ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Ijumaa, 17 Aprili 2015

Kutoka magazetini leo Tar 17/04/2015

TUHUMA ZA UFISADI: SITTA AMJIBU ZITTO KABWE

FRIDAY, APRIL 17 2015, 0 : 0


WAZIRI wa Uchukuzi, Bw. Samuel Sitta, amekanusha tuhuma za Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo, Bw. Zitto Kabwe kuhusu ujenzi wa Bandari ya Mwambani, mkoani Tanga na reli kutoka eneo la banda kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC.

Alisema kuwa, gharama za mradi huo zilizotajwa na Bw. Kabwe sh. trilioni 54 kwa miradi yote miwili akidai unatekelezwa na
watuhumiwa wa sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow ni kubwa kuliko fedha zilizochotwa katika akaunti hiyo.

Bw. Sitta aliyasema hayo Dar es Salaam jana alipozungumza na waandishi wa habari juu ya ufisadi uliotajwa na Bw. Kabwe kuhusu mradi huo akiuita Mwambani Economic Corridor (MWAPORC) akimtaka Waziri mwenye dhamana afanye uchunguzi na kuchukua hatua.

Alisema hakuna ufisadi wowote katika mradi huo bali
kilichotokea, watu mbalimbali wa sekta binafsi wanabuni
miradi wanayoitafutia mitaji na kutafuta vibali serikalini.

Aliongeza kuwa, Mkurugenzi wa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited, Bw. James Rugemarila na washirika wengine, wamekuwa wakijaribu kupata wabia ili kuendeleza mradi wa Mwambani Port Development (Mwapopo).

"Lengo lao ni zuri ili tuweze kupata biashara kwa maana ya
mizigo inayotoka DRC, Serikali haihusiki kutoa pesa yoyote ila
tunasubiri walete mapendekezo yao tuyatazame," alisema.

Alisema hatua ya awali haitakuwa rahisi kusema mradi huo unakwenda sambamba na ujenzi wa reli ya kati kwani lazima ziangaliwe faida ambazo zitapatikana.

"Tulipata ushauri na kuona kuwa, sehemu kubwa ya reli itakuwa upande wa DRC, kama kuna kundi linataka kushawishi mradi huu ni vyema wakaenda kuanzia huko ili waunganishe na reli ambazo tulishaziweka katika mradi.

"Hakuna ufisadi wala hakuna mradi ambao Serikali imeingia ubia ukiacha mradi wetu wa reli...huu wa kina Rugemarila wacha waendelee kuutekeleza, wataleta mapendekezo nasi tutatazama kama tunavyotazama mengine," alisema.

Bw. Sitta aliongeza kuwa, mradi wa MWAPORC una wawekezaji wawili na hakuna ufisadi wowote bali Bw.Rugemalira amependekeza mradi.

Hivi karibuni, Bw. Kabwe akiwa Mjini Mafinga mkoani Iringa, alidai kushangazwa na hatua ya Serikali kuwapatia kazi ya ujenzi wa bandari hiyo unaoenda sambamba na ujenzi wa reli watuhumiwa wa Escrow.

Alidai watuhumiwa hao walipewa kazi hiyo kupitia mradi wa MWAPORC ambao utagharimu sh. trilioni 54 kukiwa hakuna utaratibu wa utangazaji zabuni kisheria.

Alisema mradi huo umepewa kwa Kampuni ya VIP inayomilikiwa na Bw. Rugemalira akimtaka Bw. Sitta, afanye uchunguzi kuhusu mradi huo na achukue hatua kwa kile alichodai kuna utapeli unaofanyika.

Mabehewa mabovu

Akizungumzia uchunguzi unaohusu ununuzi wa mabehewa mabovu   katika Kampuni ya Reli Tanzania (TRL), Bw. Sitta amesema amewasimamisha kazi viongozi wakuu watano wa kampuni hiyo kwa ajili ya kukamilisha uchunguzi huo.

Alisema tangu Januari mwaka huu, Serikali imekuwa ikifanyia kazi tuhuma zinazohusiana na mabehewa hayo yaliyoagizwa kutoka nchini India na TRL.

Aliwataja waliosimamishwa kuwa ni Mkurugenzi Mtendaji wa TRL, Kipallo Kisamfu, Mhandisi Mkuu wa Mitambo wa kampuni hiyo, Ngosomwile Ngosomiles, Mhasibu Mkuu Mbaraka Mchopa, Mkaguzi Mkuu wa Ndani, Jasper Kisiraga na Meneja Mkuu wa Manunuzi, Fedinard Soka.

Aliongeza kuwa, uchunguzi wa awali umebaini mabehewa mengi kati ya yaliyoagizwa yana kasoro ambapo kulikuwa na uzembe kwenye uagizwaji na ufuatiliaji kiwandani yalipokuwa yakitengenezwa na uzembe katika kuendelea kuyapokea pamoja na ubovu wake kujulikana.

"Aprili 13, mwaka huu, nilishtushwa kugundua kinyume na taarifa za awali na masharti ya mkataba wa ununuzi wa mabehewa hayo kuwa malipo yangefanyika kwa awamu ambapo cha kushangaza mabehewa mabovu malipo yake yamefanyika kwa asilimia 100," alisema Bw. Sitta.

Alisema malipo hayo yalifanyika kinyume na masharti ya mkataba, hivyo utekelezaji wa mkataba huo una dalili za
hujuma kwa TRL na kwa nchi si uzembe.

Alisisitiza kuwa, wakati viongozi hao wakiwa wamesimamishwa ili kupisha uchunguzi, ameiagiza Bodi ya Wakurugenzi ikae kikao cha dharura leo na kuteua watumishi wenye sifa ya kukaimu nafasi hizo.

Sakata la Kaimu Mkurugenzi TPA

Bw. Sitta alizungumzia sakata la Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari nchini (TPA) Madeni Kipande ambaye amesimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali dhidi yake.

Alisema baada ya Serikali kupokea tuhuma hizo, Februari 16, mwaka huu, alisimamishwa kazi kwa muda ili kupisha
uchunguzi wa tuhuma hizo.

"Serikali imeamua kumrejesha Bw. Kipande Idara Kuu ya Utumishi ili aweze kupangiwa majukumu mengine, Bw. Awadhi Massawe ataendelea kukaimu nafasi ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA hadi Serikali itakapopata mwafaka, "alisema Bw. Sitta.

Aliongeza kuwa, hatua hiyo inatokana na kudhihirika kwa utawala mbovu aliosababisha manung'uniko mengi miongoni mwa wateja, wadau wa bandari na mgawanyo mkubwa wa wafanyakazi.


CCM: NDESAMBURO AMESOMA ALAMA ZA NYAKATI

FRIDAY, APRIL 17 2015, 0 : 0


SIKU chache baada ya Mbunge wa Moshi Mjini, mkoani Kilimanjaro, Bw. Philemon Ndesamburo (CHADEMA), kutangaza azma yake ya kutogombea kiti hicho katika Uchaguzi Mkuu ujao, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeibuka na kusema mbunge huyo amesoma alama za nyakati.

Bw. Ndesamburo ambaye amedumu kwa vipindi vitatu mfululizo katika nafasi hiyo, alitoa msimamo wa kutogombea tena kwenye mkutano wa adhara uliofanyika Kata ya Bondeni, mjini Moshi, Aprili 14, mwaka huu akidai kumkabidhi mikoba yake Meya
wa Manispaa ya Moshi, Bw. Japhari Michael.

Katibu wa CCM mkoani humo, Bw. Deogratius Rutta, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari Mjini Moshi akisema kuwa, hatua ya Ndesamburo kutangaza kutogombea nafasi hiyo ni ishara ya kusoma alama za nyakati kwani wangemgaragaza vibaya.

"Nampongeza Ndesamburo kwa kusoma alama za nyakati na amefanya vizuri kutokana na umri wake ili asije kuondoka kwa aibu ya kuangushwa vibaya na CCM...wakazi wa Moshi wamechoshwa na ahadi zisizotekelezeka," alisema.

Aliongeza kuwa, Bw. Ndesamburo ameshtuka mapema kuyakimbia mapambano kwani kipindi chake cha uongozi kilikuwa kiishie mwaka huu katika Uchaguzi Mkuu ujao.

"Amewadanganya wakazi wa Moshi kwa muda mrefu hivyo mwaka huu hawakuwa tayari kumpa ubunge bali wapo tayari kumpa mgombea wa CCM," alisema.

Alisema hatua ya kumkabidhi mikoba yake Bw. Michael ni kumuuzia mbuzi kwenye gunia baada ya kuona hawezi tena kuchaguliwa jimboni humo kutokana na kuboronga katika
kipindi chake chote alichoshikilia kiti hicho.

"Uamuzi wa Ndesamburo, utawafanya wanachama wengi wa CHADEMA kurudi CCM kwani kile kilichowapeleka huko hawajakipata, ahadi walizopewa ni hewa," alisema.

Bw. Rutta alisema CCM kimejipanga vyema katika Uchaguzi Mkuu ujao kwa kunyakua majimbo yote yanayoshikiliwa na upinzani mkoani humo yakiwemo Rombo, Hai na Vunjo.

Aliongeza kuwa, CHADEMA hakuna demokrasia ya kweli kwani ni chama cha familia ndio maana Bw. Ndesamburo ameamua kumtangaza mrithi wake badala ya kutoa nafasi kwa wanachama kugombea nafasi hiyo.

"Michael naye kasoma alama za nyakati kwani Kata ya Bomambuzi anayoiongoza kwa sasa, asingeweza kuchaguliwa, kwani CCM imejipanga kuichukua kwa kishindo," alisema.

Alisema CCM kinatumia demokrasia ya wazi na kuwataka wanachama wao, kujitokeza ili kuwania nafasi mbalimbali za uongozi akitumia fursa hiyo kuwaonya wanachama
wasaliti akitaka wabadilike ili wasifukuzwe.

KITAIFA

VIONGOZI CCM WATAHDHARISHWA

FRIDAY, APRIL 17 2015, 0 : 0


MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa(NEC) ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) Wilaya ya Kibaha Mjini Rugemalira Rutatina,amewataka viongozi wa CCM kuacha tabia ya kuwachagulia wananchi kiongozi kwani kufanya hivyo inaleta madhara ya kumpata kiongozi ambaye hana msaada kwa wananchi.

Aidha, Rutatina alisema kuwa kitendo hicho kinasababisha majimbo mengi ya CCM kuangukia mikononi mwa wapinzani na kwamba hali hiyo lazima ikomeshwe mara moja kinyume na hapo hatua za kinidhamu zitachukuliwa.

Rutatina,alitoa kauli hiyo jana  Mjini Kibaha wakati akizungumza na wanachama wa CCM,viongozi na wananchi  katika mkutano wake uliofanyika Mtaa wa Sheli ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kuimarisha chama hicho.

Alisema kuwa,wapo baadhi ya viongozi wa CCM ambao wamekuwa na tabia ya kuwakumbatia watu na kuwalazimisha wananchi wamchague kiongozi ambaye hawampendi jambo ambalo linaathiri mwenendo mzima wa CCM.

Rutatina, alisema umefika wakati wa viongozi wa CCM kuheshimu maamuzi ya wananchi ya kumchagua mtu wanayemtaka kwani hali hiyo itakiletea heshima CCM kwa kupata kiongozi makini mwenye kujali maendeleo ya wananchi wake.

"Lazima tuwe makini tunapofika muda wa uchaguzi,tuache wananchi wafanye maamuzi yao ya kumchagua kiongozi wanayemtaka kutoka ndani ya CCM na si kuwachagulia mtu," alisema Rutatina.

Aidha, Rutatina alitumia nafasi hiyo kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika Uchaguzi Mkuu wa urais,ubunge na udiwani unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu.

Rutatina amehaidi kushirikiana na wananchi wa Kibaha Mjini katika kutatua  changamoto mbalimbali za kimaendeleo zilizopo maeneo wilayani humo ambapo moja ya changamoto hizo ni maji,barabara,afya na umeme.

Hata hivyo,Rutatina alitumia nafasi hiyo kuwasihi wananchi kujitokeza katika kuipigia kura katiba muda utakapofika ili waweze kupata haki zao na kwamba bila hivyo hakutakuwa na mafanikio ya kimaendeleo

KIMATAIFA

-----------------------------------------------------------------

MAHAKAMA YAZIMA VINU VYA NYUKLIA JAPAN

THURSDAY, APRIL 16 2015, 0 : 0
MAHAKAMA moja nchini Japan imetoa amri ya kuzuia kufunguliwa upya kwa kiwanda kimoja cha nyuklia kilichopo pwani ya Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.Vinu 50 vya nyuklia vya Japan vilifungwa mwaka 2011 kufuatia mkasa wa Fukushima; lakini Serikali ya Waziri Mkuu, Sinzo Abe, inashinikiza vinu h...  

MHUDUMU WA NDEGE ASAHAULIKA KWENYE BUTI, YATUA KWA DHARURA

WEDNESDAY, APRIL 15 2015, 0 : 0
NDEGE ya Shirika la Ndege la Alaska ililazimika kutua kwa dharura baada ya mhudumu wa ndege kugundulika alikuwa amesahaulika ndani ya sehemu ya kupakia mizigo ya ndege hiyo. Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana nchini humo zinaelezea kuwa ndege hiyo ya kubeba abiria 170 imelazimika kutua baad...  

SHULE ZAFUNGULIWA SIERRA LEONE

  • WEDNESDAY, APRIL 15 2015, 0 : 0
    SHULE zilizokuwa zimefungwa nchini Sierra Leone tangu Julai mwaka uliopita kutokana na mlipuko wa ugonjwa hatari wa Ebola zimefunguliwa.Kwa mujibu wa Taarifa zilizotolewa kupitia Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), zimeeleza kuwa shirika la Afya Duniani limethibitisha kufunguliwa kwa s...  

NIGERIA YAADHIMISHA KUTEKWA NYARA WANAFUNZI

  • WEDNESDAY, APRIL 15 2015, 0 : 0
    MAELFU ya watu nchini Nigeria wamejitokeza kuadhimisha mwaka mmoja tangu kutekwa nyara kwa wanafunzi 200 katika mji wa Chibok na wapiganaji wa Boko Haramu.Maadhimisho hayo yalifanyika jana huko Nigeria ambapo ni mwaka mmoja umepita tangu wapiganaji wa Boko Haramu kuteka nyara zaidi ya wanafu...  

17 WAUAWA KATIKA SHAMBULIZI LA AL-SHABAAB

  • WEDNESDAY, APRIL 15 2015, 0 : 0
    WATU 17 wameripotiwa kuuawa na wengine 20 kujeruhiwa vibaya wakati wanamgambo wa Kiislamu wa Al-Shabaab waliposhambulia majengo ya Wizara ya Elimu mjini Mogadishu, Somalia.Kwa mujibu wa BBC wavamizi hao walilipua bomu lililotegwa ndani ya gari kwenye ukuta wa jengo hilo kabla ya wavamizi kui...  

UNHCR YAAHIDI KUSHIRIKIANA NA KENYA

  • WEDNESDAY, APRIL 15 2015, 0 : 0
    SHIRIKA la Umoja wa Mataifa linalosimamia wakimbizi- UNHCR limesema kuwa liko tayari kufanya kazi na Serikali ya Kenya ili kuhakikisha kuwa sheria za Kenya zinafuatwa kikamilifu katika kambi ya wakimbizi ya Dadaab karibu na mpaka wake na Somalia.Shirika hilo limeitaka Serikali ya Kenya kufik...  
  • SOURCE. MAJIRA



Hakuna maoni: