mzuri na nia
njema kwa watanzania,” alisema Profesa Semboja.
Akizungumzia watumishi hewa, Profesa Semboja alishauri baada ya
operesheni ya kuwatafuta upande wa rasilimali watu ndani ya utumishi wa
umma lazima utoe taarifa nzima na kufafanua kilichotokea.
Kwa upande wa Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson
Bana, alisema hatua aliyoichukua Dk Magufuli ya kumvua uongozi Kilango
ni ishara kuwa anatoa kipaumbele katika suala zima la uwajibikaji lakini
pia hapendi viongozi wasiojishughulisha.
“Inaonesha dhahiri Dk Magufuli katika masuala nyeti yanayogusa taifa
hapendi majibu mepesi wala njia za mkato. Hii inamaanisha kuwa viongozi
hawana budi kuzifanyia kazi taarifa wanazopewa na kujiridhisha kwanza,”
alisema Dk Bana.
Awali gazeti hili lilizungumza na Kilango kwa njia ya simu ili kuweza
kupata upande wake kuhusu nini kilitokea na kusababisha kutoa taarifa
hiyo isiyo sahihi kuhusu watumishi hewa mkoani Shinyanga, ambapo mara
baada ya salamu, mwandishi alipojitambulisha alikata simu.
Juzi Rais Magufuli alitengua uteuzi wa mkuu huyo wa mkoa baada kutoa
taarifa za uongo kwenye vyombo vya habari kuwa mkoani kwake hakuna
watumishi hewa. Alisema baada ya taarifa hiyo, aliunda timu maalumu kwa
ajili ya uhakiki wa watumishi hewa mkoani humo na ndani ya siku moja,
walibaini kuwepo kwa watumishi hewa 45 waliokuwa tayari wamelipwa
mishahara yenye gharama ya Sh milioni 339.9.
BUNGE limetoa siku tatu kwa Jeshi la Polisi kuwasilisha kwenye Kamati
ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) mkataba wa Kampuni Lugumi
Enterprises wenye thamani ya Sh bilioni 37.
Hatua hii inakuja siku mbili baada ya jeshi hilo kudaiwa kukaidi
agizo la kamati hiyo, iliyotaka likabidhi nyaraka za utekelezaji wa
mkataba ufanyiwe tathmini kutokana na malalamiko yaliyotolewa na
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali(CAG) katika hesabu za mwaka
2013/2014.
Akizungumza jana na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya PAC,
Aeshi Hilaly alisema agizo la kamati la kutaka mkataba huo, lilitolewa
wiki iliyopita kuwezesha wabunge kuangalia utekelezaji wake.
“Jana (juzi) ilikuwa siku ya mwisho kwa jeshi kuwasilisha mkataba huo
ofisi za Bunge, lakini mpaka leo (jana) muda huu ninapozungumza nanyi
(saa 7:30 mchana) walikuwa hawajawasilisha. “
Siku zote tumekuwa tukitoa maagizo kwa mdomo na taasisi nyingi
zimekuwa zikitekeleza, lakini hili la mkataba wa Lugumi naona kwa
wenzetu limekuwa gumu, hivyo tumeamua kuwakumbusha kwa maandishi,”
alisema.
Alisema kamati hiyo imetoa siku tatu tangu barua itakapopelekwa na
ofisi za Bunge, kuhakikisha wanatekeleza agizo hilo ili kamati hiyo
iweze kupitia utekelezaji wa mkataba huo na baadaye kupeleka mapendekezo
kwenye Bunge.
“ Katika suala hili, Kamati haitarudi nyuma, hivyo tunawaomba wenzetu
wa Jeshi la Polisi kutupa ushirikiano, si jambo la peke yangu kuamua,
ni la Bunge, baada ya kupitia tunapeleka mapendekezo bungeni ambalo
ndilo litakaloamua nini kifanyike,” alisisitiza.
Hata hivyo, habari zilizofikia HabariLeo jana zinasema jeshi hilo
lilipeleka mkataba huo katika Kamati ya Mambo ya Nje na Usalama na juzi
badala ya Kamati ya PAC iliyoagiza. “Kuna taarifa kuwa mkataba huo
umepelekwa kwenye kamati ya Mambo ya Nje inayoongozwa na Mbunge wa
Muheza, Balozi Adadi Rajabu,” kilisema chanzo chetu.
Hata hivyo, Adadi aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI)
alikanusha madai hayo kwa kujibu kifupi kwa ujumbe wa simu kuwa, “suala
hilo limepelekwa PAC.” Kamati ya PAC ilipokuwa ikipitia hesabu za Jeshi
la Polisi, ilibaini kuwapo mkataba tata wa Kampuni ya Lugumi Enterprises
.
Kupitia mkataba huo wa mwaka 2011, Kampuni ya Lugumi Enterprises
ilipewa zabuni ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika
vituo vya polisi 108 nchini kwa gharama ya Sh bilioni 37.
Inasadikiwa kampuni hiyo imekwishalipwa Sh bilioni 34 kati ya Sh
bilioni 37 ikiwa ni sawa na asilimia 99 ya fedha zote, huku ikiwa
imefunga mashine katika vituo 14 pekee katika jiji la Dar es Salaam,
ambavyo pia inadaiwa havijulikani maeneo vilipo.
Headline za magazeti ya Leo zinaletwa kwenu Kwa hisani ya New Mwalimu education centre inayopatikana eneo la ilula madizini _iringa Tanzania majengo ya kanisa catholic kigango cha madizini madizini
Head line news za magazeti ya Leo zinaletwa kwenu Kwa hisani ya new Mwalimu tuition centre Inayopatikana ilula madizini kanisa la Romani catholic wanafundisha masomo ya ziada Kwa kidato cha kwanza mpaka cha sita na Kwa wanaotaka kurudia mitihani yao nyote mnakaribishwa Kwa mawasiliano zaidi piga