ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumatatu, 18 Aprili 2016

Bajeti ya Magufuli kusomwa Juni 9

Imeandikwa na Mwandishi Wetu KWA mara ya kwanza Bajeti ya Serikali ya Rais John Magufuli inatarajiwa kuwasilishwa Juni 9, mwaka huu, kwenye Mkutano wa Tatu wa Bunge la 11, unaoanza mjini Dodoma kesho.
Bajeti hiyo itawasilishwa rasmi na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Phillip Mpango saa 10 kamili jioni siku ya Alhamisi baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya Hali ya Uchumi wa Nchi asubuhi siku hiyo.
Taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Mawasiliano cha Bunge jana, ilieleza kuwa baada ya kuwasilishwa kwa bajeti hiyo, ambayo mapendekezo yake ya awali kwa wabunge yalibainisha kuwa itakuwa ni ya Sh trilioni 29, wabunge wataijadili kwa muda wa siku tisa kuanzia Juni 13 hadi Juni 21, mwaka huu.
Pamoja na bajeti hiyo, pia Dk Mpango atawasilisha Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa miaka mitano 2015/16 hadi 2020/21.
“Baada ya kuwasilishwa kwa mpango huo, Bunge pia litapokea na kujadili utekelezaji wa bajeti kwa wizara zote kwa mwaka wa fedha 2015/16 na makadirio ya matumizi ya Serikali 2016/17, kazi itakayofanyika kuanzia Aprili 22 hadi Juni 2, mwaka huu,” ilieleza taarifa ya Bunge.
Hivi karibuni, Dk Mpango aliwasilisha mapendekezo ya ukomo wa bajeti hiyo ya mwaka 2016/17 mbele ya wabunge jijini Dar es Salaam, na kubainisha kuwa inatarajiwa kuwa ya Sh trilioni 29.539 sawa na ongezeko la asilimia 31.32 ya bajeti iliyopita ya mwaka 2015/2016.
Kwa mujibu wa mapendekezo ya bajeti hiyo, Serikali inalenga kutumia Sh trilioni 15.105 sawa na asilimia 82 ya mapato ya ndani, mapato ya kodi na yasiyo na kodi na mapato kutoka halmashauri Sh trilioni 2.693 na Sh bilioni 665.4 na washirika wa maendeleo wanatarajiwa kuchangia Sh trilioni 3.600 ambayo ni sawa na asilimia 12 ya bajeti yote.
Akichanganua mapendekezo hayo, alisema kwa upande wa matumizi katika mwaka ujao wa fedha, Serikali inapanga kutumia Sh trilioni 17.719 kwa matumizi ya kawaida na Sh trilioni 11.820 kwa matumizi ya maendeleo sawa na asilimia 40 ya bajeti yote.
Aidha, alitaja vipaumbele vingine kuwa ni viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda, kufungamanisha maendeleo ya uchumi na rasilimali watu na mazingira wezeshi kwa uendeshaji biashara.
Pamoja na kuwasilishwa kwa bajeti hiyo, pia katika Mkutano huo Tatu wa Bunge unaoanza kesho, pamoja na kuwasilishwa hati za mezani, Bunge pia litapokea Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2014/15 ambayo hivi karibuni ilikabidhiwa kwa Rais Magufuli.
“Pia Bunge litapokea majibu ya Serikali kuhusu hoja zilizotolewa na CAG kwa hesabu za mwaka wa fedha 2014/15,” ilisema taarifa hiyo ya Kitengo cha Mawasiliano cha Bunge.
Taarifa hiyo ilisema pia katika mkutano huo, Bunge litajadili na kupitisha miswada miwili ambayo ni Muswada wa Sheria ya Matumizi wa Mwaka 2016 na Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2016.
“Vilevile inategemea kuwa Serikali itawasilisha bungeni miswada ya Sheria kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa bungeni mara baada ya shughuli ya kupitisha bajeti kukamilika,” ilisema taarifa hiyo.
Aidha, katika mkutano huo kutakuwa na shughuli ya uchaguzi wa Mwenyekiti wa Bunge kwa ajili ya kuziba nafasi iliyoachwa wazi baada ya Spika wa Bunge, Job Ndugai, kufanya mabadiliko ya baadhi ya wajumbe wa Kamati za Kudumu za Bunge. Nafasi hiyo imeachwa wazi na Mbunge wa Viti Maalumu, Dk Mary Mwanjelwa.
Aidha, wabunge wapya wanne ambao ni Shamsi Vuai Nahodha wa Jimbo la Kijitoupele, Ritha Kabati na Oliver Semguruka wote Viti Maalumu CCM na Lucy Owenya wa Viti Maalumu Chadema, wanatarajiwa kuapishwa rasmi.

Hakuna maoni: