Imeandikwa na
Mwandishi Wetu
KWA mara ya kwanza Bajeti ya Serikali ya Rais John Magufuli
inatarajiwa kuwasilishwa Juni 9, mwaka huu, kwenye Mkutano wa Tatu wa
Bunge la 11, unaoanza mjini Dodoma kesho.
Bajeti hiyo itawasilishwa rasmi na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk
Phillip Mpango saa 10 kamili jioni siku ya Alhamisi baada ya
kuwasilishwa kwa taarifa ya Hali ya Uchumi wa Nchi asubuhi siku hiyo.
Taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano cha Bunge jana,
ilieleza kuwa baada ya kuwasilishwa kwa bajeti hiyo, ambayo mapendekezo
yake ya awali kwa wabunge yalibainisha kuwa itakuwa ni ya Sh trilioni
29, wabunge wataijadili kwa muda wa siku tisa kuanzia Juni 13 hadi Juni
21, mwaka huu.
Pamoja na bajeti hiyo, pia Dk Mpango atawasilisha Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa miaka mitano 2015/16 hadi 2020/21.
“Baada ya kuwasilishwa kwa mpango huo, Bunge pia litapokea na
kujadili utekelezaji wa bajeti kwa wizara zote kwa mwaka wa fedha
2015/16 na makadirio ya matumizi ya Serikali 2016/17, kazi
itakayofanyika kuanzia Aprili 22 hadi Juni 2, mwaka huu,” ilieleza
taarifa ya Bunge.
Hivi karibuni, Dk Mpango aliwasilisha mapendekezo ya ukomo wa bajeti
hiyo ya mwaka 2016/17 mbele ya wabunge jijini Dar es Salaam, na
kubainisha kuwa inatarajiwa kuwa ya Sh trilioni 29.539 sawa na ongezeko
la asilimia 31.32 ya bajeti iliyopita ya mwaka 2015/2016.
Kwa mujibu wa mapendekezo ya bajeti hiyo, Serikali inalenga kutumia
Sh trilioni 15.105 sawa na asilimia 82 ya mapato ya ndani, mapato ya
kodi na yasiyo na kodi na mapato kutoka halmashauri Sh trilioni 2.693 na
Sh bilioni 665.4 na washirika wa maendeleo wanatarajiwa kuchangia Sh
trilioni 3.600 ambayo ni sawa na asilimia 12 ya bajeti yote.
Akichanganua mapendekezo hayo, alisema kwa upande wa matumizi katika
mwaka ujao wa fedha, Serikali inapanga kutumia Sh trilioni 17.719 kwa
matumizi ya kawaida na Sh trilioni 11.820 kwa matumizi ya maendeleo sawa
na asilimia 40 ya bajeti yote.
Aidha, alitaja vipaumbele vingine kuwa ni viwanda vya kukuza uchumi
na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda, kufungamanisha maendeleo ya
uchumi na rasilimali watu na mazingira wezeshi kwa uendeshaji biashara.
Pamoja na kuwasilishwa kwa bajeti hiyo, pia katika Mkutano huo Tatu
wa Bunge unaoanza kesho, pamoja na kuwasilishwa hati za mezani, Bunge
pia litapokea Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali
(CAG) ya mwaka 2014/15 ambayo hivi karibuni ilikabidhiwa kwa Rais
Magufuli.
“Pia Bunge litapokea majibu ya Serikali kuhusu hoja zilizotolewa na
CAG kwa hesabu za mwaka wa fedha 2014/15,” ilisema taarifa hiyo ya
Kitengo cha Mawasiliano cha Bunge.
Taarifa hiyo ilisema pia katika mkutano huo, Bunge litajadili na
kupitisha miswada miwili ambayo ni Muswada wa Sheria ya Matumizi wa
Mwaka 2016 na Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2016.
“Vilevile inategemea kuwa Serikali itawasilisha bungeni miswada ya
Sheria kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa bungeni mara baada ya
shughuli ya kupitisha bajeti kukamilika,” ilisema taarifa hiyo.
Aidha, katika mkutano huo kutakuwa na shughuli ya uchaguzi wa
Mwenyekiti wa Bunge kwa ajili ya kuziba nafasi iliyoachwa wazi baada ya
Spika wa Bunge, Job Ndugai, kufanya mabadiliko ya baadhi ya wajumbe wa
Kamati za Kudumu za Bunge. Nafasi hiyo imeachwa wazi na Mbunge wa Viti
Maalumu, Dk Mary Mwanjelwa.
Aidha, wabunge wapya wanne ambao ni Shamsi Vuai Nahodha wa Jimbo la
Kijitoupele, Ritha Kabati na Oliver Semguruka wote Viti Maalumu CCM na
Lucy Owenya wa Viti Maalumu Chadema, wanatarajiwa kuapishwa rasmi.