ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Alhamisi, 22 Septemba 2016

Basi laua watu 13 Mwanza


MAISHA ya Watanzania yameendelea kupotea katika ajali za barabarani baada ya ajali nyingine, iliyohusisha basi la abiria la kampuni ya Super Shem kugongana na daladala (Hiace) na kusababisha watu 13 kufa na wengine zaidi ya 10 kujeruhiwa.
Ajali hiyo ilitokea jana saa 12 asubuhi katika kijiji cha Mwamaya, kwenye makutano ya barabara kuu ya Mwanza na ya kutoka Misasi, katika eneo la Hungumalwa.
Basi hilo lililokuwa linatoka Mbeya kwenda Mwanza, liligongana hiace na kuharibika vibaya. Rais John Magufuli amemtumia salamu za rambirambi kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella kufuatia vifo vya watu hao 13 na majeruhi wa ajali hiyo.
Mapema wiki hii, basi lingine la New Force linalofanya safari kati ya Dar es Salaam na Songea mkoani Ruvuma, liliacha njia na kupinduka katika kijiji cha Lilombwi Kata ya Kifanya wilayani Njombe, mkoani Njombe na kuua watu 12 huku wengine 30 wakijeruhiwa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema imesababishwa na mwendo kasi usio na tahadhari.
Alisema mbali na vifo hivyo 13, watu watatu kati ya majeruhi 10, wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando na hali zao ni mbaya. Msangi akiwa eneo la tukio pamoja na Mongela ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati za Ulinzi na Usalama ya Mkoa, alisema ajali hiyo ni ya saa 12:15 asubuhi na dereva wa hiace akiwa katika mwendo kasi, alishindwa kumudu gari.
Msangi aliyataja magari yaliyohusika katika ajali hiyo kuwa ni la kampuni ya Supa Shem lenye namba za usajili T 874 CWE, lililokuwa linaendeshwa na Anthony Shirima na hiace namba T368 CWQ iliyokuwa ikiendeshwa na dereva ambaye jina lake halijafahamika na hali yake ni mbaya.
Alisema miili ya marehemu tisa, imekwishatambuliwa na ndugu zao, ambapo miili mitatu ya mama na mtoto, haijatambuliwa na imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba; na mwili mmoja umehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Misungwi.
Aliwataja waliokufa katika ajali hiyo, waliotambuliwa na ndugu zao na makazi yao katika mabano kuwa ni Monica Shiji, Christian Emanuel, Thereza Majengwa (Gulumwa), Lwinzi Kope (Chasalawe) na Mabula Magi (Rukwa).
Wengine ni Isaya Deogratias (Mande), Moses Kamel mkazi wa Dodoma-Kwimba na mama na mtoto ambao kwa sasa bado hawajatambuliwa. Kamanda Msangi alisema ajali hiyo imetokea wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Usalama Barabarani, hivyo watatumia fursa hiyo kutoa elimu kwa madereva kujua na kuzingatia sheria za usalama barabarani.
Aliwataja majeruhi watatu, kati ya kumi, waliotambulika kuwa ni Faustine Emmanuel ambaye ni konda wa Hiace, Shija Roketi na mtoto mdogo aliyejulikana kwa jina moja la Martin.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mongela ambaye aliongozana na kamati za ulinzi na usalama za wilaya na mkoa, alimuagiza Msangi kukamata madereva wazembe ambao hawaheshimu sheria za usalama barabarani.
Salamu za Rais Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Dar es Salaam jana, ilieleza kuwa Rais John Magufuli amepokea taarifa ya ajali hiyo ya Mwanza kwa mshituko, kwa kuwa ni siku moja imepita tangu Watanzania wengine 12 kufa katika ajali ya basi la New Force iliyotokea Njombe.
"Nimesikitishwa sana na vifo vingine vya Watanzania wenzetu, waliopoteza maisha katika ajali huko Mwanza, nakuomba Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella unifikishie salamu za pole kwa familia zote zilizopoteza ndugu, jamaa na marafiki katika ajali hii.
Nawaombea wote waliotangulia mbele za haki wapumzishwe mahali pema na pia wote walioguswa na msiba wawe na moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu katika kipindi kigumu cha majonzi ya kuondokewa na jamaa zao," alisema Magufuli.
Rais Magufuli pia aliwaombea majeruhi wote wa ajali hiyo, wapone haraka ili waungane na familia zao na kuendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa.

Hakuna maoni: