ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumamosi, 11 Juni 2016

Amuua mkewe, achoma moto nyumba mbili

Imeandikwa na Samson Chacha, Tarime
MKAZI wa kitongoji cha Nyabirama kijiji cha Matongo Nyamongo, Tarafa ya Ingwe, wilayani Tarime mkoani Mara Wambura Mrimi (50) amepata kipigo kutoka kwa wananchi na kulazwa akiwa na hali mbaya kwa tuhuma za kumchinja kwa kumkata shingo mke wake Maria Maningo (38) na kuchoma nyumba zake mbili baada ya kumhusisha mke wake na imani za kishirikina.
Mrimi amelazwa katika Hospitali ya wilaya Tarime akiwa chini ya ulinzi mkali. Kamanda wa Polisi Tarime Rorya, ACP Andrew Satta alisema kuwa tukio hilo la mauaji lilifanyika June 8, mwaka huu katika kitongoji cha Nyabirama, kijiji cha Matongo Nyamongo baada ya kutokea ugomvi kati ya mke na mume.
Alisema Mrimi alikuwa akimtuhumu mke wake Maria kuwa anamloga na kushiriki katika mambo ya kishirikina lakini mke alikuwa akikana tuhuma hizo. Kamanda Satta alisema wakati wakigombana mtuhumiwa Mrimi alikuwa na panga mkononi ndipo alipomkata shingo mkewe na kuacha panga limeninginia na kisha kuchoma nyumba zao mbili zilizokuwa zimeezekwa kwa nyasi.
Thamani ya nyumba hizo na mali zilizoteketea hazikuweza kufahamika mara moja. Alisema wananchi ambao ni wakazi wa kitongoji hicho cha Nyabirama walisikitishwa na kitendo hicho na kuamua kupiga yowe na kumkamata mtuhumiwa na kuanza kumshambulia kwa mawe hadi alipookolewa na polisi waliofika mapema eneo hilo na kumchukua kwa gari akiwa hajitambui.
Kamanda Sitta alisema mtuhumiwa huyo alikimbizwa hospitalini hapo kwa matibabu zaidi na yupo chini ya ulinzi wa Polisi hadi sasa na mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Kituo cha Afya Nyamongo kwa uchunguzi zaidi wakati ukisubiri kukabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya maziko.

Hakuna maoni: