ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Alhamisi, 30 Aprili 2015

KUTOKA MAGAZETINI LEO TAR 30/04/2015

Mwanafunzi auawa baada ya kukutwa na barua ya mapenzi


Serikali yatangaza mikakati ya kuimarisha shilingi

WAZIRI wa Fedha, Saada Mkuya Salum amesema kupatikana kwa mikopo ya kibiashara yenye thamani ya dola za Marekani milioni 500 zitasaidia kupunguza kushuka kwa thamani ya Shilingi ya Tanzania.
Akizungumzia mwenendo wa mfumko wa bei wakati wa kuwasilisha Mapendekezo ya Mfumo wa Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka 2015/16 kwa wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jana jijini Dar es Salaam, alisema serikali imekuwa ikiweka mikakati kadhaa ya kuhakikisha sarafu inaimarika.
“Napenda kuwahakikishia wabunge na wananchi kuwa Serikali inachukua hatua muhimu za kuhakikisha thamani ya Shilingi inaendelea kuimarika,” alisema.
Alisema maeneo ambayo wamepanga kutumia ni kuimarisha maeneo maalumu ya kuzalisha bidhaa za kuuza nje na maeneo maalumu ya uwekezaji kiuchumi.
“Watanzania wazitumie fursa hizi ili kuongeza mauzo nje sambamba na kupunguza uagizaji wa bidhaa na huduma zisizo za lazima kutoka nje,” alisema.
Mkuya alisema kumekuwapo na sababu kadhaa za kutetereka kwa thamani ya Shilingi ya Tanzania ambazo ni kuwapo na mapato kidogo yanayotokana na mauzo ya nje kwa wastani wa mapato yanayoweza kugharamia asilimia kati ya 60 na 70 ya mahitaji kutoka nje ya nchi.
Alisema pia kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia hali ambayo imeathiri mapato yatokanayo na dhahabu kwa kiasi kikubwa.
”Kwa mfano mwaka unaoishia Januari 2015, mapato kutokana na dhahabu yalishuka kwa takribani dola za Marekani milioni 334 na hivyo kupunguza ahueni ambayo ingeweza kupatikana kwa ongezeko la mauzo ya bidhaa za viwanda pamoja na utalii."
Alisema pia ongezeko la mahitaji ya dola kwa ajili ya malipo ya gawio nje ya nchi kwa baadhi ya makampuni binafsi, ucheleweshaji wa fedha za mikopo ya kibiashara (kiasi cha dola milioni 536) katika kipindi cha miezi tisa ya kwanza ya mwaka wa fedha 2014/15.
“Matarajio yetu ni kwamba fedha kutoka nje zitaingia siku za karibuni kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha. Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda na Biashara, Luhaga Mpina alisema sababu ya kuporomoka kwa sarafu kunatokana na Benki Kuu na serikali kwa ujumla kutokuwa na udhibiti wa matumizi ya fedha za kigeni. “Nchi nyingi zinadhibiti sana matumizi ya dola, lakini hapa kwetu unaweza kwenda kwenye duka la kubadilishia hela, hupewi risiti na hakuna udhibiti wote,” alisema.
Mpina alisema kuna haja sasa kampuni nne ambazo zina matumizi makubwa ya dola ya Tanesco, MSD, Tanroads na waagizaji wa mafuta kununua dola BoT badala ya kununua kwenye benki ya biashara.

Msajili avionya vyama vya siasa

Last Updated on 30 April 2015
MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amevionya vyama vya siasa na wanasiasa wasikamiane na kukomoana kwa sababu, kufanya hivyo hakujengi demokrasia wala kuisaidia nchi.
Badala yake, amevielekeza viimarishe uelewano na kusaidiana, ili kujenga Tanzania yenye amani na utulivu, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea katika uchaguzi mkuu.
Akizungumza Dar es Salaam jana wakati wa kufungua mkutano wa siku mbili wa mashauriano ya jinsi ya kufikia na kuutekeleza uchaguzi mkuu wa Oktoba kwa amani, Jaji Mutungi alisema ameona dalili za wanasiasa na vyama vyao kukamiana.
Mkutano huo umeandaliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwa ushirikiano na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), litakalotoa ripoti ya utendaji wa ofisi hiyo katika mkutano utakaoendelea leo jijini humo, lengo likiwa kuishauri namna ya kuboresha utendaji.
Katika mkutano huo unaohusisha wadau mbalimbali wa siasa nchini, wakiwemo wawakilishi wa vyama 22 vya siasa na taasisi tofauti, Jaji Mutungi alisema, “Tanzania ina tunu ya amani, hivyo wanasiasa wasijaribu kuivuruga kwa kuendesha siasa zisizo zingatia dhana ya demokrasia ya kweli.
Alionya kuwa uzembe wowote utakaofanywa na wanasiasa au vyama vyao unaweza kuiathiri nchi, na kuwafanya Watanzania wajute kuingia katika mfumo wa siasa za vyama vingi.
Jaji huyo alisema pia kuwa amejiridhisha kuwa baadhi ya vyama vya siasa vimeshindwa kuielewa vizuri dhana ya demokrasia ya vyama vingi, hivyo kuwa na fikra za kukamiana na kukomoana, ambazo kwa namna yoyote, hazimsaidii Mtanzania.
“Ninawaomba wanasiasa na vyama vyenu muelewe kuwa, harakati zote za kufikia uchaguzi mkuu zinapaswa kuwa na lengo la kumtafuta kiongozi atakayeiendesha nchi ifikie maendeleo. “...Sote tunajenga nyumba moja ambayo ni nchi yetu, hivyo, hatupaswi kugombania fito kwa mtindo utakaosababisha nyumba isijengwe,”Jaji Mutungi alisisitiza na kuongeza kuwa mikutano kama hiyo itaendelea kuwepo ili kupanua uelewa wa wanasiasa juu ya dhana hiyo ya demokrasia ya vyama vingi. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Philipe Poinsot aliipongeza Tanzania kwa kuendelea kukuza demokrasia ya vyama vingi na kuwakumbusha wanasiasa na vyama vyao kuwa wao ndio wenye dhamana ya kuilinda demokrasia hiyo pamoja na amani iliyopo.
Alisema,”katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu, Tanzania imekuwa na vuguvugu linaloweza kusababisha hali ya sintofahamu kwa wananchi, jambo ambalo si jema hasa endapo nchi inaelekea kwenye uchaguzi mkuu na matukio muhimu ya upigaji kura ya maoni.
Katika hatua nyingine, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Idara ya Sayansi ya Siasa, Dk Benson Bana alisema, ingawa demokrasia ya vyama vingi inaonesha kuanza kufanikiwa nchini, vyama vya siasa bado vinaitekeleza vikiwa na dhana ya utengano.
back to top  


MICHEZO NA BURUDANI
  

Pluijm: Natamani kikubwa zaidi ya ubingwa VPL


NA JENNIFER ULLEMBO, DAR ES SALAAM
KOCHA Mkuu wa timu ya Yanga, Hans Van Der Pluijm, amesema ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara ni kitu kidogo sana kwake, kwani bado nafsi yake inatamani kitu kikubwa zaidi kwa klabu hiyo.
Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 4-1dhidi ya Polisi Morogoro katika mchezo wa ligi uliofanyika Jumatatu Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam na kufikisha jumla ya pointi 53, zilizopelekea klabu hiyo kutangazwa kuwa mabingwa wapya msimu huu.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Pluijm alisema tayari amejipatia sifa hapa nyumbani kwa kuipa ubingwa Yanga, akieleza sasa ni wakati wa kuonyesha maajabu kimataifa.
Pluijm alisema kuelekea katika mchezo wa marudiano dhidi ya Etoile Du Sahel ya Tunisia, tayari mikakati yake yote ambayo alijiwekea kabla ya mchezo huo wa marudiano imekamilika.
“Ubingwa wa ligi ni kitu kidogo kwangu, hapa kinachotakiwa kufanyika sasa ni kuelekeza nguvu zote kimataifa,” alisema Pluijm.
Mholanzi huyo alisema wakati anakabidhiwa kikosi cha Yanga, alijiwekea dhamira ya kuwapa ubingwa na hilo limeweza kutimia.
“Nilipokuwa naingia mkataba nilisema lazima timu ninayoifundisha ichukue kombe la ligi, bado nataka kuishuhudia ikifanya kitu kikubwa zaidi,” alisema Pluijm.
Timu hiyo inatarajiwa kuvaana na Etoile du Sahel katika mchezo wa raundi ya pili ya michuano ya Kombe la Shirikisho, baada ya kutoka sare ya bao 1-1 kwenye mchezo wa awali uliofanyika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam wiki mbili zilizopita. Tayari timu hiyo imetua Tunisia kwa ajili ya mchezo huo.(SOURCE: MTANZANIA)

Hakuna maoni: