ILULA IRINGA TANZANIA

ILULA IRINGA TANZANIA
KIKOTI.COM BLOG - ILULA IRINGA TANZANIA / 0769694963 .......................................

Jumatano, 25 Mei 2016

MAGAZETINI:#Bilioni 15/- kukabiliana na ukosefu wa ajira

Imeandikwa na Theopista Nsanzugwanko, Dodoma
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama amesema serikali imetenga Sh bilioni 15 kwa ajili ya kuongeza ujuzi na kukabiliana na ukosefu wa ajira nchini.
Mhagama alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Josephine Chagula (CCM) aliyetaka kujua mpango wa serikali kuwawezesha vijana wa mkoa wa Geita kuwapatia ujuzi ili waweze kujiajiri na kuajiriwa.
Akijibu swali hilo, Mhagama alisema katika bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwenye bajeti yake ya mwaka huu, wametenga fedha hizo ili kuweza kuajiriwa katika viwanda vilivyopo na vitakavyoanzishwa.
Aidha, katika swali hilo la nyongeza, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alisema kila mkoa una Shirika la viwanda vidogo (Sido) ambalo linatakiwa kutoa elimu ya ujasiriamali bila malipo.
Hivyo alitaka kupeleka vijana ili wapate elimu bure itakayowawezesha kupata ujuzi wa kujiajiri na kuajiriwa.
Katika swali lake la msingi, Chagula alitaka kujua mpango wa Serikali kujenga viwanda vya kusindika mazao katika mkoa wa Geita, kutokana na vijana wengi kukosa ajira na hasa ikizingatiwa sehemu kubwa ya uchumi wa mkoa huo unategemea kilimo.
Akijibu swali hilo, Mwijage alisema kwa kutambua umuhimu wa viwanda katika kuchangia ukuaji wa uchumi nchini, wizara hiyo kupitia makakati unganishi wa Maendeleo ya viwanda kwa lengo la kuhamasisha wananchi na wadau kuwekeza katika kuanzisha viwanda.
Alisema katika mkakati huo unazitaka Mamlaka za serikali za Mitaa na Miji kutenga maeneo ya uwekezaji katika viwanda hadi ngazi ya kata ambayo yatatumika kuanzisha mitaa ya viwanda kwa kutumia malighafi zinazopatikana katika maeneo husika.

Hakuna maoni: