ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Alhamisi, 10 Machi 2016

Simba leo tena

TIMU ya soka ya Simba na Mbeya City leo zinashuka dimbani kwenye viwanja viwili tofauti kusaka pointi tatu muhimu katika mfululizo wa mechi za Ligi Kuu bara. Simba itakuwa mwenyeji wa Ndanda FC kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam wakati Mbeya City itakuwa mwenyeji wa Stand United kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya.
Wekundu hao wa Msimbazi huenda wakapanda kileleni tena iwapo watafanikiwa kuwafunga Ndanda Fc katika mchezo huo kwa kuwa watafikisha pointi 51 na kuishusha Yanga yenye pointi 50.
Mwishoni mwa wiki iliyopita Simba ilikaa kileleni kwa siku mbili kabla ya Yanga juzi kupanda na kumpiku kufuatia ushindi wake wa mabao 5-0 dhidi ya African Sports ya Tanga. Simba, Yanga na Azam FC zinatofautiana kwa pointi chache kiasi kwamba mmoja akishinda, mwingine anashuka.
Simba ina uwezekano wa kushinda mchezo wa Ndanda, kwani katika mchezo wake wa raundi ya kwanza ilishinda bao 1-0 ugenini mjini Mtwara. Hali itakuwa mbaya kwa Ndanda kama itakubali kichapo kwa mara nyingine kwani licha ya kuwa katika nafasi ya nane, ina pointi 24 ambazo hazitoshi kuihakikishia kubaki salama kwenye msimamo wa ligi kwa kuwa timu zilizoko chini yake zinaweza kupanda kutokana na kutofautiana pointi chache.
Kwa upande wa Mbeya City, huenda ikafanya vizuri leo baada ya kuonesha kiwango bora chenye mabadiliko katika mchezo dhidi ya Simba wiki iliyopita. Licha ya kufungwa mchezo huo, walicheza vizuri isipokuwa inayumbushwa na ubutu wa safu yake ya ushambuliaji.
Pengine kwa vile inacheza kwenye uwanja wake wa nyumbani wanaweza kutumia faida hiyo katika kufanya vizuri na kufuta machungu ya kufungwa na timu hiyo ya Shinyanga bao 1-0 katika mchezo wa raundi ya kwanza.

APR, Yanga watambiana

HOMA ya pambano la raundi ya kwanza la Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na APR ya Rwanda, imezidi kupanda, kiasi cha kila moja kutamba kumshikisha adabu mpinzani wake.
Tayari makocha wa klabu hizo, Hans van der Pluijm wa Yanga na Nizar Khanfir wa APR aliyeweka rekodi ya kuwa mwarabu wa kwanza kufundisha soka Rwanda baada ya kuanza kazi rasmi jana, ameelezea utayari wake kushinda mechi ya Jumamosi wiki hii huko Kigali, Rwanda.
Khanfir amekaririwa jana kuwa, ameshawaona Yanga kupitia video mbalimbali na kwamba anataka kuwafunga Jumamosi. “Lengo letu ni kushinda huo mchezo,”amesema na kuongeza; “Nimeona baadhi ya video zao na tutaendelea kuwachambua katika siku chache zijazo kuelekea kwenye mechi”.
Kwa ujumla, Khanfir amesema malengo yake makuu katika miezi sita ya mwanzo ni kuiwezesha timu kutetea ubingwa wa Rwanda na pia kuifikisha mbali katika Ligi ya Mabingwa Afrika. Mtaalamu huyo wa Tunisia aliongoza mazoezi yake ya kwanza APR jana Uwanja wa Kicukiro akisaidiwa na kocha aliyemkuta kazini, Emmanuel Rubona.
“APR ni timu kubwa Rwanda na ina heshima kubwa Afrika na pia ina wachezaji wengi katika timu ya taifa, ambacho ndicho kilichonivutia mimi kukubali kazi hii,” amesema Khanfir. “Wachezaji ni vijana wadogo na timu ina uwiano mzuri ambao unafaa vizuri katika falsafa yangu. Tunaitaka kuipeleka timu katika kiwango kingine.
Ni wajuzi na tunataka kuongeza ufundi zaidi, lakini zaidi ya hapo nimevutiwa na timu kwa ujumla,” amesema. Wakati Khanfir akisema hayo, Pluijm kwa upande wake amesema anatambua wanakwenda Kigali kwenye mchezo mgumu wa ugenini dhidi ya APR, lakini watapambana wasipoteze.
“APR ni timu nzuri na watakuwa wamejiandaa vizuri, lakini sisi tuko vizuri, tutakwenda kupambana tusipoteze mchezo, ili tumalizie vizuri mchezo wa nyumbani,”amesema. Yanga SC inatarajiwa kuondoka leo nchini kwenda Kigali kwa ajili ya mchezo huo, unaotarajiwa kuwa mkali na wa kusisimua.
Mechi hiyo inatarajiwa kuchezeshwa na marefa wa Malawi Jumamosi Uwanja wa Amahoro, Kigali Rwanda. Duncan Lengani anatarajiwa kupuliza filimbi, wakati washika vibendera watakuwa Clemence Kanduku na Jonizio Luwizi.
Mchezo wa marudiano wiki moja baadaye Dar es Salaam, utachezeshwa na marefa wa Shelisheli; katikati Bernard Camille na pemebeni watakuwapo Eldrick Adelaide na Gerard Pool.
Mchezo wa kwanza utafanyika mjini Kigali, Rwanda Machi 12 kabla ya timu hizo kurudiana Dar es Salaam Machi 19 na mshindi wa jumla atakutana na mshindi wa mchezo mwingine wa raundi ya kwanza, kati ya Al Ahly ya Misri na Recreativo de Libolo ya Angola mwezi ujao.

St Joseph watakiwa kurudi darasani

WAZIRI wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako ameingilia kati mgogoro wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha St. Joseph Dar es Salaam, waliogomea kufanya mitihani na kuwataka warejee madarasani wakati matatizo yao yakishughulikiwa.
Wanafunzi hao walikuwa katika siku ya tatu ya mgomo wao jana ambapo pamoja na mambo mengine walikuwa wakilalamikia mapungufu yaliyopo chuoni hapo, ikiwa ni pamoja na maabara za kufanyia mafunzo kwa vitendo, matatizo ya kiutawala, mitaala ya kufundishia pamoja na ada.
Profesa Ndalichako aliwasili chuoni hapo jana asubuhi na kukagua mazingira ya kufundishia ya chuo hicho kwa kutembelea maabara zote chuoni hapo na kisha kwenda kuzungumza na utawala, Serikali ya wanafunzi na mwisho alihutubia wanafunzi wote.
Ndalichako baada ya kuzungumza na pande zote mbili aliagiza wanafunzi hao warejee madarasani kuendelea na mitihani yao na kuutaka uongozi wa chuo uyafanyie marekebisho mapungufu ya kiutawala yaliyojitokeza.
Aidha ameiagiza Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), chini ya Katibu Mtendaji wake, Profesa Yunus Mgaya kufuatilia na kuchunguza kwa makini madai ya wanafunzi hao juu ya kuwepo kwa wahadhiri wasio na sifa zinazotakiwa.

Magufuli aitamani Vietnam

RAIS John Magufuli amesema anatamani mafanikio ya nchi ya Vietnam kiuchumi na kubainisha kuwa ziara ya Rais wa nchi hiyo, Truong Tang Sang nchini, ni fursa na changamoto kwa watanzania kujifunza mambo mengi, yatakayosaidia kukuza pia uchumi wa Tanzania.
Aidha amehamasisha Watanzania kuchangamkia fursa na rasilimali zilizopo nchini katika kujiinua na kuimarisha nchi yao kiuchumi. Alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi tajiri kwa rasilimali na fursa nyingi, ingawa bado iko nyuma kimaendeleo. Kwa upande wake, Rais Sang amesema nchi yake na Tanzania zimekubaliana kushirikiana katika maeneo ya biashara, kilimo, viwanda na uvuvi lengo likiwa ni kuhakikisha nchi zote zinanufaika kwenye ushirikiano huo.
Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari na marais hao Ikulu Dar es Salaam jana, Dk John Magufuli alisema ni wakati sasa wa Tanzania kujifunza kutoka kwa nchi hiyo ya Vietnam ambayo pamoja na kukabiliwa na vita ya muda mrefu, imefanikiwa kuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi wa kati. “Ukweli ni kwamba ziara ya Rais Sang nchini kwetu ni muhimu sana na imekuja kwa wakati muafaka.
Mwaka 1976 Rais wa Vietnam alikuja nchini na alichukua mbegu ya korosho na kuipeleka nchini kwake, na leo hii Vietnam ni moja ya nchi zinazoongoza kwa kuzalisha korosho duniani,” alisema. Alitaja mafanikio mengine ya nchi hiyo ni pamoja na kuwa na uchumi wa kati, licha ya kukabiliwa na mapigano ya muda mrefu. Ilipata uhuru wake mwaka 1945 na ilidumu kwenye mapigano hadi Julai 2, mwaka 1976.
Alisema mwaka 1977 mapato ya kila raia wake yalikuwa ni dola 100, lakini sasa imefanikiwa kupandisha mapato hayo na sasa kila raia wa nchi hiyo mapato yake ni dola 2000 kwa mwaka na imepunguza kiwango cha umasikini kwa asilimia 50. “Sisi tangu mwaka 1960 bado tuko kwenye nchi masikini, kwa hiyo hii ni changamoto kwa nchi yetu. Tunatakiwa kujifunza kuondokana na hali hii.
Wao uzalishaji kwa mchele wanalima mara tatu kwa mwaka, sisi tunalima mara moja tu na inawezekana uzalishaji wetu ni mdogo sana,” alisema. Alisema nchi hiyo pamoja na kuchukua mbegu ya korosho nchini, ndio nchi inayoongoza kwa kuzalisha korosho duniani, wakati Tanzania ndio iliyotoa mbegu hiyo, zao hilo badala ya kuzalishwa kwa wingi ndio uzalishaji wake unafifia.
“Samaki sina uhakika kama walichukua huku, lakini leo hii Vietnam ni wazalishaji wa samaki wakubwa sana. Lakini kwa nchi yetu ambayo ina maziwa 21 na mito kila mahali na bahari lakini uzalishaji wa samaki uko chini…” “Tuna ng’ombe zaidi ya bilioni 22 hadi bilioni 23 nafikiri tunaweza kuwa wa pili barani Afrika baada ya Ethiopia, lakini ngozi zetu za viatu hapa tunaagiza nje.
Kwa hiyo kwa hili watanzania tunatakiwa tusiogope kujifunza kwa wale waliotutangulia ili na sisi nchi yetu iweze kufika mahali pazuri,” alisisitiza Dk Magufuli. Alisema ujio wa Rais Sang pamoja na ujumbe wake wa zaidi ya mawaziri takribani 20 na wafanyabiashara ni wakati pekee wa Watanzania na wa Vietnam, kuimarisha ushirikiano uliokuwepo kwa zaidi ya miaka 50 sasa kuhakikisha uhusiano unaleta maendeleo kwa pande zote.
“Ziara hii ni muafaka kwetu sisi watanzania kujenga uhusiano mzuri na nchi ya Vietnam ili kuweza kujifunza na sisi tuweze kufikia lengo letu la kuwa nchi ya kipato cha kati,” alisema. Pamoja na hayo, Rais Magufuli alisema katika mazungumzo yake na Rais wa Vietnam alipata mwaliko wa kutembelea nchi hiyo mwakani. “Kwa kweli mwaliko huu nimeupokea na ninajisikia kuthaminiwa na kuheshimiwa sana,” alisema.
Kwa upande wake, Rais Sang alisema anajisikia fahari kuona uhusiano kati ya Tanzania na nchi yake unaimarika. Alisisitiza kuwa uhusiano na ushirikiano huo utaleta maendeleo ya dhati baina ya nchi hizo mbili. Alipongeza serikali kupambana dhidi ya umasikini kwa kusisitiza kuwa inafanya vizuri kiuchumi kwani ni miongoni mwa nchi za Afrika ambazo uchumi wake unakua kwa kasi.
“Kama rafiki wa karibu tunavutiwa na maendeleo yenu hasa katika kupambana na umasikini lakini pia ukuaji wa kasi wa uchumi wenu. Katika mazungumzo yetu na Rais Magufuli tumezungumzia masuala mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya kilimo, biashara na viwanda,” alisema rais huyo. Aidha, alisema uhusiano wa nchi hizo mbili ni wa muda mrefu, kwani pamoja na umbali wa kijiografia Tanzania ni nchi ya kwanza Afrika kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Vietnam.
Alisema ziara hiyo ni moja ya njia za kudumisha na kuboresha zaidi uhusiano na ushirikiano baina ya nchi hizo mbili. Rais huyo alisema kwenye mazungumzo yake na Magufuli, wamekubaliana kushirikiana katika maeneo yatakayonufaisha nchi zote. Maeneo hayo ni kilimo, biashara, viwanda na mawasiliano. Pia walisaini mikataba ya kutowatoza kodi mara mbili wawekezaji na wafanyabiashara wanaowekeza katika nchi hizo.
Aidha Rais huyo alisema katika kikao chake na Rais Magufuli pamoja na mawaziri wa nchi zote mbili wamekubaliana kuanzisha tume ya pamoja itakayosimamia masuala ya uhusiano na ushirikiano baina ya nchi hizo mbili. Aidha marais hao walizungumzia masuala ya kimataifa ambapo wote kwa pamoja walikubaliana suala la kuhakikisha amani na utulivu linapewa kipaumbele na mataifa yote duniani.
“Tulikubaliana kuwa nchi zote zina wajibu wa kuhakikisha suala la amani linapewa kipaumbele, ikiwemo na mataifa ya kimataifa kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha na kutuliza vurugu zinazoibuka katika nchi mbalimbali,” alisema. Alisisitiza kuwa amemwalika Rais Magufuli kutembelea Vietnam wakati wowote. Tayari Marais wastaafu Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete, walishafanya ziara katika nchi hiyo wakati wa utawala wao.
Rais Sang aliyeongozana na ujumbe wa watu 51 ataendelea kuwepo nchini kwa ajili ya kumalizia ziara yake katika maeneo mbalimbali, ikiwemo kutembelea Mamlaka ya Ukanda Maalum wa Uwekezaji (EPZA).

Wawekezaji wa Vietnam waalikwa

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewaalika wawekezaji kutoka Vietnam na kuwahakikishia kuwa Tanzania ni nchi inayoheshimu uwekezaji na kwamba Serikali imesaini mikataba mbalimbali ya kupinga kutaifisha mali za wawekezaji.
Majaliwa aliyasema hayo Dar es Salaam jana kwenye kongomano baina ya ujumbe wa Tanzania na Rais wa Vietnam, Truong Tan San aliyeongozana na ujumbe wake katika ziara ya siku nne nchini na wafanyabiashara wa Tanzania.
Waziri Majaliwa alisema Tanzania ni nchi yenye mazingira mazuri ya uwekezaji katika nyanja mbalimbali na kusisitiza kwamba wanaotaka kuwekeza nchini wanafurahia mazingira hayo na uwepo wa dhamana ya mitaji waliyowekeza.
“Ukiwekeza Tanzania una uhakika wa usalama wa mtaji na uwekezaji wako kwa sababu nchi imesaini mikataba mbalimbali ya kupinga utaifishaji mali za wawekezaji na kuhimiza uwekezaji wa kigeni katika mazingira salama na yenye amani,” alisema Majaliwa.
Alisema kila mara nchi imekuwa ikiboresha sheria na kuimarisha ushirikishwaji wa sekta binafsi ili kuchochea mazingira ya uwekezaji kwa lengo la kuimarisha uchumi na kuinua maisha ya wananchi wake.
Akizungumzia soko mara baada ya kuwekeza nchini, Waziri Majaliwa alisema, wawekezaji wanaowekeza nchini wana uhakika wa masoko ya zaidi ya watu milioni 300 waishio Mashariki na Kusini mwa Afrika, ambao hufurahia kuwepo kwa nchi katika Jumuiya kama ya SADC na EAC.
Aidha, nchi zaidi ya sita ambazo hazina bahari hutegemea bandari ya Tanzania kufanya biashara na masoko katika eneo hilo. Akizungumzia uwekezaji kutoka nje ya nchi, Waziri Majaliwa alisema serikali imekua ikiboresha mazingira ya uwekezaji na hiyo imeongeza uwekezaji kutoka nje.
Alisema mfano mzuri ni uwekezaji wa Kampuni ya Viettel Tanzania Ltd, ambao ni wawekezaji kutoka Vietnam

YASEMAVYO MAGAZETI TAR 10/03/2016Thursday, March 10, 2016 :

 Ndalichako: Vyeti Vya Form Six Vilivyo Katika Mfumo wa GPA Havitabadilishwa Kwenda Division 
 https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiX6Mpq_jhttge5s_qQ1IGLkZJQQ3rcc4-vMPf4F9RYAlyxZo0TfcZmhTh_qD0pydiPFlvxCDd7Ue7nDP44QYTPhiBB_JcGSDLRYSkKWBR4927_SkyXg6V8FF9VVhyphenhyphenqN8VvdRr46J63BgK5/s1600/ndalichako.jpg
Serikali imesema haina mpango wa kubadili vyeti vya wanafunzi waliomaliza kidato cha sita mwaka jana kutoka kwenye mfumo wa alama za GPA kwenda Divisheni.

Msimamo huo wa serikali, umetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako.
 
Amesema serikali haina mpango wa kubadili mfumo huo wa vyeti kwani tangu awali wanafunzi walisoma kwa mfumo wa GPA na vyeti vilitoka kwa mfumo huo.

“Hatuwezi kubadili vyeti hivyo, isipokuwa vimehitajika kwa ajili ya marekebisho madogo ambayo Katibu Mkuu wa Wizara, aliyasema lakini siyo kubadili kwenda mfumo wa divisheni,” alisema.

Februari mwaka huu, Baraza la Taifa la Mitihani (Necta), lilitangaza kusitishwa kwa ugawaji wa vyeti vya kidato cha sita kwa wanafunzi waliohitimu mwaka 2015, huku likiagiza kuwa vile vilivyokwisha gawanywa kwa wahitimu hao vinatakiwa kurejeshwa kwenye chombo hicho.

Hata hivyo, Katibu Mtendaji wa Necta, Dk, Charles Msonde, hakubainisha marekebisho ambayo wanatakiwa kuyafanya kwenye vyeti hivyo na badala yake kudai baraza linataka kujiridhisha na baadhi ya vitu.

Hatua hiyo ya kubadili vyeti hivyo iliibua utata mkubwa, huku baadhi ya wadau wakiwamo maofisa elimu, wakihisi Necta huenda inalenga kuvibadili vyeti hivyo kutoka kwenye mfumo wa wastani wa alama (GPA), kwenda kwenye ule wa jumla (division).

Atupwa Jela Miaka 7 kwa Kumkata Mkewe Sehemu za Siri Ili Apate Mali

Kikoti blog

Mkazi wa Kata ya Mbugani, Manispaa ya Tabora, Mashaka Maziku (60) amehukumiwa kifungo cha miaka saba jela kwa kosa la kumkata sehemu za siri mkewe kwa imani za kishirikina ili apate mali.

Hakimu Joctan Rushwela alisema jana kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Tabora imeridhishwa na ushahidi uliotolewa upande wa mashtaka.

Hakimu Rushwela alisema anamhukumu mshtakiwa huyo kwenda jela ili iwe fundisho kwa wengine wanaokuwa na tamaa ya kujipatia mali kwa njia za kishirikina.

Awali wakili wa Serikali, Idd Mgeni alidai kuwa mshtakiwa huyo na mganga wa jadi, walitenda kosa hilo kati ya Oktoba 29 na Novemba 2, 2014 katika eneo la Kazaroho Kata ya Mbugani, Manispaa ya Tabora.

Wakati wa tukio hilo, ilidaiwa kuwa Maziku aliambiwa na mganga huyo ambaye ni mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, Kahele Paul kwamba akipeleka sehemu za siri za mkewe atapata Sh5milioni.

Alidai baada ya kupewa ushauri huo, alimchukua mkewe na kwenda kumnywesha pombe ili aweze kutimiza ukatili huo.

Alidai baada ya kunywa pombe nyingi, alichukua kisu na kumkata sehemu za siri mkewe na kuzihifadhi kwenye mfuko wa suruali yake na kutoweka. 
Alidai kwa mujibu wa mashahidi wanne, mwanamke huyo alikuwa akipiga kelele kutokana na maumivu makali aliyopata huku akivuja damu nyingi.